37. SURAT ASS'AFFAT
(Imeteremka
Makka)
Sura hii imeanza kwa kiapo
kwa mataifa miongoni mwa viumbe vya Mwenyezi Mungu ambayo yana sifa ya
kujipanga kwa safu, na kuzuia, na kusoma. Kiapo hicho ni kuwa hakika Mwenyezi
Mungu ni Mmoja. Na Ishara zinashuhudia kwa hayo. Kwani Yeye ni Mola Mlezi wa
mbingu na ardhi na vilio baina yao, na Yeye ni Mola Mlezi wa mashariki na
magharibi, ambaye aliye ipamba mbingu ya dunia kwa nyota, na akaifanya
ihifadhike na muasi aliye acha ut'iifu wa Mwenyezi Mungu. Na baada ya
kuthibitisha itikadi ya Tawhidi, Sura imeendelea kuthibitisha itikadi ya
kufufuliwa. Na ikawahadharisha wenye kutia shaka kuwa huko kufufuliwa
kutawazukia ghafla nao wanaona. Na ikazileta dalili za kumkinika huko, bali
wepesi wa kutokea kwake, na hali wao wanayaona hayo na wanasema: Hii ndiyo Siku
ya Hisabu! Na wataambiwa: Hii ndiyo Siku ya mpambanuo mlio kuwa mkiikanusha. Na
watakusanywa madhaalimu na walivyo kuwa wakiviabudu. Na watasailiwa na
watahojiwa. Na watakuwa wakisingiziana wao kwa wao madhambi walio yapata, na
hali wote watakuwa wanashirikiana pamoja katika adhabu. Kwani walijivuna
wakakataa kumuamini Mwenyezi Mungu Mmoja, na wakamsingizia Mtume wao kuwa ana
kichaa na wazimu; na hali kuwa hapana shaka kuwa kawajia na Haki. Na Mitume
wamesema kweli katika waliyo kuja nayo kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Na Waumini
wenye ikhlasi watastareheshwa kwa kila namna ya neema. Na watazikumbuka neema
za Mwenyezi Mungu. Watawatokea watu waovu, na watawaona katikati ya Moto wa
Jahim. Watamhimidi Mwenyezi Mungu kwa alivyo walinda, na walivyo okoka
wasifuate wito wa wale waovu. Baada ya hayo Sura ikaingia ikieleza mashukio ya
walio dhulumu na mashukio ya Waumini. Tena ikafuatiliza kwa kueleza khabari za
Mitume wengine ili kumpoza Mtume wa Mwenyezi Mungu, na kuwapa mawaidha watu
wake wanao pinga. Na baada ya hadithi mbali mbali za zama mbali mbali na watu
mbali mbali, zilizo eleza cheo cha Ujumbe na Wajumbe wenyewe, Sura imetengua
madai ya washirikina kwamba Mwenyezi Mungu ana mabinti na wao wana watoto
wanaume. Na kwamba Yeye amewafanya Malaika ni wanawake. Na kwamba ipo nasaba ya
kukhusiana baina yake na majini. Mwenyezi Mungu Ametakasika na hayo wanayo
yazua. Na waja wake ndio watanusuriwa, na jeshi lake ndilo litakalo shinda. Na
adhabu yake itaifanya ovu asubuhi ya wanao onywa. Na Sura ikakhitimisha kwa
kumtakasa Mola Mlezi wa Utukufu na hayo wanayo mzulia. Na amani ishuke kwa
Mitume wote, na Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu
wote.
KWA JINA LA MWENYEZI
MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
|