Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 37. SURAT ASS'AFFAT
    • 51 - 100
Previous - Next

Click here to hide the links to concordance

51 - 100

51. Aseme msemaji mmoja miongoni mwao: Hakika mimi nalikuwa na rafiki

52. Aliye kuwa akinambia: Hivyo wewe ni katika wanao sadiki

53. Ati tukisha kufa tukawa udongo na mafupa, ndio tutalipwa na kuhisabiwa?

54. Atasema: Je! Nyie mnawaona?

55. Basi atachungulia amwone katikati ya Jahannamu.

56. Atasema: Wallahi! Ulikaribia kunipoteza.

57. Na lau kuwa si neema ya Mola wangu Mlezi bila ya shaka ningeli kuwa miongoni mwa walio hudhurishwa.

58. Je! Sisi hatutakufa,

59. Isipo kuwa kifo chetu cha kwanza? Wala sisi hatutaadhibiwa.

60. Hakika huku bila ya shaka ndiko kufuzu kukubwa.

61. Kwa mfano wa haya nawatende watendao.

62. Je! Kukaribishwa hivi si ndio bora, au mti wa Zaqqum?

63. Hakika Sisi tumeufanya huo kuwa ni mateso kwa walio dhulumu.

64. Hakika huo ni mti unao toka katikati ya Jahannamu.

65. Mashada ya matunda yake kama kwamba vichwa vya mashet'ani.

66. Basi hakika bila ya shaka hao watayala hayo, na wajaze matumbo.

67. Kisha juu yake wanyweshwe mchanganyo wa maji yamoto yaliyo chemka.

68. Kisha hakika marejeo yao bila ya shaka yatakuwa kwenye Jahannamu.

69. Hakika waliwakuta baba zao wamepotea.

70. Na wao wakafanya haraka kufuata nyayo zao.

71. Na bila ya shaka walikwisha potea kabla yao wengi wa watu wa zamani.

72. Na Sisi hakika tuliwapelekea waonyaji.

73. Basi hebu angalia ulikuwaje mwisho wa walio onywa.

74. Isipo kuwa waja wa Mwenyezi Mungu walio khitariwa.

75. Na hakika Nuhu alitwita, na Sisi ni bora wa waitikiaji.

76. Na tulimwokoa yeye na ahali zake kutokana na msiba mkubwa.

77. Na tuliwajaalia dhuriya zake ndio wenye kubakia.

78. Na tukamwachia (sifa njema) kwa walio kuja baadaye.

79. Iwe salama kwa Nuhu ulimwenguni kote!

80. Kwa hakika hivi ndivyo tunavyo walipa wanao fanya mema.

81. Hakika yeye ni katika waja wetu walio amini.

82. Kisha tukawazamisha wale wengine.

83. Na hakika Ibrahim alikuwa katika kundi lake,

84. Alipo mjia Mola wake Mlezi kwa moyo mzima.

85. Alimwambia baba yake na watu wake: Mnaabudu nini?

86. Kwa kuzua tu mnataka miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu?

87. Mnamdhania nini Mola Mlezi wa walimwengu wote?

88. Kisha akapiga jicho kutazama nyota.

89. Akasema: Hakika mimi ni mgonjwa!

90. Nao wakamwacha, wakampa kisogo.

91. Basi akaiendea miungu yao kwa siri, akaiambia: Mbona hamli?

92. Mna nini hata hamsemi?

93. Kisha akaigeukia kuipiga kwa mkono wa kulia.

94. Basi wakamjia upesi upesi.

95. Akasema: Hivyo mnaviabudu vitu mnavyo vichonga wenyewe?

96. Na hali Mwenyezi Mungu ndiye aliye kuumbeni nyinyi na hivyo mnavyo vifanya!

97. Wakasema: Mjengeeni jengo, na kisha mtupeni motoni humo!

98. Basi walitaka kumfanyia vitimbi, lakini tukawafanya wao ndio wa chini.

99. Na akasema: Hakika mimi nahama, nakwenda kwa Mola wangu Mlezi; Yeye ataniongoa.

100. Ewe Mola wangu Mlezi! Nitunukie aliye miongoni mwa watenda mema.




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License