Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 15. SURATUL HIJR
    • 51 - 99
Previous - Next

Click here to hide the links to concordance

51 - 99

51. Na uwape khabari za wageni wa Ibrahim.

52. Walipo ingia kwake na wakasema: Salama! Yeye akasema: Hakika sisi tunakuogopeni.

53. Wakasema: Usiogope. Sisi tunakubashiria kijana mwenye ujuzi.

54. Akasema: Mnanibashiria nami uzee umenishika! Basi kwa njia gani mnanibashiria?

55. Wakasema: Tunakubashiria kwa haki; basi usiwe miongoni mwa wanao kata tamaa.

56. Akasema: Na nani anaye kata tamaa na rehema ya Mola wake Mlezi ila wale walio potea?

57. Akasema: Hebu nini amri yenu, enyi wajumbe?

58. Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwa kaumu ya wakosefu!

59. Isipo kuwa walio mfuata Luut'i. Bila ya shaka sisi tutawaokoa hao wote.

60. Ila mkewe. Tunakadiria huyo atakuwa miongoni watao bakia nyuma.

61. Basi wale wajumbe walipo fika kwa Luut'i,

62. Alisema (Luut'i): Hakika nyinyi ni watu msio juulikana.

63. Wakasema: Bali sisi tumekuletea yale waliyo kuwa wakiyafanyia shaka.

64. Na tumefika kwako kwa Haki, na hakika sisi tunasema kweli.

65. Basi ondoka na ahli zako usiku ungalipo, nawe ufuate nyuma yao, wala yeyote kati yenu asigeuke nyuma. Na mwende mnapo amrishwa.

66. Na tukamfunulia hukumu hiyo, ya kwamba hata wa mwisho wao hao ikifika asubuhi atakuwa kesha katiliwa mbali.

67. Na wakaja watu wa mji ule nao furahani.

68. Akasema: Hakika hawa wageni wangu, basi msinifedheheshe.

69. Na mcheni Mwenyezi Mungu, wala msinihizi.

70. Wakasema: Sisi hatukukukataza usimkaribishe yeyote?

71. Akasema: Hawa binti zangu, ikiwa nyinyi ni watendaji.

72. Naapa kwa umri wako! Hakika hao walikuwa katika ulevi wao, wakihangaika ovyo.

73. Ukelele ukawatwaa wakipambaukiwa.

74. Na tukaigeuza nchi juu chini, na tukawanyeshea mvua ya mawe ya udongo wa Motoni.

75. Hakika katika hayo zipo ishara kwa waaguzi.

76. Na miji hii ipo kwenye njia inayo pitiwa.

77. Hakika katika hayo ipo ishara kwa Waumini.

78. Na hakika watu wa Kichakani walikuwa wenye kudhulumu.

79. Kwa hivyo tukawaadhibu. Na nchi mbili hizi ziko kwenye njia ilio wazi.

80. Na bila ya shaka wakaazi wa Hijr waliwakanusha Mitume.

81. Na tuliwapa ishara zetu, nao wakazipuuza.

82. Nao walikuwa wakichonga majumba katika milima kwa amani.

83. Basi ukelele ukawatwaa asubuhi.

84. Hayakuwafaa waliyo kuwa wakiyachuma.

85. Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyomo ndani yake ila kwa ajili ya Haki. Na hakika Kiyama kitafika. Basi samehe msamaha mzuri.

86. Hakika Mola wako Mlezi ndiye Muumbaji Mjuzi.

87. Na tumekupa Aya saba zinazo somwa mara kwa mara, na .

88. Usivitumbulie macho yako vitu tulivyo waneemesha makundi fulani kati yao, wala usiwahuzunikie. Na wainamishie bawa lako (la huruma) Waumini.

89. Na sema: Hakika mimi ni mwonyaji mwenye kubainisha.

90. Kama hivyo tuliwateremshia walio gawa,

91. Ambao wakaifanya Qur'ani vipande vipande.

92. Basi Naapa kwa Mola wako Mlezi! Tutawahoji wote,

93. Kwa waliyo kuwa wakiyatenda.

94. Basi wewe yatangaze uliyo amrishwa, na jitenge na washirikina.

95. Hakika Sisi tunatosha kukukinga na wanao kejeli.

96. Hao wanao fanya kuwa pamoja na Mwenyezi Mungu yupo mungu mwingine. Basi, watakuja jua!

97. Na Sisi tunajua kwa hakika kuwa wewe kifua chako kinaona dhiki kwa hayo wayasemayo.

98. Basi mtakase Mola wako Mlezi kwa kumhimidi, na uwe miongoni wanao msujudia.

99. Na muabudu Mola wako Mlezi mpaka ikufikie Yakini.

 




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License