Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 40. SURAT GHAAFIR (AU AL MUUMIN)
    • 51 - 85
Previous - Next

Click here to hide the links to concordance

51 - 85

51. Hakika bila ya shaka Sisi tunawanusuru Mitume wetu na walio amini katika uhai wa duniani na siku watapo simama Mashahidi,

52. Siku ambayo hautawafaa madhaalimu udhuru wao, nao watapata laana, na watapata makaazi mabaya kabisa.

53. Na kwa hakika tulimpa Musa uwongofu, na tukawarithisha Wana wa Israili Kitabu,

54. Ambacho ni Uwongofu na Ukumbusho kwa wenye akili.

55. Basi subiri. Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni kweli. Na omba msamaha kwa dhambi zako, na umtakase Mola wako Mlezi kwa kumhimidi jioni na asubuhi.

56. Hakika hao wanao bishana katika Ishara za Mwenyezi Mungu bila ya uthibitisho wowote uliyo wajia, hawana vifuani mwao ila kutaka ukubwa tu, na wala huo hawaufikilii. Basi jikinge kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.

57. Bila ya shaka kuumba mbingu na ardhi ni kukubwa zaidi kuliko kuwaumba watu. Lakini watu wengi hawajui.

58. Na kipofu na mwenye kuona hawalingani; na walio amini na watendao mema hawalingani na muovu. Ni machache mnayo yakumbuka.

59. Hakika Saa (ya Kiyama) itafika, nayo haina shaka. Lakini watu wengi hawaamini.

60. Na Mola wenu Mlezi anasema: Niombeni nitakuitikieni. Kwa hakika wale ambao wanajivuna na kuniabudu Mimi wataingia Jahannamu wadhalilike.

61. Mwenyezi Mungu aliye kufanyieni usiku ili mpate kutulia humo, na mchana wa kuonea. Hakika Mwenyezi Mungu bila ya shaka ni Mwenye fadhila juu ya watu, lakini watu wengi hawashukuru.

62. Huyo ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu Mlezi, Muumba wa kila kitu. Hapana mungu ila Yeye; basi mnageuzwa wapi?

63. Namna hivi ndivyo walivyo geuzwa walio kuwa wakizikataa Ishara za Mwenyezi Mungu.

64. Ni Mwenyezi Mungu aliye kufanyieni ardhi kuwa ni pahala pa kukaa, na mbingu kuwa dari. Na akakutieni sura, na akazifanya nzuri sura zenu, na akakuruzukuni vitu vizuri. Huyo ndiye Mwenyezi Mungu Mola wenu Mlezi. Basi ametukuka Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu wote.

65. Yeye ndiye aliye Hai - hapana mungu isipo kuwa Yeye. Basi muabuduni Yeye mkimsafishia Dini Yeye. Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote.

66. Sema: Mimi nimekatazwa kuwaabudu hao mnao waomba badala ya Mwenyezi Mungu, zilipo nijia hoja zilizo dhaahiri kutokana na Mola wangu Mlezi. Na nimeamrishwa nisilimu kwa Mola wa walimwengu wote.

67. Yeye ndiye aliye kuumbeni kwa udongo, kisha kwa tone la manii, kisha kwa pande la damu, kisha akakutoeni katika hali ya mtoto mchanga, kisha mpate kufikilia utu uzima, kisha mpate kuwa wazee. Na kati yenu wapo wanao kufa kabla, na ili mfikie muda ulio kwisha wekwa, na ili mpate kufahamu.

68. Yeye ndiye anaye huisha na anaye fisha. Akihukumu jambo liwe, basi huliambia: Kuwa! Likawa.

69. Je! Huwaoni wale wanao bishana katika Ishara za Mwenyezi Mungu? Wanageuziwa wapi?

70. Ambao wamekanusha Kitabu na yale tuliyo watuma Mitume wetu. Basi watakuja jua.

71. Zitakapo kuwa pingu shingoni mwao na minyororo, huku wanabururwa

72. Katika maji ya moto, kisha wanaunguzwa Motoni,

73. Tena wataambiwa: Wako wapi mlio kuwa mkiwashirikisha

74. Badala ya Mwenyezi Mungu? Watasema: Wametupotea, bali tangu zamani hatukuwa tukiomba kitu! Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu anawaachia makafiri wapotelee mbali.

75. Haya ni kwa sababu mlikuwa mkijitapa katika ardhi pasipo haki, na kwa sababu mlikuwa mkijishaua.

76. Ingieni kwenye milango ya Jahannamu, mdumu humo milele. Basi ni maovu yaliyoje makaazi ya wanao takabari!

77. Basi subiri, hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya kweli. Na ama tukikuonyesha baadhi ya yale tuliyo waahidi au tukikufisha, lakini wao watarudishwa kwetu tu.

78. Na bila ya shaka tuliwatuma Mitume kabla yako. Wengine katika hao tumekusimulia khabari zao, na wengine hatukukusimulia. Na haiwi Mtume alete Ishara yoyote ila kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Basi ikija amri ya Mwenyezi Mungu huhukumiwa kwa Haki, na hapo wapotofu watakhasiri.

79. Mwenyezi Mungu aliye kujaalieni nyama hoa, mifugo, ili muwapande baadhi yao, na muwale baadhi yao.

80. Na katika hao mnayo manufaa kadhaa wa kadhaa, na mnapata kwao haja ziliomo vifuani mwenu; na mnachukuliwa juu yao, na juu ya marikebu.

81. Naye anakuonyesheni Ishara zake. Basi Ishara gani za Mwenyezi Mungu mnazo zikataa?

82. Kwani hawatembei katika ardhi wakaona ulikuwaje mwisho wa walio kuwa kabla yao? Wao walikuwa wengi kuliko hawa, na wamewashinda kwa nguvu na athari katika nchi. Wala hayakuwafaa hayo waliyo kuwa wakiyachuma.

83. Walipo wajia Mitume wao kwa dalili zilizo wazi walijitapa kwa ilimu waliyo kuwa nayo. Basi yakawazunguka waliyo kuwa wakiyafanyia maskhara.

84. Walipo iona adhabu yetu walisema: Tumemuamini Mwenyezi Mungu kuwa ni wa pekee, na tunaikataa miungu tuliyo kuwa tukiishirikisha naye.

85. Lakini imani yao haikuwa yenye kuwafaa kitu wakati ambao wamekwisha iona adhabu yetu. Huu ndio mwendo wa Mwenyezi Mungu ulio kuwa kwa waja wake. Na hapo walio kufuru walikhasiri.

 




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License