1 - 50
1. S'ad, Naapa kwa Qur'ani yenye mawaidha.
2. Lakini walio kufuru wamo katika majivuno na upinzani
3. Mataifa mangapi tumeyaangamiza kabla yao, na wakapiga
kelele, lakini wakati wa kuokoka ulikwisha pita.
4. Na walistaajabu kuwajia mwonyaji anaye tokana nao
wenyewe, na makafiri wakasema: Huyu ni mchawi, mwongo.
5. Amewafanya miungu wote kuwa ni Mungu Mmoja tu? Hakika
hili ni jambo la ajabu.
6. Na wakaondoka wakubwa wao wakiwaambia: Nendeni zenu na
dumuni na miungu yenu, kwani hili ni jambo lililo pangwa.
7. Sisi hatukusikia haya katika mila hii ya mwisho. Haya si
chochote ila ni uzushi tu.
8. Ati yeye tu ndiye aliye teremshiwa mawaidha peke yake
katika sisi? Lakini hao wana shaka na mawaidha yangu, bali hawajaionja adhabu
yangu.
9. Au wanazo wao khazina za rehema za Mola wako Mlezi,
Mwenye nguvu, Mpaji?
10. Au wao wana ufalme wa mbingu na ardhi na viliomo kati
yao? Basi nawazipande njia za kwendea huko!
11. Hao ni askari watao shindwa miongoni mwa makundi yatayo
shindwa.
12. Walikanusha kabla yao kaumu ya Nuhu, na kina A'adi na
Firauni mwenye majengo.
13. Na Thamud na kaumu Lut'i na watu wa Machakani. Hayo ndiyo makundi.
14. Hao
wote waliwakadhibisha Mitume; basi wakastahiki adhabu yangu.
15. Na
hawa hawangojei ila ukelele mmoja tu usio na muda.
16. Na wao husema: Mola wetu Mlezi! Tuletee upesi sehemu
yetu ya adhabu kabla ya Siku ya Hisabu.
17. Subiri kwa hayo wayasemayo, na umkumbuke mja wetu
Daudi, mwenye nguvu. Hakika yeye alikuwa mwingi wa kutubia.
18. Hakika tuliidhalilisha milima pamoja naye ikisabihi
jioni na asubuhi pamoja naye.
19. Na pia ndege walio kusanywa makundi kwa makundi; wote
walikuwa wanyenyekevu kwake.
20. Na tukautia nguvu ufalme wake, na tukampa hikima, na
kukata hukumu.
21. Na je! Imekufikia khabari ya wagombanao walipo pindukia
ukuta kuingia chumbani?
22. Walipo muingilia Daudi, naye akawaogopa. Wakasema:
Usiogope! Sisi ni wagombanao wawili, mmoja wetu amemdhulumu mwenziwe. Basi tuhukumu
kwa haki, wala usipendelee. Na utuongoe kwenye njia iliyo sawa.
23. Hakika huyu ndugu yangu ana kondoo wa kike tisiini na
tisa; na mimi ninaye kondoo mke mmoja. Akasema: Nipe huyo nikufugie! Na
amenishinda kwa maneno.
24. Akasema: Kweli amekudhulumu kwa kumtaka kondoo wako
mmoja kuongezea kwenye kondoo wake. Na hakika washirika wengi hudhulumiana wao
kwa wao, isipo kuwa walio amini na wakatenda mema. Na hao ni wachache. Na Daudi akajua kuwa
tumemfanyia mtihani. Basi akamwomba msamaha Mola wake Mlezi, na akaanguka
kusujudu na kutubia.
25. Basi
tukamsamehe kwa hayo. Naye kwa hakika anao mkaribisho mkubwa na marejeo mazuri
kwetu.
26. Ewe
Daudi! Hakika Sisi tumekufanya wewe uwe Khalifa katika nchi. Basi wahukumu watu
kwa haki, wala usifuate matamanio yakakupoteza kwenye Njia ya Mwenyezi Mungu.
Hakika wanao ipotea Njia ya Mwenyezi Mungu wakaiacha, watapata adhabu kali kwa
sababu ya kusahau kwao Siku ya Hisabu.
27. Na
hatukuziumba mbingu na ardhi na viliomo ndani yao bure. Hiyo ni dhana ya walio
kufuru. Ole wao walio kufuru kwa Moto utao wapata.
28. Je!
Tuwafanye walio amini na wakatenda mema kama wafanyao uharibifu katika nchi? Au
tuwafanye wachamngu kama waovu?
29. Na
hiki Kitabu, tumekuteremshia wewe, kimebarikiwa, ili wazizingatie Aya zake, na
wawaidhike wenye akili.
30. Na Daudi tukamtunukia Suleiman. Alikuwa mja mwema. Na
hakika alikuwa mwingi wa kutubia.
31. Alipo pelekewa jioni farasi wasimamao kidete, tayari
kutoka shoti;
32. Basi akasema: Navipenda vitu vizuri kwa kumkumbuka Mola
wangu Mlezi. Kisha wakafichikana nyuma ya boma.
33. (Akasema:) Nirudishieni! Akaanza kuwapapasa miguu na
shingo.
34. Na tulimtia mtihanini Suleiman, na tukauweka mwili juu
ya kiti chake, kisha akarejea kwa kutubu.
35. Akasema: Mola wangu Mlezi! Nisamehe na unipe ufalme
usio mwelekea yeyote baada yangu. Hakika Wewe ndiye Mpaji.
36. Basi
tukaufanya upepo umtumikie, ukenda kwa amri yake, popote alipo taka kufika.
37. Na
tukayafanya mashet'ani yamtumikie, wote wajenzi na wapiga mbizi.
38. Na
wengine wafungwao kwa minyororo.
39. Hichi ndicho kipawa chetu. Basi toa au zuia, bila ya
hisabu.
40. Na hakika yeye kwetu Sisi ana cheo cha kukaribishwa
kwetu, na pahala pazuri pa kurejea.
41. Na mkumbuke mja wetu Ayubu alipo mwita Mola wake Mlezi
akasema: Kwa hakika Shet'ani amenifikishia udhia na adhabu.
42. (Akaambiwa:) Piga-piga ardhi kwa mguu wako! Basi haya
maji baridi ya kuogea na ya kunywa.
43. Na tukampa ahali zake na wengine kama wao pamoja nao,
kuwa ni rehema itokayo kwetu, na iwe kumbusho kwa watu wenye akili.
44. Na shika kicha cha vijiti tu mkononi mwako, kisha ndio
upigie nacho, wala usivunje kiapo. Hakika tulimkuta mwenye subira, mbora wa
waja, kwa hakika alikuwa mwingi wa kutubu.
45. Na wakumbuke waja wetu, Ibrahim na Is-haqa na Yaa'qubu
walio kuwa na nguvu na busara.
46. Sisi tumewakhusisha wao kwa sifa ya ukumbusho wa
Akhera.
47. Na hakika wao kwetu sisi ni wateuliwa walio bora.
48. Na mkumbuke Ismail na Alyasaa na Dhulkifli, na wote hao
ni katika walio bora.
49. Huu ni ukumbusho. Na hakika wachamngu wana marudio
mazuri.
50. Bustani za milele zitazo funguliwa milango yao kwa
ajili yao.
|