51 - 100
51. Au umbo lolote mnalo liona kubwa katika vifua vyenu. Watasema:
Nani atakaye turudisha tena? Sema: Yule yule aliye kuumbeni mara ya kwanza!
Watakutikisia vichwa vyao, na watasema: Lini hayo? Sema: A'saa yakawa karibu!
52. Siku atakapo kuiteni, na nyinyi mkamuitikia kwa
kumshukuru, na mkadhani kuwa hamkukaa ila muda mdogo tu.
53. Waambie waja wangu waseme maneno mazuri, maana Shet'ani
huchochea ugomvi baina yao. Hakika Shet'ani ni adui aliye dhaahiri kwa
mwanaadamu.
54. Mola wenu Mlezi anakujueni vilivyo. Akipenda atakurehemuni,
na akipenda atakuadhibuni. Na hatukukutuma ili uwe mlinzi juu yao.
55. Na Mola wako Mlezi anawajua vilivyo waliomo mbinguni na
katika ardhi. Na hakika tumewafadhilisha baadhi ya Manabii kuliko wengine; na
Daudi tulimpa Zaburi.
56. Sema: Waombeni hao mnao wadaia badala yake Yeye.
Hawawezi kukuondoleeni madhara, wala kuyaweka pengine.
57. Hao wanao waomba, wao wenyewe wanatafuta njia ya
kwendea kwa Mola wao Mlezi - hata miongoni mwao walio karibu mno - na
wanataraji rehema zake na wanaikhofu adhabu yake. Hakika adhabu ya Mola wako
Mlezi yafaa kutahadhari nayo.
58. Na hapana mji wowote ila Sisi tutauteketeza kabla ya
Siku ya Kiyama, au tutaupa adhabu kali. Haya yamekwisha andikwa katika Kitabu.
59. Na hapana kinacho tuzuia kupeleka miujiza ila ni kuwa watu
wa zamani waliikanusha. Na tuliwapa Wathamudi ngamia jike kuwa ni Ishara iliyo
dhaahiri, lakini walidhulumu kwaye. Nasi hatupeleki Ishara ila kwa ajili ya
kuhadharisha.
60. Na tulipo kwambia: Hakika Mola wako Mlezi amekwisha
wazunguka hao watu. Na hatukuifanya ndoto tulio kuonyesha ila ni kuwajaribu
watu, na mti ulio laaniwa katika Qur'ani. Na tunawahadharisha, lakini
haiwazidishii ila uasi mkubwa.
61. Na pale tulipo waambia Malaika: Msujudieni Adam.
Wakamsujudia isipo kuwa Iblisi. Akasema: Je! Nimsujudie uliye muumba kwa
udongo?
62. Akasema: Hebu nambie khabari ya huyu uliye mtukuza juu
yangu. Ukiniakhirisha mpaka Siku ya Kiyama, hapana shaka nitawaangamiza dhuriya
zake wasipo kuwa wachache tu.
63. Akasema Mwenyezi Mungu: Ondokelea mbali! Atakaye
kufuata katika wao, basi Jahannamu itakuwa ndiyo malipo yenu, malipo ya
kutimia.
64. Na wachochee uwawezao katika wao kwa sauti yako, na
wakusanyie jeshi lako la wapandao farasi na waendao kwa miguu. Na shirikiana
nao katika mali na wana, na waahidi. Na Shet'ani hawapi ahadi ila ya udanganyifu.
65. Hakika wewe huna mamlaka juu ya waja wangu. Na Mola
wako Mlezi anatosha kuwa ni wa kutegemewa.
66. Mola wenu Mlezi ndiye anaye kuendesheeni marikebu
katika bahari ili mtafute katika fadhila zake. Hakika Yeye ni Mwenye
kukurehemuni nyinyi.
67. Na inapo kufikieni taabu katika bahari, hao mnao waomba
wanapotea, isipo kuwa Yeye tu. Na anapo kuvueni mkafika nchi kavu, mnageuka.
Ama mwanaadamu ni mwingi wa kukanusha.
68. Je! Mmeaminisha ya kuwa hatakudidimizeni upande wowote
katika nchi kavu, au kwamba hatakuleteeni tufani la kokoto? Kisha msipate wa
kumtegemea.
69. Au mmeaminisha ya kuwa hatakurudisheni humo mara
nyengine na kukupelekeeni kimbunga cha upepo akakuzamisheni kwa mlivyo kufuru,
na kisha msipate wa kukunusuruni nasi.
70. Na hakika tumewatukuza wanaadamu, na tumewapa vya
kupanda nchi kavu na baharini, na tumewaruzuku vitu vizuri vizuri, na
tumewafadhilisha kwa fadhila kubwa kuliko wengi miongoni mwa tulio waumba.
71. Siku tutapo waita kila kikundi cha watu kwa mujibu wa
wakifuatacho - basi atakaye pewa kitabu chake kwa mkono wake wa kulia, basi hao
watasoma kitabu chao wala hawatadhulumiwa hata chembe.
72. Na aliye kuwa hapa kipofu, basi atakuwa kipofu Akhera,
na atakuwa aliye ipotea zaidi Njia.
