43. SURAT AZZUKHRUF
(Imeteremka
Makka)
Imeanzia Sura hii kwa
harufi mbili za alifbete, na ikafuatia kwa kuitaja Qur'ani na kueleza cheo
chake kwa Mwenyezi Mungu. Kisha Sura ikaingia kubainisha msimamo wa wale wanao
zifanyia maskhara Risala za Mitume wao, na ikazileta dalili nyingi za
kuthibitisha Imani ya Mwenyezi Mungu pekee. Na juu ya hoja hizo wao wakamzulia
Mwenyezi Mungu kuwa ana washirika, na wakamfanya kuwa ana watoto wa kike, na
wao wanao wa kiume. Na walipo ishiwa na hoja wakashikilia mila za baba
zao.
Kisha Sura ikasimulia kisa cha Ibrahim, na ikafuatiliza kule kuyaona makuu
makafiri wa Makka ya kwamba Qur'ani iliteremka juu ya Muhammad, wala isiteremke
juu ya mmoja katika wakuu wa miji yao miwili. Hayo ni kama kwamba wao ndio
wanao zigawanya fadhila za Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu alikwisha wagawia
maisha yao ya duniani, kwa kuwa wao wenyewe wameshindwa hayo. Kisha Sura
ikathibitisha kwamba lau kuwa si kuchukia wasije watu wote wakakufuru basi bila
ya shaka angeli mpa kafiri starehe na mapambo na uzuri wote wa duniani.
Kadhaalika Sura imebainisha kwamba mwenye kupuuza Haki Mwenyezi Mungu
humsalitisha na Shet'ani amwongoze kwenye maangamio. Kisha Sura inasimulia kisa
cha Musa na Firauni, na alivyo ghurika Firauni na ufalme wake, na yaliyo
mteremkia Firauni na kaumu yake ya mateso ya Mwenyezi Mungu. Na hayo akafuatiwa
kutajwa Bin Maryamu, na kwamba yeye ni mja aliye neemeshwa na Mwenyezi Mungu,
na akawaita watu wende kwenye Njia Iliyo Nyooka. Na baada ya kuonya kwa adhabu
ya Siku ya Kiyama itayo wapata walio dhulumu, na kubashiriwa Waumini kuwa
watapata Pepo ambayo ndani yake macho yao yatatua, Sura inakhitimisha kueleza
kuwa Ufalme wa Mwenyezi Mungu umeenea kote, na hao walio washirikisha naye
hawanalo wawezalo. Basi, ewe Muhammad! Wapuuzilie mbali, na useme: Salamu!
Watakuja jua!
KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
|