1 - 50
1. H'a,
Mim.
2.
Uteremsho wa Kitabu umetoka kwa Mwenyezi Mungu Mwenye nguvu, Mwenye kujua.
3. Anaye
samehe dhambi na anaye pokea toba, Mkali wa kuadhibu, Mwenye ukarimu, hakuna
mungu ila Yeye; marejeo ni kwake.
4.
Hawazibishi Ishara za Mwenyezi Mungu ila walio kufuru; basi kusikughuri wewe
kutanga tanga kwao katika nchi.
5. Kabla
yao walikadhibisha kaumu ya Nuhu na makundi mengine baada yao. Na kila taifa
lilikuwa na hamu juu ya Mtume wao wamkamate. Na walibishana kwa upotovu ili
kuipindua haki. Kwa hivyo niliwakamata. Basi ilikuwaje adhabu yangu!
6. Namna
hivi limewathibitikia makafiri neno la Mola wako Mlezi ya kwamba wao ni watu wa
Motoni.
7. Wale
wanao beba A'rshi, na wanao izunguka, wanamsabihi na kumhimidi Mola wao Mlezi,
na wanamuamini, na wanawaombea msamaha walio amini kwa kusema: Mola wetu Mlezi!
Umekienea kila kitu kwa rehema na ujuzi. Basi wasamehe walio tubu na wakaifuata
Njia yako, na waepushe na adhabu ya Jahannamu.
8. Mola wetu Mlezi! Na waingize katika Bustani za Milele
ulizo waahidi. Na uwape haya pia wale walio fanya mema miongoni mwa wazee wao
na wake zao na dhuriya zao. Hakika Wewe ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.
9. Na waepushe na maovu; kwani umwepushaye maovu siku hiyo,
hakika umemrehemu; na huko ndiko kufuzu kukubwa.
10. Kwa hakika wale walio kufuru watanadiwa: Bila ya shaka
kukuchukieni Mwenyezi Mungu ni kukubwa kuliko kujichukia nyinyi nafsi zenu,
mlipo kuwa mnaitwa kwenye Imani nanyi mkakataa.
11. Watasema: Mola wetu Mlezi! Umetufisha mara mbili, na
umetuhuisha mara mbili! Basi tunakiri madhambi yetu. Basi je, ipo njia ya kutoka?
12. Hayo ni
hivyo kwa sababu mlikuwa akiombwa Mwenyezi Mungu peke yake mnakataa. Na
akishirikishwa mnaamini. Basi hukumu ni ya Mwenyezi Mungu Mtukufu Mkuu.
13. Yeye ndiye
anaye kuonyesheni Ishara zake, na anakuteremshieni kutoka mbinguni riziki. Na
hapana anaye kumbuka ila anaye rejea.
14. Basi
mwombeni Mwenyezi Mungu mkimsafia Dini Yeye tu, na wangachukia makafiri.
15. Yeye ndiye
Mwenye vyeo vya juu, Mwenye A'rshi. Hupeleka Roho kwa amri yake juu ya amtakaye
katika waja wake, ili kuonya kwa Siku ya Mkutano.
16. Siku
watakayo dhihiri wao. Hapana kitacho fichikana chochote chao kwa Mwenyezi
Mungu. Ufalme ni wa nani leo? Ni wa Mwenyezi Mungu Mmoja Mtenda nguvu.
17. Leo kila nafsi italipwa kwa iliyo chuma. Hapana dhulma
leo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhisabu.
18. Na waonye siku inayo kurubia, wakati nyoyo zitakapo
fika kooni, nao wamejaa huzuni. Madhaalimu hawatakuwa na rafiki, wala mwombezi
wa kuitikiwa.
19. (Mwenyezi Mungu) anajua khiyana ya macho na yanayo
ficha vifua.
20. Na Mwenyezi Mungu huhukumu kwa haki; lakini hao wanao
waomba badala yake hawahukumu chochote. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye
kusikia Mwenye kuona.
21. Kwani hawatembei katika ardhi wakaona jinsi ulivyo kuwa
mwisho wa walio kuwa kabla yao? Hao walikuwa wamewazidi hawa kwa nguvu na
athari katika nchi. Na Mwenyezi Mungu aliwatia mkononi kwa sababu ya madhambi
yao. Na wala hapakuwa wa kuwalinda na Mwenyezi Mungu.
22. Hayo ni kwa sababu walikuwa wanawajia Mitume wao kwa
hoja zilizo wazi, lakini wakawakataa, ndipo Mwenyezi Mungu akawakamata. Bila ya
shaka Yeye ni Mwenye nguvu, Mkali wa kuadhibu.
23. Na kwa yakini tulimtuma Musa pamoja na Ishara zetu na
uthibitisho ulio wazi,
24. Kumwendea Firauni na Hamana na Qaruni, wakasema: Huyu
ni mchawi, mwongo mkubwa.
25. Basi alipo waletea Haki inayo toka kwetu, walisema:
Waueni watoto wanaume wa wale walio muamini na wawacheni hai wanawake wao. Na
haviwi vitimbi vya makafiri ila katika upotovu.
26. Na Firauni akasema: Niachieni nimuuwe Musa, naye amwite
Mola wake Mlezi! Mimi nachelea asije kubadilishieni dini yenu, au akatangaza uharibifu
katika nchi.
27. Na Musa akasema: Mimi najikinga kwa Mola wangu Mlezi na
Mola wenu Mlezi anilinde na kila mwenye jeuri asiye iamini Siku ya Hisabu.
