101 - 129
101. Na katika
mabedui walio jirani zenu wamo wanaafiki; na katika wenyeji wa Madina pia wapo
walio bobea katika unaafiki. Wewe huwajui. Sisi tunawajua. Tutawaadhibu mara
mbili, kisha watarudishwa kwenye adhabu kubwa.
102. Na wengine
walikiri dhambi zao, wakachanganya vitendo vyema na vingine viovu. Asaa
Mwenyezi Mungu akapokea toba zao. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe
Mwenye kurehemu.
103. Chukua
sadaka katika mali zao, uwasafishe na uwatakase kwazo, na uwaombee rehema.
Hakika maombi yako ni utulivu kwao. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia Mwenye
kujua.
104. Je! Hawajui
ya kwamba Mwenyezi Mungu anapokea toba ya waja wake, na anazikubali sadaka, na
kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa kupokea toba na Mwenye kurehemu?
105. Na sema: Tendeni vitendo. Na Mwenyezi Mungu, na Mtume
wake, na Waumini wataviona vitendo vyenu. Na mtarudishwa kwa Mwenye kujua siri
na dhaahiri; naye atakuambieni mliyo kuwa mkiyatenda.
106. Na wapo wengine wanangojea amri ya Mwenyezi Mungu -
ama atawaadhibu au atawasamehe. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua Mwenye
hikima.
107. Na wapo walio jenga msikiti kwa ajili ya madhara na ukafiri
na kuwafarikisha Waumini, na pa kuvizia kwa walio mpiga vita Mwenyezi Mungu na
Mtume wake hapo kabla. Na bila ya shaka wataapa kwamba: Hatukukusudia ila wema
tu. Na Mwenyezi Mungu anashuhudia kuwa wao ni waongo.
108. Usisimame kwenye msikiti huo kabisa. Msikiti ulio
jengwa juu ya msingi wa uchamngu tangu siku ya mwanzo unastahiki zaidi wewe
usimame ndani yake. Humo wamo watu wanao penda kujitakasa. Na Mwenyezi Mungu
anawapenda wanao jitakasa.
109. Je! Mwenye kuweka msingi wa jengo lake juu ya kumcha
Mwenyezi Mungu na radhi zake ni bora au mwenye kuweka msingi wa jengo lake juu
ya ukingo wa shimo linalo burugunyika, na likaburugunyika naye katika Moto wa
Jahannamu? Na Mwenyezi Mungu hawaongoi watu madhaalimu.
110. Na jengo lao hilo walilo lijenga litakuwa sababu ya
kutia wasiwasi nyoyoni mwao mpaka nyoyo zao hizo zikatike vipande vipande. Na
Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua Mwenye hikima.
111. Hakika Mwenyezi Mungu amenunua kwa Waumini nafsi zao
na mali zao kwa kuwa wao watapata Pepo. Wanapigana katika Njia ya Mwenyezi
Mungu - wanauwa na wanauwawa. Hii ni ahadi aliyo jilazimisha kwa Haki katika
Taurati na Injili na Qur'ani. Na nani atimizae ahadi kuliko Mwenyezi Mungu?
Basi furahini kwa biashara yenu mliyo fanya naye. Na huko ndiko kufuzu kukubwa,
112. (Kwa) wanao tubia, wanao abudu, wanao himidi, wanao
kimbilia kheri, wanao rukuu, wanao sujudu, wanao amrisha mema na wanao kataza
maovu, na wanao linda mipaka ya Mwenyezi Mungu. Na wabashirie Waumini.
113. Haimpasii Nabii na wale walio amini kuwatakia msamaha
washirikina, ijapo kuwa ni jamaa zao, baada ya kwisha bainika kuwa hao ni watu
wa Motoni.
114. Wala haikuwa Ibrahim kumtakia msamaha baba yake ila
kwa sababu wa ahadi aliyo fanya naye. Lakini ilipo mbainikia kwamba yeye ni
adui ya Mwenyezi Mungu, alijiepusha naye. Hakika Ibrahim alikuwa mwingi wa
kuomba, mnyenyekevu, mvumilivu.
