1 - 50
1. SUBHANA, Ametakasika aliye mchukua mja wake usiku mmoja
kutoka Msikiti Mtukufu mpaka Msikiti wa Mbali, ambao tumevibariki vilivyo
uzunguka, ili tumuonyeshe baadhi ya Ishara zetu. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia
na Mwenye kuona.
2. Na tukampa Musa Kitabu, na tukakifanya uwongofu kwa Wana
wa Israili. (Tukawambia): Msiwe na mtegemewa ila Mimi!
3. Enyi kizazi tuliyo wachukua pamoja na Nuhu! Hakika yeye
alikuwa mja mwenye shukrani.
4. Na tukawahukumia Wana wa Israili katika Kitabu kwamba:
Hakika nyinyi mtafanya fisadi katika nchi mara mbili, na kwa yakini mtapanda
kiburi, kiburi kikubwa.
5. Basi itapo fika ahadi ya kwanza yake tutakupelekeeni
waja wetu wa kali kwa vita. Watakuingilieni ndani ya majumba. Na hii ilikuwa
ahadi iliyo timizwa.
6. Kisha tukakurudishieni nguvu zenu dhidi yao, na
tukakusaidieni kwa mali na wana, na tukakujaalieni mkawa wengi zaidi.
7. Basi mkifanya wema, mnajifanyia wema nafsi zenu. Na
mkifanya ubaya, mnajifanyia wenyewe. Na ikifika ahadi ya mwisho ili waziharibu
nyuso zenu, na waingie Msikitini kama walivyo ingia mara ya kwanza, na waharibu
kila walicho kiteka kwa uharibifu mkubwa.
8. Huenda Mola wenu Mlezi akakurehemuni. Na mkirudia na Sisi
tutarudia. Na tumeifanya Jahannamu kuwa ni gereza kwa ajili ya makafiri.
9. Hakika hii Qur'ani inaongoa kwenye ya yaliyo nyooka
kabisa, na inawabashiria Waumini ambao wanatenda mema ya kwamba watapata malipo
makubwa.
10. Na yakwamba wale wasio iamini Akhera tumewaandalia
adhabu chungu.
11. Na mwanaadamu huomba shari kama vile aombavyo kheri,
kwani mwanaadamu ni mwenye pupa.
12. Na tumefanya usiku na mchana kuwa ishara mbili. Tena
tukaifuta ishara ya usiku, na tukaifanya ishara ya mchana ni yenye mwangaza ili
mtafute fadhila itokayo kwa Mola wenu Mlezi, na mpate kujua idadi ya miaka na
hisabu. Na kila kitu tumekifafanua waziwazi.
13. Na kila mtu tumemfungia a'mali yake shingoni mwake. Na
Siku ya Kiyama tutamtolea kitabu atakacho kikuta kiwazi kimekunjuliwa.
14. Ataambiwa: Soma kitabu chako! Nafsi yako inakutosha leo
kukuhisabu.
15. Anaye ongoka basi anaongoka kwa ajili ya nafsi yake. Na
anaye potea basi anapotea kwa khasara yake mwenyewe. Wala habebi mbebaji mzigo
wa mwengine. Wala Sisi hatuadhibu mpaka tumpeleke Mtume.
16. Na pindi tukitaka kuuteketeza mji huwaamrisha wale
wenye starehe na taanusi, lakini wao huendelea kutenda maovu humo. Basi hapo
kauli huthibiti juu ya mji huo, nasi tukauangamiza kwa maangamizo makubwa.
17. Na kaumu ngapi tumeziangamiza baada ya Nuhu! Na Mola
wako Mlezi anatosha kabisa kuwa ni Mwenye kuzijua na kuziona dhambi za waja
wake.
18. Anaye taka yapitayo upesi upesi, tutafanya haraka
kumletea hapa hapa tunayo yataka kwa tumtakaye. Kisha tumemwekea Jahannamu;
ataingia humo hali ya kuwa ni mwenye kulaumiwa na kufurushwa.
19. Na anaye itaka Akhera, na akazifanyia juhudi a'mali
zake, naye ni Muumini, basi hao juhudi yao itakuwa ni ya kushukuriwa.
20. Wote hao tunawakunjulia - hawa na hao - katika neema za
Mola wako Mlezi. Wala neema za Mola wako Mlezi hazizuiliki.
21. Angalia vipi tulivyo wafadhili baadhi yao kuliko
wenginewe. Na hakika Akhera ni yenye daraja kubwa zaidi na fadhila kubwa zaidi.
22. Usimfanye mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu,
usije ukawa wa kulaumiwa uliye tupika.
23. Na Mola wako Mlezi ameamrisha kuwa msimuabudu yeyote
ila Yeye tu, na wazazi wawili muwatendee wema. Mmoja wao akifikia uzee, naye
yuko kwako, au wote wawili, basi usimwambie hata: Ah! Wala usiwakemee. Na sema
nao kwa msemo wa hishima.