28. Na akasema mtu mmoja Muumini, aliye kuwa mmoja katika
watu wa Firauni aliye ficha Imani yake: Mtamuuwa mtu kwa sababu anasema Mola
wangu Mlezi ni Mwenyezi Mungu? Na hali naye amekujieni na hoja zilizo wazi? Na
akiwa yeye mwongo basi uwongo wake ni juu yake mwenyewe, na akiwa mkweli
yatakufikieni baadhi ya hayo anayo kuahidini. Hakika Mwenyezi Mungu hamwongoi
apindukiaye mipaka, mwongo mkubwa.
29. Enyi
watu wangu! Leo mna ufalme, mmeshinda katika nchi; basi ni nani atakaye
nisaidia kutuokoa na adhabu ya Mwenyezi Mungu kama ikitufikia? Firauni akasema:
Sikupeni shauri ila ile niliyo iona, wala sikuongozeni ila kwenye njia ya
uwongofu.
30. Na
akasema yule aliye amini: Enyi watu wangu! Hakika mimi nakukhofieni mfano wa siku
za makundi,
31. Mfano
wa hali ya watu wa Nuhu na A'di na Thamudi na wale wa baada yao. Na Mwenyezi
Mungu hataki kuwadhulumu waja.
32. Na
enyi watu wangu! Hakika mimi nakukhofieni Siku ya mayowe.
33. Siku
mtakapo geuka kurudi nyuma. Hamtakuwa na wa kukulindeni kwa Mwenyezi Mungu. Na
mwenye kuhukumiwa na Mwenyezi Mungu kupotea, basi huyo hana wa kumwongoa.
34. Na
alikwisha wajieni Yusuf zamani kwa dalili zilizo wazi, lakini nyinyi mliendelea
katika shaka kwa yale aliyo kuleteeni; mpaka alipo kufa mkasema: Mwenyezi Mungu
hataleta kabisa Mtume baada yake. Kama hivyo Mwenyezi Mungu humwacha kupotea
anaye pindukia mipaka katika maasi anaye jitia shaka.
35. Hao
ambao wanajadiliana katika Ishara za Mwenyezi Mungu pasipo ushahidi wowote ulio
wafikia, ni chukizo kubwa mbele ya Mwenyezi Mungu na mbele ya walio amini. Hivi
ndivyo Mwenyezi Mungu apigavyo muhuri juu ya kila moyo wa jeuri anaye jivuna.
36. Na Firauni akasema: Ewe Hamana! Nijengee mnara ili
nipate kuzifikia njia,
37. Njia za mbinguni ili nikamwone Mungu wa Musa. Na kwa
hakika mimi bila ya shaka namjua kuwa ni mwongo tu. Na hivi ndivyo Firauni
alivyo pambiwa ubaya wa vitendo vyake, na akazuiliwa Njia. Na vitimbi vya
Firauni havikuwa ila katika kuangamia tu.
38. Na yule aliye amini alisema: Enyi watu wangu! Nifuateni
mimi, nitakuongozeni njia ya uwongozi mwema.
39. Enyi
watu wangu! Hakika haya maisha ya dunia ni starehe ipitayo tu, na hakika Akhera
ndiyo nyumba ya daima.
40. Mwenye
kutenda uovu hatalipwa ila sawa na huo uwovu wake, na anaye tenda wema, akiwa mwanamume
au mwanamke, naye ni Muumini, basi hao wataingia Peponi, waruzukiwe humo bila
ya hisabu.
41. Na
enyi watu wangu! Kwa nini mimi nakuiteni kwenye uwokofu, nanyi mnaniita kwenye
Moto?
42.
Mnaniita nimkufuru Mwenyezi Mungu na nimshirikishe na yule ambaye simjui, nami
nakuiteni kwa Mwenye nguvu Mwenye kusamehe?
43. Bila
ya shaka mnaye niitia kumuabudu hastahiki wito duniani wala Akhera. Na hakika
marejeo yetu ni kwa Mwenyezi Mungu. Na wanao pindukia mipaka ndio watu wa
Motoni!
44. Basi
mtayakumbuka ninayo kuambieni. Nami namkabidhi Mwenyezi Mungu mambo yangu.
Hakika Mwenyezi Mungu anawaona waja wake.
45. Basi
Mwenyezi Mungu akamlinda na ubaya wa hila walizo zifanya. Na adhabu mbaya
itawazunguka watu wa Firauni.
46.
Wanaonyeshwa Moto asubuhi na jioni. Na itapo fika Saa ya Kiyama patasemwa:
Waingizeni watu wa Firauni katika adhabu kali kabisa!
47. Na
watapo hojiana huko Motoni, wanyonge watawaambia walio jitukuza: Hakika sisi
tulikuwa wafuasi wenu, basi je, hamtuondolei sehemu ya huu Moto?
48.
Watasema walio jitukuza: Hakika sote sisi tumo humo humo! Kwani Mwenyezi Mungu
kesha hukumu baina ya waja!
49. Na
walio Motoni watawaambia walinzi wa Jahannamu: Mwombeni Mola wenu Mlezi
atupunguzie walau siku moja ya adhabu.
50. Nao
watasema: Je! Hawakuwa wakikufikieni Mitume wenu kwa hoja zilio wazi? Watasema:
Kwani? Watasema: Basi ombeni! Na maombi ya makafiri hayawi ila ni kupotea bure.
|