Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 23. SURATUL MUUMINUN
    • 1 - 50
Previous - Next

Click here to hide the links to concordance

1 - 50

1. HAKIKA wamefanikiwa Waumini,

2. Ambao ni wanyenyekevu katika Sala zao,

3. Na ambao hujiepusha na mambo ya upuuzi,

4. Na ambao wanatoa Zaka,

5.Na ambao wanazilinda tupu zao,

6. Isipo kuwa kwa wake zao au kwa iliyo wamiliki mikono yao ya kulia. Kwani hao si wenye kulaumiwa.

7. Lakini anaye taka kinyume cha haya, basi hao ndio warukao mipaka.

8. Na ambao wanazitimiza amana zao na ahadi zao,

9. Na ambao Sala zao wanazihifadhi -

10. Hao ndio warithi,

11. Ambao watairithi Pepo ya Firdausi, wadumu humo.

12. Na kwa yakini tumemuumba mtu kutokana na asli ya udongo.

13. Kisha tukamjaalia awe tone ya mbegu ya uzazi katika kalio madhubuti.

14. Kisha tukaiumba tone kuwa damu iliyo ganda, na tukaiumba damu kuwa pande la nyama, kisha tukaliumba pande la nyama kuwa mifupa, na mifupa tukaivika nyama. Kisha tukamfanya kiumbe mwengine. Basi ametukuka Mwenyezi Mungu Mbora wa waumbaji.

15. Kisha hakika nyinyi baada ya hayo mtakufa.

16. Kisha hakika nyinyi Siku ya Kiyama mtafufuliwa.

17. Na kwa yakini tumeziumba juu yenu njia saba. Nasi hatukuwa wenye kughafilika na viumbe.

18. Na tumeteremsha kutoka mbinguni maji kwa kiasi na tukayatuliza katika ardhi. Na hakika Sisi tunaweza kuyaondoa.

19. Kwa maji hayo tukakufanyieni bustani za mitende na mizabibu, mnapata humo matunda mengi, na katika hayo mnakula;

20. Na mti utokao katika mlima wa Sinai, unatoa mafuta na kuwa kitoweo kwa walao.

21. Na hakika mnayo mazingatio makubwa katika nyama hoa - tunakunywesheni katika vile viliomo matumboni mwao, na nyinyi mnapata katika hao manufaa mengi, na pia mnawala.

22. Na juu yao na juu ya marikebu mnabebwa.

23. Na hakika tulimtuma Nuhu kwa watu wake, akasema: Enyi watu wangu! Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna mungu asiye kuwa Yeye. Basi je! Hamwogopi?

24. Walisema wale wakuu walio kufuru katika watu wake: Huyu si chochote ila ni mtu tu kama nyinyi. Anataka kujipa ubora juu yenu. Na lau kuwa Mwenyezi Mungu amependa basi yakini angeli teremsha Malaika. Hatukusikia haya kwa baba zetu wa zamani.

25. Huyu si lolote ila ni mtu mwenye wazimu. Basi mngojeeni tu kwa muda.

26. Akasema (Nuhu): Mola wangu Mlezi! Ninusuru kwa kuwa wamenikanusha.

27. Tukampa wahyi: Unda jahazi mbele ya macho yetu na uwongozi wetu! Basi itapo fika amri yetu na ikafurika tanuri, hapo waingize ndani yake wa kila namna dume na jike, na ahali zako, isipo kuwa yule ambaye katika wao juu yake imekwisha tangulia kauli. Wala usinitajie hao walio dhulumu. Kwani hao bila ya shaka watazamishwa.

28. Basi utakapo tulia wewe na walio pamoja nawe humo marikebuni, sema: Alhamdulillahi Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu, aliye tuokoa na watu madhaalimu!

29. Na sema: Mola wangu Mlezi! Niteremshe mteremsho wenye baraka, na Wewe ni Mbora wa wateremshaji.

30. Hakika katika hayo yapo mazingatio. Na kwa yakini Sisi ni wenye kuwafanyia mtihani.

31. Kisha baada yao tukaanzisha kizazi kingine.

32. Tukawapelekea Mtume miongoni mwao, kuwaambia: Muabuduni Mwenyezi Mungu! Hamna mungu asiye kuwa Yeye. Jee, hamwogopi?

33. Na wakubwa katika watu wake walio kufuru na wakakanusha mkutano wa Akhera, na tukawadekeza kwa starehe katika maisha ya dunia, walisema: Huyu si chochote ila ni binaadamu kama nyinyi; anakula mlacho, na anakunywa mnywacho.

34. Na nyinyi mkimt'ii mtu kama nyinyi basi hakika mtakuwa khasarani.

35. Hivyo anakuahidini ati ya kwamba mtakapo kufa na mkawa udongo na mifupa kuwa mtatolewa?

36. Hayawi! Hayawi hayo mnayo ahidiwa.

37. Hapana ila uhai wetu wa duniani tu, tunakufa na kuishi basi. Wala sisi hatutafufuliwa.

38. Huyu si lolote ila ni mtu anaye mzulia Mwenyezi Mungu uwongo, wala sisi sio wa kumuamini.

39. Akasema: Mola wangu Mlezi! Ninusuru kwa sababu wananikanusha.

40. (Mwenyezi Mungu) akasema: Baada ya muda mchache watakuwa wenye kujuta.

41. Basi ukawanyakua ukelele kwa haki, na tukawafanya kama takataka zinazo elea juu ya maji. Ikapotelea mbali kaumu ya madhaalimu!

42. Kisha tukaleta baada yao vizazi vingine.

43. Hapana umma uwezao kutanguliza ajali yake wala kuikawiza.

44. Kisha tukawatuma Mitume wetu, mmoja baada ya mmoja. Kila umma alipo wafikia Mtume wao walimkanusha. Tukawafuatanisha hawa baada ya hawa, na tukawafanya ni hadithi za kusimuliwa. Wakapotelea mbali watu wasio amini.

45. Kisha tukamtuma Musa na nduguye, Haaruni, pamoja na ishara zetu na hoja zilizo wazi.

46. Kumwendea Firauni na wakuu wake. Lakini walijivuna, nao walikuwa watu majeuri.

47. Wakasema: Je, tuwaamini wanaadamu wawili hawa kama sisi, na ambao watu wao ni watumwa wetu?

48. Basi wakawakanusha, na wakawa miongoni mwa walio angamizwa.

49. Na hakika tulimpa Musa Kitabu ili wapate kuongoka.

50. Na tukamfanya mwana wa Mariamu na mama yake kuwa ni Ishara, na tukawapa makimbilio kwenda mahali palipo inuka penye utulivu na chemchem za maji.




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License