Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 19. SURAT MARYAM
    • 51 - 98
Previous - Next

Click here to hide the links to concordance

51 - 98

51. Na mtaje Musa katika Kitabu. Hakika yeye alikuwa ni mwenye kuchaguliwa, na alikuwa Mtume, Nabii.

52. Na tulimwita upande wa kulia wa mlima na tukamsogeza kunong'ona naye.

53. Nasi kwa rehema zetu tukampa nduguye, Harun, awe Nabii.

54. Na mtaje katika Kitabu Ismail. Bila ya shaka yeye alikuwa ni mkweli wa ahadi, na alikuwa Mtume, Nabii.

55. Na alikuwa akiwaamrisha watu wake Sala na Zaka, na alikuwa mbele ya Mola wake Mlezi mwenye kuridhiwa.

56. Na mtaje katika Kitabu Idris. Hakika yeye alikuwa ni mkweli Nabii.

57. Na tulimuinua daraja ya juu.

58. Hao ndio alio waneemesha Mwenyezi Mungu miongoni mwa Manabii katika uzao wa Adam, na katika uzao wa wale tulio wapandisha pamoja na Nuhu, na katika uzao wa Ibrahim na Israil, na katika wale tulio waongoa na tukawateuwa. Wanapo somewa Aya za Mwingi wa Rehema huanguka kusujudu na kulia.

59. Lakini wakaja baada yao walio wabaya, wakaacha Sala, na wakafuata matamanio. Basi watakuja kuta malipo ya ubaya.

60. Isipo kuwa walio tubu, wakaamini, na wakatenda mema. Hao, basi, wataingia Peponi wala hawatadhulumiwa chochote.

61. Bustani za milele alizo waahidi Rahmani waja wake katika siri. Hakika ahadi yake hapana shaka itafika.

62. Humo hawatasikia upuuzi, ila Salama tu. Na watapata humo riziki zao asubuhi na jioni.

63. Hiyo ndiyo Pepo tutayo warithisha katika waja wetu walio kuwa wachamngu.

64. (Nao watasema:) Wala hatuteremki ila kwa amri ya Mola wako Mlezi. Ni yake Yeye yaliyoko mbele yetu na yaliyoko nyuma yetu, na yaliyomo katikati ya hayo. Na Mola wako Mlezi si mwenye kusahau.

65. Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na vilivyo baina yake. Basi muabudu Yeye tu, na udumu katika ibada yake. Je, mnamjua mwenye jina kama lake?

66. Na mwanaadamu husema: Hivyo, nitakapo kufa, ni kweli nitafufuliwa niwe hai tena?

67. Je! Hakumbuki mwanaadamu ya kwamba tulimuumba kabla, na hali hakuwa chochote?

68. Basi naapa kwa Mola wako Mlezi! Kwa yakini tutawakusanya wao pamoja na mashet'ani; kisha tutawahudhurisha kuizunguka Jahannamu, nao wamepiga magoti!

69. Kisha kwa yakini tutawatoa katika kila kundi wale miongoni mwao walio zidi kumuasi Arrahmani, Mwingi wa Rahema..

70. Tena hakika Sisi tunawajua vyema zaidi wanao stahiki kuunguzwa humo.

71. Wala hapana yeyote katika nyinyi ila ni mwenye kuifikia. Hiyo ni hukumu ya Mola wako Mlezi ambayo lazima itimizwe.

72. Kisha tutawaokoa wale walio mchamngu; na tutawaacha madhaalimu humo wamepiga magoti.

73. Na wanapo somewa Aya zetu zilizo wazi, walio kufuru huwaambia walio amini: Lipi katika makundi mawili lenye cheo kizuri na lilio bora barazani?

74. Na kaumu ngapi tuliziangamiza zilizo kuwa na mapambo mazuri zaidi na wazuri zaidi kwa kuwatazama!

75. Sema: Walio katika upotofu basi Arrahmani Mwingi wa Rahema atawapururia muda mpaka wayaone waliyo onywa - ama ni adhabu au ni Saa. Hapo ndipo watapo jua ni nani mwenye makao mabaya na mwenye askari dhaifu.

76. Na Mwenyezi Mungu huwazidishia uwongofu wenye kushika uwongofu. Na mema yenye kudumu ni bora katika malipo mbele ya Mola wako Mlezi na yana mwisho mwema.

77. Je, umemwona aliye zikanya Ishara zetu na akasema: Kwa hakika mimi nitapewa mali na wana!

78. Kwani yeye amepata khabari za ghaibu, au amechukua ahadi kwa Arrahmani Mwingi wa Rehema?

79. Hasha! Tutaandika anayo yasema, tutamkunjulia muda wa adhabu.

80. Na tutamrithi hayo anayo yasema, na atatufikia mtupu peke yake!

81. Na wamechukua miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu ili ati iwape nguvu.

82. Sivyo kabisa! Wataikataa hiyo ibada yao, na watakuwa ndio dhidi yao.

83. Kwani huoni ya kwamba tumewatuma mashet'ani kwa makafiri wawachochee kwa uchochezi?

84. Basi usiwafanyie haraka. Sisi tunawahisabia idadi ya siku zao.

85. Siku tutayo wakusanya wachamngu kuwapeleka kwa Arrahmani Mwingi wa Rehema kuwa ni wageni wake.

86. Na tukawachunga wakhalifu kuwapeleka Jahannamu hali ya kuwa wana kiu.

87. Hawatakuwa na mamlaka ya uombezi ila wale walio chukua ahadi kwa Arrahmani Mwingi wa Rehema..

88. Na wao ati husema kuwa Arrahmani Mwingi wa Rehema ana mwana!

89. Hakika mmeleta jambo la kuchusha mno!

90. Zinakaribia mbingu kutatuka kwa hilo, na ardhi kupasuka, na milima kuanguka vipande vipande.

91. Kwa kudai kwao kuwa Arrahmani Mwingi wa Rehema ana mwana.

92. Wala hahitajii Arrahmani Mwingi wa Rehema kuwa na mwana.

93. Hapana yeyote aliomo mbinguni na ardhini ila atafika kwa Arrahmani Mwingi wa Rehema kuwa ni mtumwa wake.

94. Yeye hakika amewadhibiti na amewahisabu sawa sawa.

95. Na kila mmoja katika wao atamfikia Siku ya Kiyama peke yake.

96. Hakika walio amini na wakatenda mema Arrahmani Mwingi wa Rehema atawajaalia mapenzi.

97. Na hakika tumeifanya nyepesi (Qur'ani) kwa ulimi wako, ili uwabashirie kwayo wachamngu, na uwaonye kwayo watu wabishi.

98. Na kaumu ngapi tumezihiliki kabla yao. Je! Unawaona hata mmoja katika wao au unasikia hata mchakato wao?  .

 




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License