27. SURAT AN-NAML
(Imeteremka
Makka)
SURA AN-NAML ni ya Makka. Aya
zake ni 93.
Imeanza kwa harufi za kutamkwa, kukumbusha cheo cha Qur'ani ambayo imetoka
katika jinsi ya maneno ya Kiarabu. Na juu ya hivyo imewashinda hao Waarabu
kuleta mfano wake. Na tena pia ni kama kumzindua aliye ghafilika aisikilize.
Baada yake kimekuja kisa cha Musa a.s. Na imetajwa baadhi ya miujiza yake, na
kisa cha Daudi a.s. na kurithiwa kwake na mwanawe, Mfalme Sulaiman, na
kukusanyika majini, na watu, na ndege kwa ajili yake. Na imetajwa kufahamu
kwake Sulaiman maneno ya wanyama, na shukrani yake kwa neema hii. Kisha kutoweka
ndege Hud-hud, na akaja na kisa cha Balqis, na kuabudu kwake bibi huyu na watu
wake kuliabudu jua. Tena Sulaiman akampelekea barua, naye akamjibu kwa
kumpelekea zawadi baada ya kushauriana na watu wake, na ikaelezwa kuletwa kiti
chake cha enzi kwa njia ya mwenye ilimu ya Kitabu, na kuingia kwake huyo bibi
katika qasri (jumba la kifalme) la Sulaiman, nalo likamshitua, na akatangaza
ut'iifu wake na Imani yake kumuamini Sulaiman.
Na Sura hii imetaja hadithi ya Saleh a.s. na kaumu yake, na hadithi ya Lut'i a.s.
na kaumu yake, na kuvuka kwake, na kuangamia kwa mafisadi. Na Sura tukufu hii
imezindua ziangaliwe dalili za aliye umba mbingu na ardhi zenye kuthibitisha
uwezo wake na upweke wake.
Na ikaashiria cheo cha katika kazi ya Daa'wa (Wito), na vipi washirikina
wanavyo ipuuza juu ya kuwa muujiza wake umekamilika. Na imetaja yatakayo kuwa
atapo toka mnyama akisema na watu kuwa walikuwa hawana yakini ya Ishara zetu.
Kisha Sura ikaelekea ulimwengu, na vipi watavyo fazaika waliomo wakati wa
mpulizo wa kufufuliwa na kukusanywa. Na ikanabihisha hali ya ardhi, na kwamba
milima yake inakwenda kama yaendavyo mawingu, na ikasimulia yanayo mfuatia
Mtume katika kazi yake ya Daa'wa, na kwamba ni waajibu Mwenyezi Mungu Aliye
takasika asifiwe.
KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU
MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
|