51 - 98
51. Na mtaje
Musa katika Kitabu. Hakika yeye alikuwa ni mwenye kuchaguliwa, na alikuwa
Mtume, Nabii.
52. Na tulimwita
upande wa kulia wa mlima na tukamsogeza kunong'ona naye.
53. Nasi kwa
rehema zetu tukampa nduguye, Harun, awe Nabii.
54. Na mtaje
katika Kitabu Ismail. Bila ya shaka yeye alikuwa ni mkweli wa ahadi, na alikuwa
Mtume, Nabii.
55. Na alikuwa akiwaamrisha
watu wake Sala na Zaka, na alikuwa mbele ya Mola wake Mlezi mwenye kuridhiwa.
56. Na mtaje
katika Kitabu Idris. Hakika yeye alikuwa ni mkweli Nabii.
57. Na tulimuinua daraja ya juu.
58. Hao ndio alio waneemesha Mwenyezi Mungu miongoni mwa
Manabii katika uzao wa Adam, na katika uzao wa wale tulio wapandisha pamoja na
Nuhu, na katika uzao wa Ibrahim na Israil, na katika wale tulio waongoa na
tukawateuwa. Wanapo somewa Aya za Mwingi wa Rehema huanguka kusujudu na kulia.
59. Lakini wakaja baada yao walio wabaya, wakaacha Sala, na
wakafuata matamanio. Basi watakuja kuta malipo ya ubaya.
60. Isipo kuwa walio tubu, wakaamini, na wakatenda mema.
Hao, basi, wataingia Peponi wala hawatadhulumiwa chochote.
61. Bustani za milele alizo waahidi Rahmani waja wake
katika siri. Hakika ahadi yake hapana shaka itafika.
62. Humo hawatasikia upuuzi, ila Salama tu. Na watapata
humo riziki zao asubuhi na jioni.
63. Hiyo ndiyo Pepo tutayo warithisha katika waja wetu
walio kuwa wachamngu.
64. (Nao watasema:) Wala hatuteremki ila kwa amri ya Mola
wako Mlezi. Ni yake Yeye yaliyoko mbele yetu na yaliyoko nyuma yetu, na
yaliyomo katikati ya hayo. Na Mola wako Mlezi si mwenye kusahau.
65. Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na vilivyo baina yake.
Basi muabudu Yeye tu, na udumu katika ibada yake. Je, mnamjua mwenye jina kama
lake?
66. Na mwanaadamu husema: Hivyo, nitakapo kufa, ni kweli
nitafufuliwa niwe hai tena?
67. Je! Hakumbuki mwanaadamu ya kwamba tulimuumba kabla, na
hali hakuwa chochote?
68. Basi naapa kwa Mola wako Mlezi! Kwa yakini
tutawakusanya wao pamoja na mashet'ani; kisha tutawahudhurisha kuizunguka
Jahannamu, nao wamepiga magoti!
69. Kisha kwa yakini tutawatoa katika kila kundi wale
miongoni mwao walio zidi kumuasi Arrahmani, Mwingi wa Rahema..
70. Tena hakika Sisi tunawajua vyema zaidi wanao stahiki
kuunguzwa humo.
71. Wala hapana yeyote katika nyinyi ila ni mwenye
kuifikia. Hiyo ni hukumu ya Mola wako Mlezi ambayo lazima itimizwe.
72. Kisha tutawaokoa wale walio mchamngu; na tutawaacha
madhaalimu humo wamepiga magoti.
73. Na wanapo somewa Aya zetu zilizo wazi, walio kufuru
huwaambia walio amini: Lipi katika makundi mawili lenye cheo kizuri na lilio
bora barazani?
74. Na kaumu ngapi tuliziangamiza zilizo kuwa na mapambo
mazuri zaidi na wazuri zaidi kwa kuwatazama!
75. Sema: Walio katika upotofu basi Arrahmani Mwingi wa
Rahema atawapururia muda mpaka wayaone waliyo onywa - ama ni adhabu au ni Saa.
Hapo ndipo watapo jua ni nani mwenye makao mabaya na mwenye askari dhaifu.
76. Na Mwenyezi Mungu huwazidishia uwongofu wenye kushika
uwongofu. Na mema yenye kudumu ni bora katika malipo mbele ya Mola wako Mlezi
na yana mwisho mwema.
77. Je, umemwona aliye zikanya Ishara zetu na akasema: Kwa
hakika mimi nitapewa mali na wana!
78. Kwani yeye amepata khabari za ghaibu, au amechukua
ahadi kwa Arrahmani Mwingi wa Rehema?
79. Hasha!
Tutaandika anayo yasema, tutamkunjulia muda wa adhabu.
80. Na
tutamrithi hayo anayo yasema, na atatufikia mtupu peke yake!
81. Na
wamechukua miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu ili ati iwape nguvu.
82. Sivyo
kabisa! Wataikataa hiyo ibada yao, na watakuwa ndio dhidi yao.
83. Kwani
huoni ya kwamba tumewatuma mashet'ani kwa makafiri wawachochee kwa uchochezi?
84. Basi
usiwafanyie haraka. Sisi tunawahisabia idadi ya siku zao.
85. Siku
tutayo wakusanya wachamngu kuwapeleka kwa Arrahmani Mwingi wa Rehema kuwa ni
wageni wake.
86. Na
tukawachunga wakhalifu kuwapeleka Jahannamu hali ya kuwa wana kiu.
87.
Hawatakuwa na mamlaka ya uombezi ila wale walio chukua ahadi kwa Arrahmani
Mwingi wa Rehema..
88. Na wao
ati husema kuwa Arrahmani Mwingi wa Rehema ana mwana!
89. Hakika
mmeleta jambo la kuchusha mno!
90.
Zinakaribia mbingu kutatuka kwa hilo, na ardhi kupasuka, na milima kuanguka
vipande vipande.
91. Kwa
kudai kwao kuwa Arrahmani Mwingi wa Rehema ana mwana.
92. Wala
hahitajii Arrahmani Mwingi wa Rehema kuwa na mwana.
93. Hapana
yeyote aliomo mbinguni na ardhini ila atafika kwa Arrahmani Mwingi wa Rehema
kuwa ni mtumwa wake.
94. Yeye hakika
amewadhibiti na amewahisabu sawa sawa.
95. Na
kila mmoja katika wao atamfikia Siku ya Kiyama peke yake.
96. Hakika
walio amini na wakatenda mema Arrahmani Mwingi wa Rehema atawajaalia mapenzi.
97. Na
hakika tumeifanya nyepesi (Qur'ani) kwa ulimi wako, ili uwabashirie kwayo
wachamngu, na uwaonye kwayo watu wabishi.
98. Na kaumu
ngapi tumezihiliki kabla yao. Je! Unawaona hata mmoja katika wao au unasikia
hata mchakato wao? .
|