24. Na uwainamishie bawa la unyenyekevu kwa kuwaonea
huruma. Na useme: Mola wangu Mlezi! Warehemu kama walivyo nilea utotoni.
25. Mola wenu anajua kabisa yaliyo nyoyoni mwenu. Ikiwa
nyinyi mtakuwa wema, basi hakika Yeye ni Mwenye kuwaghufiria wanao tubia kwake.
26. Na mpe aliye jamaa yako haki yake, na masikini, na
msafiri; wala usitumie ovyo kwa fujo.
27. Hakika wabadhirifu ni ndugu wa Mashet'ani. Na Shet'ani
ni mwenye kumkufuru Mola wake Mlezi.
28. Na ikiwa unajikurupusha nao, nawe unatafuta rehema ya
Mola wako Mlezi unayo itaraji, basi sema nao maneno laini.
29. Wala usiufanye mkono wako kama ulio fungwa shingoni
mwako, wala usiukunjue wote kabisa, utabaki ukilaumiwa muflisi.
30. Hakika Mola wako Mlezi humkunjulia riziki amtakaye, na
humpimia amtakaye. Hakika Yeye kwa waja wake ni Mwenye kuwajua na kuwaona.
31. Wala msiwauwe wana wenu kwa kuogopa umasikini. Sisi
tunawaruzuku wao na nyinyi. Hakika kuwaua hao ni khatia kubwa.
32. Wala msikaribie uzinzi. Hakika huo ni uchafu na njia
mbaya.
33. Wala msiuwe nafsi ambayo Mwenyezi Mungu amekataza isipo
kuwa kwa haki. Na aliye uliwa kwa kudhulumiwa basi tumempa madaraka mrithi
wake. Lakini asipite mpaka katika
kuuwa. Kwani yeye
anasaidiwa.
34. Wala
msiyakaribie mali ya yatima, isipo kuwa kwa njia iliyo bora, mpaka afike
utuuzimani. Na timizeni ahadi. Kwa hakika ahadi itasailiwa.
35. Na timizeni kipimo mpimapo. Na pimeni kwa mizani zilizo
sawa. Hayo ni wema kwenu na khatimaye ndio bora.
36. Wala usiyafuate usiyo na ujuzi nayo. Hakika masikio, na
macho, na moyo - hivyo vyote vitasailiwa.
37. Wala
usitembee katika ardhi kwa maringo. Hakika wewe huwezi kuipasua ardhi wala
kufikia urefu wa milima.
38. Haya
yote ubaya wake ni wenye kuchukiza kwa Mola wako Mlezi.
39. Haya
ni katika hikima alizo kufunulia Mola wako Mlezi. Wala usimweke pamoja na
Mwenyezi Mungu mungu mwengine, usije ukatupwa katika Jahannamu ukilaumiwa na
kufurushwa.
40. Je!
Mola wenu Mlezi amekuteulieni wavulana, na Yeye akawafanya Malaika ni banati
zake? Kwa hakika nyinyi mnasema usemi mkubwa.
41. Na
tumekwisha bainisha katika Qur'ani hii ili wapate kukumbuka. Lakini
haikuwazidisha ila kuwa mbali nayo.
42. Sema:
Lau kuwa wangeli kuwa pamoja naye miungu mingine kama wasemavyo, basi wangeli
tafuta njia ya kumfikia Mwenye Kiti cha Enzi.
43.
Subhanahu Wa Taa'la, Ametakasika na Ametukuka juu kabisa na hayo wanayo yasema.
44.
Zinamtakasa zote mbingu saba na ardhi na vyote viliomo ndani yake. Na hapana
kitu ila kinamtakasa kwa sifa zake. Lakini nyinyi hamfahamu kutakasa kwake.
Hakika Yeye ni Mpole na Mwenye maghfira.
45. Na unapo soma Qur'ani tunaweka baina yako na wale wasio
iamini Akhera pazia linalo wafunika.
46. Na tunaweka vifuniko juu ya nyoyo zao wasije
wakaifahamu, na tunaweka kwenye masikio yao uziwi. Na unapo mtaja katika
Qur'ani Mola wako Mlezi peke yake, basi wao hugeuka nyuma wakenda zao.
47. Sisi tunajua vyema kabisa sababu wanayo sikilizia
wanapo kusikiliza, na wanapo nong'ona. Wanapo sema hao madhaalimu: Nyinyi
hamumfuati isipo kuwa mtu aliye rogwa.
48. Tazama vipi wanavyo kupigia mifano. Basi wamepotea. Kwa
hivyo hawawezi kuipata njia.
49. Na walisema: Je! Tutapo kuwa mifupa na mapande yaliyo
vurugika, tutafufuliwa kwa umbo jipya?
50. Sema: Kuweni hata mawe na chuma.
|