Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 26. SURAT ASH-SHUA'RAA
    • 151 - 200
Previous - Next

Click here to hide the links to concordance

151 - 200

151 Wala msit'ii amri za walio pindukia mipaka,

152. Ambao wanafanya ufisadi katika nchi, wala hawatengenezi.

153. Wakasema: Hakika wewe ni miongoni mwa walio rogwa.

154. Wewe si chochote ila ni mtu kama sisi. Basi lete Ishara ukiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.

155. Akasema: Huyu ngamia jike; awe na zamu yake ya kunywa, na nyinyi muwe na zamu yenu ya kunywa katika siku maalumu.

156. Wala msimguse kwa uwovu, isije ikakushikeni adhabu ya Siku Kubwa.

157. Lakini wakamuuwa, na wakawa wenye kujuta.

158. Basi ikawapata adhabu. Hakika katika hayo ipo Ishara. Lakini hawakuwa wengi wao wenye kuamini.

159. Na hakika Mola wako Mlezi ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.

160. Watu wa Lut'i waliwakanusha Mitume.

161. Alipo waambia ndugu yao, Lut'i: Je! Hamumchimngu?

162. Hakika mimi kwenu ni Mtume muaminifu kwenu.

163. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na nit'iini mimi.

164. Wala mimi sikutakini ujira juu yake; ujira wangu hauko ila kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

165. Je! Katika viumbe vyote mnawaingilia wanaume?

166. Na mnaacha alicho kuumbieni Mola wenu Mlezi katika wake zenu? Ama kweli nyinyi ni watu mnao ruka mipaka!

167. Wakasema: Ewe Lut'i! Usipo acha, hapana shaka utakuwa miongoni mwa wanao tolewa mji!

168. Akasema: Hakika mimi ni katika wanao kichukia hichi kitendo chenu.

169. Mola wangu Mlezi! Niokoe mimi na ahali zangu na haya wayatendayo.

170. Basi tukamwokoa yeye na ahali zake wote,

171. Isipo kuwa kikongwe katika walio kaa nyuma.

172. Kisha tukawaangamiza wale wengine.

173. Na tukawanyeshea mvua, basi ni ovu mno mvua ya waliyo onywa.

174. Hakika katika hayo ipo Ishara. Na hawakuwa wengi wao wenye kuamini.

175. Na hakika Mola wako Mlezi bila ya shaka ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

176. Watu wa Machakani waliwakanusha Mitume.

177. Shuaibu alipo waambia: Je! Hamfanyi mkamchamngu?

178. Hakika mimi kwenu ni Mtume muaminifu.

179. Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini mimi.

180. Wala sikutakini ujira juu yake. Ujira wangu hauko ila kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

181. Timizeni kipimo sawa sawa, wala msiwe katika wanao punja.

182. Na pimeni kwa haki iliyo nyooka;

183. Wala msiwapunje watu vitu vyao, wala msifanye jeuri kwa ufisadi.

184. Na mcheni aliye kuumbeni nyinyi na vizazi vilivyo tangulia.

185. Wakasema: Hakika wewe ni katika walio rogwa.

186. Na wewe si chochote ila ni mtu tu kama sisi, na kwa yakini tunakuona wewe ni katika waongo.

187. Hebu tuangushie vipande kutoka mbinguni ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.

188. Akasema: Mola wangu Mlezi anajua zaidi mnayo yatenda.

189. Basi walimkanusha, na ikawashika adhabu ya siku ya kivuli. Hakika hiyo ilikuwa adhabu ya siku kubwa.

190. Hakika katika hayo ipo Ishara, lakini hawakuwa wengi wao wenye kuamini.

191. Na hakika Mola wako Mlezi bila ya shaka ndiye Yeye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.

192. Na bila ya shaka hii ni Uteremsho wa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

193. Ameuteremsha Roho muaminifu,

194. Juu ya moyo wako, ili uwe katika Waonyaji,

195. Kwa ulimi wa Kiarabu ulio wazi.

196. Na hakika bila ya shaka haya yamo katika Vitabu vya kale.

197. Je! Haikuwa kwao ni Ishara kwamba wanayajua haya wanazuoni wa Wana wa Israili?

198. Na lau kuwa tungeli iteremsha juu ya mmoja wa wasio kuwa Waarabu,

199. Na akawasomea, wasingeli kuwa wenye kuamini.

200. Namna hivi tunaingiza katika nyoyo za wakosefu.




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License