73. Na hakika walikaribia kukushawishi uache tuliyo
kufunulia ili utuzulie mengineyo. Na hapo ndio wangeli kufanya rafiki.
74. Na lau kuwa hatukukuweka imara ungeli karibia
kuwaelekea kidogo.
75. Hapo basi bila ya shaka tungeli kuonjesha adhabu
mardufu ya uhai, na adhabu mardufu ya kifo. Kisha usinge pata mtu wa kukunusuru
nasi.
76. Na walitaka kukukera ili uitoke nchi. Na hapo wao wasingeli
bakia humo ila kwa muda mchache tu.
77. Huo ndio mwendo kwa Mitume tulio watuma kabla yako.
Wala hupati mabadiliko katika mwendo wetu.
78. Shika Sala jua linapo pinduka mpaka giza la usiku, na
Qur'ani ya al fajiri. Hakika Qur'ani ya alfajiri inashuhudiwa daima.
79. Na amka usiku kwa ibada; ni ziada ya sunna khasa kwako
wewe. Huenda Mola wako Mlezi akakunyanyua cheo kinacho sifika.
80. Na sema: Mola wangu Mlezi! Niingize muingizo mwema, na
unitoe kutoka kwema. Na unipe nguvu zinazo toka kwako zinisaidie.
81. Na sema: Kweli imefika, na uwongo umetoweka. Hakika
uwongo lazima utoweke!
82. Na tunateremsha katika Qur'ani yaliyo ni matibabu na
rehema kwa Waumini. Wala hayawazidishii madhaalimu ila khasara.
83. Na mwanaadamu tunapo mneemesha hugeuka na kujitenga
kando. Na inapo mgusa shari hukata tamaa.
84. Sema:
Kila mmoja anafanya kwa namna yake. Na Mola wenu Mlezi anajua aliye ongoka
katika njia.
85. Na
wanakuuliza khabari za Roho. Sema: Roho ni katika mambo ya Mola wangu Mlezi.
Nanyi hamkupewa katika ilimu ila kidogo tu.
86. Na tungeli penda tungeli yaondoa tuliyo kufunulia.
Kisha usingeli pata mwakilishi wa kukupigania kwetu kwa haya.
87. Isipo kuwa iwe rehema itokayo kwa Mola wako Mlezi.
Hakika fadhila yake kwako ni kubwa.
88. Sema: Wangeli kusanyika watu na majini ili walete mfano
wa hii Qur'ani basi hawaleti mfano wake, hata wakisaidiana wao kwa wao.
89. Na hakika tumewaeleza watu katika hii Qur'ani kwa kila
mfano. Lakini watu wengi wanakataa isipo kuwa kukanusha tu.
90. Na walisema: Hatutakuamini mpaka ututimbulie chemchem
katika ardhi hii.
91. Au uwe na kitalu cha mitende na mizabibu, na
utupitishie mito kati yake ikimiminika.
92. Au utuangushie mbingu vipande vipande kama ulivyo dai;
au utuletee Mwenyezi Mungu na Malaika uso kwa uso.
93. Au uwe na nyumba ya dhahabu, au upae mbinguni. Wala
hatutaamini kupaa kwako mpaka ututeremshie kitabu tukisome. Sema: Subhana
Rabbi, Ametakasika Mola wangu Mlezi! Kwani mimi ni nani isipo kuwa ni
mwanaadamu na Mtume?
94. Na nini kilicho wazuilia watu kuamini ulipo wajia
uwongofu isipo kuwa walisema: Je! Mwenyezi Mungu humtuma mwanaadamu kuwa ni
Mtume?
95. Sema: Ingeli kuwa duniani wapo Malaika wanatembea kwa
utulivu wao, basi bila ya shaka tungeli wateremshia Malaika kuwa ni Mtume wao.
96. Sema: Mwenyezi Mungu anatosha kuwa Shahidi baina yangu
na nyinyi. Hakika Yeye anawajua vyema waja wake na anawaona.
97. Na anaye mhidi Mwenyezi Mungu basi huyo ndiye aliye
hidika. Na anaye wapotoa basi huto wapatia walinzi badala yake. Na
tutawakusanya Siku ya Kiyama hali wakikokotwa juu ya nyuso zao, nao ni vipofu
na mabubu na viziwi. Na makaazi yao ni Jahannamu. Kila moto ukifanya kusinzia
tutazidi kuuchochea uwake kwa nguvu.
98. Hayo ni malipo yao kwa sababu walizikataa ishara zetu,
na wakasema: Hivyo tukisha kuwa mifupa na mapande yaliyo vurugika tutafufuliwa
kwa umbo jipya?
99. Kwani hawakuona ya kwamba Mwenyezi Mungu aliye umba
mbingu na ardhi ni Mwenye kuweza kuumba mfano wao? Na Yeye amewawekea muda usio
na shaka yoyote. Lakini madhaalimu hawataki ila ukafiri.
100. Sema: Lau kuwa nyinyi mnazimiliki khazina za rehema za
Mola wangu Mlezi, basi hapana shaka mngeli zuia kuzitumia kwa ajili ya kukhofu.
Na mwanaadamu tangu hapo tabia yake ni mchoyo!
|