115. Na haiwi kwa Mwenyezi Mungu kuwahisabu watu kuwa
wamepotea baada ya kwisha waongoza mpaka awabainishie ya kujiepusha nayo.
Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua kila kitu.
116. Hakika Mwenyezi Mungu anao ufalme wa mbingu na ardhi;
huhuisha na hufisha. Nanyi hamna Mlinzi wala Msaidizi isipo kuwa Mwenyezi
Mungu.
117. Mwenyezi Mungu amekwisha pokea toba ya Nabii na
Wahajiri na Ansari walio mfuata katika saa ya dhiki, pale baada ya kukaribia
nyoyo za baadhi yao kugeuka. Basi akapokea toba yao, kwani hakika Yeye kwao wao
ni Mpole na ni Mwenye kuwarehemu.
118. Na pia wale watatu walio achwa nyuma hata dunia
wakaiona dhiki juu ya ukunjufu wake, na nafsi zao zikabanika, na wakayakinika
kuwa hapana pa kumkimbia Mwenyezi Mungu isipo kuwa kwake Yeye. Kisha
akawaelekea kwa rehema yake ili nao waendelee kutubu. Hakika Mwenyezi Mungu
ndiye Mwenye kupokea toba na Mwenye kurehemu.
119. Enyi mlio amini! Mcheni Mwenyezi Mungu, na kuweni
pamoja na wakweli.
120. Haiwafalii watu wa Madina na Mabedui walio jirani zao
kubakia nyuma wasitoke na Mtume, wala kujipendelea nafsi zao kuliko yeye. Hayo
ni kwa kuwa hakiwapati kiu, wala machofu, wala njaa, kwa ajili ya Njia ya
Mwenyezi Mungu, wala hawendi mahali panapo waghadhibisha makafiri, wala
hakiwapati chochote kutokana na maadui, ila huandikiwa kuwa ni kitendo chema.
Hakika Mwenyezi Mungu haupotezi ujira wa wanao fanya mema.
121. Wala hawatoi cha kutoa kidogo wala kikubwa, wala
hawalivuki bonde, ila huandikiwa, ili Mwenyezi Mungu awalipe bora ya waliyo
kuwa wakiya- tenda.
122. Wala haiwafalii Waumini kutoka wote. Lakini kwa nini
hawatoki baadhi katika kila kundi miongoni mwao, wakajifunze vyema Dini, na
kisha waje kuwaonya wenzao watakapo warejea, ili wapate kujihadharisha?
123. Enyi mlio amini! Piganeni na wale makafiri walio
karibu yenu, na wakute ugumu kwenu. Na jueni ya kwamba Mwenyezi Mungu yu pamoja
na wacha- Mngu.
124. Na inapo teremshwa Sura wapo miongoni mwao wasemao: Ni
nani miongoni mwenu Sura hii imemzidishia Imani? Ama wale walio amini
inawazidishia Imani, nao wanafurahi.
125. Ama wale wenye maradhi katika nyoyo zao, basi
inawazidishia uovu juu ya uovu wao; na wanakufa hali ni makafiri.
126. Je! Hawaoni ya kwamba wanatiwa mtihanini kila mwaka
mara moja au mara mbili? Kisha hawatubu, wala hawakumbuki.
127. Na ikiteremka Sura hutazamana wao kwa wao, (kama
kwamba wanasema:) Je! Yuko mtu anakuoneni? Kisha hugeukilia mbali. Mwenyezi
amezigeuza nyoyo zao kwa kuwa hao ni watu wasio fahamu.
128. Hakika amekwisha kujieni Mtume kutokana na nyinyi
wenyewe; yanamhuzunisha yanayo kutaabisheni; anakuhangaikieni sana. Kwa Waumini
ni mpole na mwenye huruma.
129. Basi wakigeuka, wewe sema: Mwenyezi Mungu
ananitosheleza. Hapana mungu isipokuwa Yeye tu. Mimi namtegemea Yeye, na Yeye
ndiye Mola Mlezi wa Kiti Kikuu cha Enzi.
|