51 - 78
51. Na wanao jitahidi kuzipinga Aya zetu hao ndio watu wa
Motoni.
52. Na hatukumtuma kabla yako Mtume wala Nabii ila anapo
soma, Shet'ani hutumbukiza katika masomo yake. Lakini Mwenyezi Mungu huyaondoa
anayo yatia Shet'ani; kisha Mwenyezi Mungu huzithibitisha Aya zake. Na Mwenyezi
Mungu ni Mjuzi Mwenye hikima.
53. Hayo ni ili alifanye lile analo litia Shet'ani liwe ni
fitna kwa wale wenye maradhi ndani ya nyoyo zao, na wale ambao nyoyo zao ni
ngumu. Na hakika madhaalimu wamo katika mfarakano wa mbali.
54. Na ili walio pewa ilimu wajue kuwa hayo ni Haki itokayo
kwa Mola wako Mlezi na waamini, na zipate kutua nyoyo zao. Na hakika Mwenyezi
Mungu ndiye anaye waongoa wenye kuamini kwenye Njia Iliyo Nyooka.
55. Na walio kufuru hawatoacha kuwa katika wasiwasi kwa
hilo mpaka Saa iwafikie ghafla, au iwafikie adhabu ya Siku Tasa.
56. Ufalme wote siku hiyo utakuwa wa Mwenyezi Mungu.
Atahukumu baina yao. Basi walio amini na wakatenda mema watakuwa katika Bustani
zenye neema.
57. Na walio kufuru na kuzikanusha Ishara zetu, basi hao
watapata adhabu ya kufedhehesha.
58. Na walio hama kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, kisha
wakauwawa au wakafa, bila ya shaka Mwenyezi Mungu atawaruzuku riziki njema. Na
hakika Mwenyezi Mungu ni Mbora wa wanao ruzuku.
59. BIla ya shaka atawaingiza pahala watakapo paridhia. Na
hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi na Mpole.
60. Ndio namna hivi. Na anaye lipiza mfano wa alivyo
adhibiwa, kisha akadhulumiwa, basi hapana shaka Mwenyezi Mungu atamsaidia.
Hakika Mwenyezi Mungu ni Msamehevu Mwenye maghfira.
61. Hayo ni kwa kuwa Mwenyezi Mungu huingiza usiku katika
mchana, na huuingiza mchana katika usiku, na ya kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye
kusikia Mwenye kuona.
62. Hayo ni kwa kuwa Mwenyezi Mungu ndiye Wa Kweli, na
kwamba wale wanao waomba badala yake, ni baat'ili, na hakika Mwenyezi Mungu
ndiye Aliye Juu na ndiye Mkubwa.
63. Je! Huoni kwamba Mwenyezi Mungu huteremsha maji kutoka
mbinguni, na mara ardhi inakuwa chanikiwiti? Hakika Mwenyezi Mungu ni Mpole na
Mwenye kujua.
64. Ni vyake viliomo mbinguni na viliomo katika ardhi. Na
hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujitosha na Mwenye kusifiwa.
65. Je! Huoni kwamba Mwenyezi Mungu amevidhalilisha kwenu
viliomo katika ardhi, na marikebu zipitazo baharini kwa amri yake, na
amezishika mbingu zisianguke juu ya ardhi ila kwa idhini yake. Hakika Mwenyezi
Mungu ni Mwenye huruma kwa watu, Mwenye kurehemu.
66. Na Yeye ndiye aliye kuhuisheni kisha akakufisheni, na
kisha atakufufueni. Hakika mwanaadamu hana fadhila.
67. Kila umma tumewajaalia na ibada zao wanazo zishika.
Basi wasizozane nawe katika jambo hili. Na waite watu kwendea kwa Mola wako
Mlezi. Hakika wewe uko kwenye Uwongofu Ulio Nyooka.
68. Na wakikujadili basi sema: Mwenyezi Mungu anajua zaidi
mnayo yatenda.
69. Mwenyezi Mungu atahukumu baina yenu Siku ya Kiyama
katika hayo mnayo khitalifiana.
70. Je! Hujui kwamba Mwenyezi Mungu anayajua yaliomo
mbinguni na katika ardhi? Hakika hayo yamo Kitabuni. Hakika hayo kwa Mwenyezi Mungu
ni mepesi.
71. Na wanaabudu badala ya Mwenyezi Mungu ambavyo
hakuviteremshia ushahidi, na ambavyo hawana ujuzi navyo. Na madhaalimu
hawatakuwa na wa kuwasaidia.
72. Na wanapo somewa Aya zetu zilizo wazi utaona chuki
katika nyuso za walio kufuru. Hukaribia kuwavamia wale wanao wasomea hizo Aya
zetu. Sema: Je! Nikwambieni yaliyo mabaya zaidi kuliko haya? Ni Moto. Mwenyezi
Mungu amewaahidi walio kufuru, na ni marudio mabaya hayo.
73. Enyi
watu! Unapigwa mfano, basi usikilizeni. Hakika wale mnao waomba badala
ya Mwenyezi Mungu, hawatoumba hata nzi ijapo kuwa watajumuika kwa hilo. Na nzi
akiwapokonya kitu hawawezi kukipata kwake. Amedhoofika kweli huyo mwenye kutaka
na mwenye kutakiwa.
74. Hawakumuadhimisha Mwenyezi Mungu anavyo stahiki
kuadhimishwa. Hakika Mwenyezi Mungu bila ya shaka ni Mwenye kushinda.
75. Mwenyezi Mungu huteuwa Wajumbe miongoni mwa Malaika na
miongoni mwa watu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.
76. Anayajua yaliyo mbele yao na yaliyo nyuma yao. Na kwa
Mwenyezi Mungu yatarejeshwa mambo yote.
77. Enyi mlio amini! Rukuuni na msujudu, na muabuduni Mola
wenu Mlezi, na tendeni mema, ili mfanikiwe.
78. Na fanyeni juhudi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu kama
inavyo stahiki jihadi yake. Yeye amekuteueni. Wala hakuweka juu yenu mambo
mazito katika Dini. Nayo ni mila ya baba yenu Ibrahim. Yeye (Mwenyezi Mungu)
alikuiteni Waislamu tangu zamani, na katika hii (Qur'ani) pia, ili awe Mtume
shahidi juu yenu, na nyinyi muwe mashahidi kwa watu. Basi shikeni Sala na toeni
Zaka na shikamaneni na Mwenyezi Mungu. Yeye ndiye Mlinzi wenu, Mlinzi bora
kabisa, na Msaidizi bora kabisa.
|