Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 38. SURAT S'AAD
    • 1 - 50
Previous - Next

Click here to hide the links to concordance

1 - 50

1. S'ad, Naapa kwa Qur'ani yenye mawaidha.

2. Lakini walio kufuru wamo katika majivuno na upinzani

3. Mataifa mangapi tumeyaangamiza kabla yao, na wakapiga kelele, lakini wakati wa kuokoka ulikwisha pita.

4. Na walistaajabu kuwajia mwonyaji anaye tokana nao wenyewe, na makafiri wakasema: Huyu ni mchawi, mwongo.

5. Amewafanya miungu wote kuwa ni Mungu Mmoja tu? Hakika hili ni jambo la ajabu.

6. Na wakaondoka wakubwa wao wakiwaambia: Nendeni zenu na dumuni na miungu yenu, kwani hili ni jambo lililo pangwa.

7. Sisi hatukusikia haya katika mila hii ya mwisho. Haya si chochote ila ni uzushi tu.

8. Ati yeye tu ndiye aliye teremshiwa mawaidha peke yake katika sisi? Lakini hao wana shaka na mawaidha yangu, bali hawajaionja adhabu yangu.

9. Au wanazo wao khazina za rehema za Mola wako Mlezi, Mwenye nguvu, Mpaji?

10. Au wao wana ufalme wa mbingu na ardhi na viliomo kati yao? Basi nawazipande njia za kwendea huko!

11. Hao ni askari watao shindwa miongoni mwa makundi yatayo shindwa.

12. Walikanusha kabla yao kaumu ya Nuhu, na kina A'adi na Firauni mwenye majengo.

13. Na Thamud na kaumu Lut'i na watu wa Machakani. Hayo ndiyo makundi.

14. Hao wote waliwakadhibisha Mitume; basi wakastahiki adhabu yangu.

15. Na hawa hawangojei ila ukelele mmoja tu usio na muda.

16. Na wao husema: Mola wetu Mlezi! Tuletee upesi sehemu yetu ya adhabu kabla ya Siku ya Hisabu.

17. Subiri kwa hayo wayasemayo, na umkumbuke mja wetu Daudi, mwenye nguvu. Hakika yeye alikuwa mwingi wa kutubia.

18. Hakika tuliidhalilisha milima pamoja naye ikisabihi jioni na asubuhi pamoja naye.

19. Na pia ndege walio kusanywa makundi kwa makundi; wote walikuwa wanyenyekevu kwake.

20. Na tukautia nguvu ufalme wake, na tukampa hikima, na kukata hukumu.

21. Na je! Imekufikia khabari ya wagombanao walipo pindukia ukuta kuingia chumbani?

22. Walipo muingilia Daudi, naye akawaogopa. Wakasema: Usiogope! Sisi ni wagombanao wawili, mmoja wetu amemdhulumu mwenziwe. Basi tuhukumu kwa haki, wala usipendelee. Na utuongoe kwenye njia iliyo sawa.

23. Hakika huyu ndugu yangu ana kondoo wa kike tisiini na tisa; na mimi ninaye kondoo mke mmoja. Akasema: Nipe huyo nikufugie! Na amenishinda kwa maneno.

24. Akasema: Kweli amekudhulumu kwa kumtaka kondoo wako mmoja kuongezea kwenye kondoo wake. Na hakika washirika wengi hudhulumiana wao kwa wao, isipo kuwa walio amini na wakatenda mema. Na hao ni wachache. Na Daudi akajua kuwa tumemfanyia mtihani. Basi akamwomba msamaha Mola wake Mlezi, na akaanguka kusujudu na kutubia.

25. Basi tukamsamehe kwa hayo. Naye kwa hakika anao mkaribisho mkubwa na marejeo mazuri kwetu.

26. Ewe Daudi! Hakika Sisi tumekufanya wewe uwe Khalifa katika nchi. Basi wahukumu watu kwa haki, wala usifuate matamanio yakakupoteza kwenye Njia ya Mwenyezi Mungu. Hakika wanao ipotea Njia ya Mwenyezi Mungu wakaiacha, watapata adhabu kali kwa sababu ya kusahau kwao Siku ya Hisabu.

27. Na hatukuziumba mbingu na ardhi na viliomo ndani yao bure. Hiyo ni dhana ya walio kufuru. Ole wao walio kufuru kwa Moto utao wapata.

28. Je! Tuwafanye walio amini na wakatenda mema kama wafanyao uharibifu katika nchi? Au tuwafanye wachamngu kama waovu?

29. Na hiki Kitabu, tumekuteremshia wewe, kimebarikiwa, ili wazizingatie Aya zake, na wawaidhike wenye akili.

30. Na Daudi tukamtunukia Suleiman. Alikuwa mja mwema. Na hakika alikuwa mwingi wa kutubia.

31. Alipo pelekewa jioni farasi wasimamao kidete, tayari kutoka shoti;

32. Basi akasema: Navipenda vitu vizuri kwa kumkumbuka Mola wangu Mlezi. Kisha wakafichikana nyuma ya boma.

33. (Akasema:) Nirudishieni! Akaanza kuwapapasa miguu na shingo.

34. Na tulimtia mtihanini Suleiman, na tukauweka mwili juu ya kiti chake, kisha akarejea kwa kutubu.

35. Akasema: Mola wangu Mlezi! Nisamehe na unipe ufalme usio mwelekea yeyote baada yangu. Hakika Wewe ndiye Mpaji.

36. Basi tukaufanya upepo umtumikie, ukenda kwa amri yake, popote alipo taka kufika.

37. Na tukayafanya mashet'ani yamtumikie, wote wajenzi na wapiga mbizi.

38. Na wengine wafungwao kwa minyororo.

39. Hichi ndicho kipawa chetu. Basi toa au zuia, bila ya hisabu.

40. Na hakika yeye kwetu Sisi ana cheo cha kukaribishwa kwetu, na pahala pazuri pa kurejea.

41. Na mkumbuke mja wetu Ayubu alipo mwita Mola wake Mlezi akasema: Kwa hakika Shet'ani amenifikishia udhia na adhabu.

42. (Akaambiwa:) Piga-piga ardhi kwa mguu wako! Basi haya maji baridi ya kuogea na ya kunywa.

43. Na tukampa ahali zake na wengine kama wao pamoja nao, kuwa ni rehema itokayo kwetu, na iwe kumbusho kwa watu wenye akili.

44. Na shika kicha cha vijiti tu mkononi mwako, kisha ndio upigie nacho, wala usivunje kiapo. Hakika tulimkuta mwenye subira, mbora wa waja, kwa hakika alikuwa mwingi wa kutubu.

45. Na wakumbuke waja wetu, Ibrahim na Is-haqa na Yaa'qubu walio kuwa na nguvu na busara.

46. Sisi tumewakhusisha wao kwa sifa ya ukumbusho wa Akhera.

47. Na hakika wao kwetu sisi ni wateuliwa walio bora.

48. Na mkumbuke Ismail na Alyasaa na Dhulkifli, na wote hao ni katika walio bora.

49. Huu ni ukumbusho. Na hakika wachamngu wana marudio mazuri.

50. Bustani za milele zitazo funguliwa milango yao kwa ajili yao.




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License