1 - 50
1. IMEWAKARIBIA watu hisabu yao, nao wamo katika mghafala
wanapuuza.
2. Hayawafikilii mawaidha mapya kutoka kwa Mola wao Mlezi
ila huyasikiliza na huku wanafanya mchezo.
3. Zimeghafilika nyoyo zao. Na wale walio dhulumu
hunong'onezana kwa siri: Ni nani ati huyu isipo kuwa ni binaadamu tu kama
nyinyi! Mnauwendea uchawi hali nanyi mnaona?
4. Alisema: Mola wangu Mlezi anayajua yasemwayo mbinguni na
katika ardhi. Na Yeye ni Mwenye kusikia Mwenye kujua.
5. Lakini wao walisema: Hizo ni ndoto za ovyo ovyo, bali
amezizua tu, bali huyo ni mtunga mashairi. Basi atuletee miujiza kama walivyo
tumwa wale wa mwanzo.
6. Hawakuamini kabla yao watu wa mji tulio uangamiza. Basi,
je, wataamini hawa?
7. Na kabla yako hatukuwatuma ila watu wanaume tulio wapa
wahyi (ufunuo). Basi waulizeni wenye ilimu ikiwa nyinyi hamjui.
8. Wala hatukuwafanya miili isiyo kula chakula, wala
hawakuwa wenye kuishi milele.
9. Kisha tukawatimizia miadi, na tukawaokoa wao na tulio
wataka, na tukawateketeza walio pita mipaka.
10. Na hakika tumekuteremshieni Kitabu ambacho ndani yake
yamo makumbusho yenu. Je! Hamzingatii?
11. Na mingapi katika miji iliyo kuwa ikidhulumu
tumeiteketeza, na tukawasimamisha baada yao watu wengine.
12. Basi walipo ihisi adhabu yetu, mara wakaanza kukimbia.
13. Msikimbie! Na rejeeni kwenye zile zile starehe zenu, na
maskani zenu, mpate kusailiwa!
14. Wakasema: Ole wetu! Hakika sisi tulikuwa madhaalimu.
15. Hakikuacha hicho kuwa kilio chao mpaka tukawafanya kama
walio fyekwa, wamezimika.
16. Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyo baina yao
kwa mchezo.
17. Kama tungeli taka kufanya mchezo tunge jifanyia Sisi
wenyewe, lau kwamba tungeli kuwa ni wafanyao mchezo.
18. Bali tunaitupa kweli juu ya uwongo ikauvunja na mara
ukatoweka. Na ole wenu kwa mnayo yazua.
19. Na ni vyake Yeye tu Mwenyezi Mungu vilivyomo mbinguni
na katika ardhi. Na walioko kwake hawafanyi kiburi wakaacha kumuabudu, wala
hawachoki.
20. Wanamtakasa usiku na mchana, wala hawanyong'onyei.
21. Au wamepata miungu katika ardhi inayo fufua?
22. Lau wangeli kuwamo humo miungu wengine isipo kuwa Mwenyezi
Mungu basi bila ya shaka hizo mbingu na ardhi zingeli fisidika. Subahana 'Llah
Ametakasika Mwenyezi Mungu, Bwana wa A'rshi (Kiti cha Enzi), na hayo wanayo
yazua.
23. Yeye hahojiwi kwa ayatendayo, na wao ndio wanao hojiwa
kwa wayatendayo.
24. Au wanawaabudu miungu mingine badala yake? Sema: Leteni
ushahidi wenu! Haya ni ukumbusho wa hawa walio nami, na ukumbusho wa walio
kabla yangu. Lakini wengi wao hawaijui kweli, na kwa hivyo wanapuuza.
25. Na hatukumtuma kabla yako Mtume yeyote ila tulimfunulia
ya kwamba hapana mungu isipo kuwa Mimi. Basi niabuduni Mimi tu.
26. Na wanasema: Arrahman, Mwingi wa Rehema, ana mwana! Subhanahu,
Ametakasika na hayo! Bali hao (wanao waita wana) ni watumwa walio tukuzwa.
27. Hawamtangulii kwa neno, nao wanafanya amri zake.
28. Anayajua yaliyo mbele yao na yaliyo nyuma yao. Wala
hawamwombei yeyote ila yule anaye mridhia Yeye, nao kwa ajili ya kumwogopa
wananyenyekea.
29. Na yeyote kati yao atakaye sema: Mimi ni mungu, badala
yake, basi huyo tutamlipa malipo yake Jahannamu. Hivyo ndivyo tuwalipavyo wenye
kudhulumu.
30. Je! Hao walio kufuru hawakuona kwamba mbingu na ardhi
zilikuwa zimeambatana, kisha Sisi tukazibabandua? Na tukajaalia kwa maji kila
kilicho hai? Basi je, hawaamini?
31. Na tukaweka
katika ardhi milima iliyo thibiti ili isiwayumbishe, na tukaweka humo njia pana
ili wapate kuongoka.
32. Na
tukaifanya mbingu kuwa dari iliyo hifadhiwa, lakini wanazipuuza Ishara zake.
33. Na Yeye
ndiye aliye umba usiku na mchana na jua na mwezi, vyote katika anga vinaogelea.
34. Nasi
hatukumjaalia mwanaadamu yeyote kabla yako kuwa na maisha ya milele. Basi je!
Ukifa wewe, wao wataishi milele?
35. Kila nafsi
itaonja mauti; na tunakujaribuni kwa mtihani wa shari na kheri. Na kwetu Sisi
mtarejeshwa.
36. Na wakikuona
walio kufuru hawakufanyi wewe ila ni kitu cha maskhara tu, (wakisema): Je!
Ndiye huyu anaye itaja miungu yenu? Na hali wao wanakataa kumkumbuka Arrahman,
Mwingi wa Rehema!
37. Mwanaadamu
ameumbwa na haraka. Nitakuonyesheni Ishara zangu. Basi msinihimize.
38. Na wanasema: Ahadi hii itatokea lini, ikiwa nyinyi
mnasema kweli?
39. Lau wangeli jua wale walio kufuru wakati ambao
hawatauzuia Moto kwenye nyuso zao wala migongo yao, na wala hawatanusuriwa!
40. Bali utawafikia kwa ghafla, na utawashitua na wala
hawataweza kuurudisha, wala hawatapewa muhula!
41. Na Mitume walio kabla yako walikwisha dhihakiwa. Kwa
hivyo wale walio wafanyia maskhara yaliwafika yale waliyo kuwa wakiyafanyia
dhihaka.
42. Sema: Nani anaye kulindeni usiku na mchana na Arrahmani
Mwingi wa Rehema? Bali wao wanapuuza kumkumbuka Mola wao Mlezi.
43. Au wao wanao miungu watao weza kuwakinga nasi? Hao
hawawezi kujinusuru nafsi zao, wala hawatalindwa nasi!
44. Bali tuliwastarehesha hawa na baba zao mpaka umri ukawa
mrefu kwao. Je, hawaoni ya kwamba Sisi tunaifikia ardhi tukiipunguza ncha zake?
Basi je! Hao ni wenye kushinda?
45. Sema: Mimi nakuonyeni kwa Wahyi. Na viziwi hawasikii
wito wanapo onywa.
46. Na wanapo guswa na mpulizo mmoja tu wa adhabu itokayo
kwa Mola wako Mlezi, bila ya shaka wao husema: Ole wetu! Hakika tulikuwa wenye
kudhulumu.
47. Nasi tutaweka mizani za uadilifu kwa Siku ya Kiyama.
Basi nafsi haitadhulumiwa kitu chochote. Hata ikiwa ni uzito wa chembe ya
khardali tutaileta. Nasi tunatosha kuwa washika hisabu.
48. Na kwa yakini tuliwapa Musa na Haaruni kipambanuzi, na
mwangaza, na makumbusho kwa wachamngu,
49. Ambao wanamkhofu Mola wao Mlezi faraghani, na
wanaiogopa Saa ya Kiyama.
50. Na haya ni makumbusho yaliyo barikiwa, tuliyo
yateremsha. Basi je! Mnayakataa?
|