46. SURAT AL AH'QAAF
(Imeteremka
Makka)
Sura hii tukufu inasimulia kuteremka
kwa Qur'ani kutokana na Mwenyezi Mungu, na kupasa kuiamini na kumuamini
Muhammad s.a.w. na kuisadiki Siku ya Kiyama. Na imekusudia kunabihisha watu
wazingatie yaliyo wapata walio tangulia walio muasi Mwenyezi Mungu na Mitume
wake, na imeita watu washughulikie kuwafanyia wema wazazi wawili, na kuzitunza
haki zao. Na hii Sura imeelezea kisa cha baadhi ya majini waliyo isikia ,
wakaambizana waisikilize. Wakaiona kuwa inathibitisha yale yale waliyo kuja
nayo Mitume wa kabla ya Muhammad s.a.w., inaongoa kwendea Haki na kwenye Njia
Iliyo Nyooka. Wakaiamini; na wakawataka wenzao wafuate yale yale. Ikamalizikia
hadithi kwa wito wa kumtaka Nabii s.a.w. avumilie vile anavyo kadhibishwa na
kaumu yake, na kumliwaza katika hayo kwa waliyo yastahamilia Mitume wa kabla
yake wenye azma ngumu.
KWA JINA LA MWENYEZI
MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
1. H'A MIM
2.
Uteremsho wa Kitabu umetoka kwa Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye hikima.
3.
Hatukuziumba mbingu na ardhi wala yaliyomo baina yake ila kwa haki na kwa muda
maalumu. Na walio kufuru wanayapuuza yale wanayo onywa.
4. Je!
Mwawaona wale mnao waomba badala ya Mwenyezi Mungu? Nionyesheni wameumba nini
katika ardhi; au hao wanayo shirika katika mbingu? Nileteeni Kitabu kilicho
kuwa kabla ya hiki, au alama yoyote ya ilimu, ikiwa mnasema kweli.
5. Na nani
mpotofu mkubwa kuliko hao wanao waomba, badala ya Mwenyezi Mungu, ambao
hawatawaitikia mpaka Siku ya Kiyama, na wala hawatambui maombi yao.
6. Na
ambao watu watakapo kusanywa watakuwa maadui zao, na wataikataa ibada yao.
7. Na
wanapo somewa Aya zetu zilizo wazi, walio kufuru husema juu ya haki inapo
wajia: Huu ni uchawi dhaahiri.
8. Au
wanasema: Ameizua mwenyewe! Sema: Ikiwa nimeizua mimi, basi nyinyi hamwezi
kunifaa chochote mbele ya Mwenyezi Mungu. Yeye anajua zaidi hayo mnayo ropokwa;
anatosha kuwa shahidi baina yangu na nyinyi. Na Yeye ndiye Mwenye kusamehe,
Mwenye kurehemu.
9. Sema: Mimi si kiroja miongoni mwa Mitume. Wala sijui
nitakavyo fanywa wala nyinyi. Mimi nafuata niliyo funuliwa tu kwa Wahyi, wala
mimi si chochote ila ni mwonyaji mwenye kudhihirisha wazi.
10. Sema: Mwaonaje yakiwa haya ni kweli yametoka kwa
Mwenyezi Mungu, nanyi mmeyakataa, na akashuhudia shahidi miongoni mwa Wana wa
Israili juu ya mfano wa haya, na akaamini, na nyinyi mnafanya kiburi? Hakika
Mwenyezi Mungu hawaongoi watu wenye kudhulumu.
11. Na walio kufuru waliwaambia walio amini: Lau kuwa hii
ni kheri, wasingeli tutangulia. Na walipo kosa kuongoka wakasema: Huu ni uzushi
wa zamani.
12. Na kabla yake kilikuwapo Kitabu cha Musa, kuwa chenye
uwongozi na rehema. Na hichi ni Kitabu cha kusadikisha na kilicho kuja kwa
lugha ya Kiarabu, ili kiwaonye walio dhulumu, na kiwe ni bishara kwa watendao
mema.
13. Hakika walio sema: Mola wetu Mlezi ni Mwenyezi Mungu;
kisha wakatengenea, hawatakuwa na khofu, wala hawatahuzunika.
14. Hao ndio watu wa Peponi, watadumu humo, kuwa ni malipo
kwa waliyo kuwa wakiyatenda.
15. Na tumemuusia mwanaadamu awatendee wema wazazi wake
wawili. Mama yake amechukua mimba yake kwa taabu, na akamzaa kwa taabu. Na
kuchukua mimba kwake hata kumwachisha ziwa ni miezi thalathini. Hata anapo fika
utu uzima wake, na akafikilia miaka arubaini, husema: Mola wangu Mlezi! Niwezeshe
nishukuru neema zako ulizo nineemesha mimi na wazazi wangu, na nitende mema
unayo yapenda. Na unitengenezee dhuriya zangu. Hakika mimi nimetubu kwako, na
mimi ni miongoni mwa Waislamu.
16. Hao ndio tunao wapokelea bora ya vitendo vyao walivyo
vitenda, na tunayasamehe makosa yao. Watakuwa miongoni mwa watu wa Peponi.
Miadi ya kweli hiyo walio ahidiwa.
17. Na ambaye amewafyonya wazazi wake na akawaambia: Ati
ndio mnanitisha kuwa nitafufuliwa, na hali vizazi vingi vimekwisha pita kabla
yangu! Na hao wazazi humwomba msaada Mwenyezi Mungu (na humwambia mtoto wao):
Ole wako! Amini! Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni kweli. Na yeye husema:
Hayakuwa haya ila ni visa vya watu wa kale.
18. Hao ndio ambao imehakikikishwa hukumu juu yao kama
mataifa yaliyo kwisha pita kabla yao miongoni mwa majini na watu. Hakika hao
wamekuwa wenye kukhasiri.
19. Na wote watakuwa na daraja zao mbali mbali kwa waliyo
yatenda, na ili awalipe kwa vitendo vyao, na wala hawatadhulumiwa.
20. Na siku watakapo letwa walio kufuru kwenye Moto
wataambiwa: Nyinyi mlitwaa vitu vyenu vizuri katika uhai wa duniani, na
mkastareheshwa navyo. Basi leo ndio mnalipwa adhabu ya fedheha kwa mlivyo kuwa
mkitakabari katika ardhi bila ya haki, na kwa sababu mlikuwa mkifanya upotovu.
21. Na mtaje ndugu wa kina A'di, alipo waonya watu wake
kwenye vilima vya mchanga. Na kwa yakini waonyaji wengi walitokea kabla yake na
baada yake kuwaambia: Msimuabudu isipo kuwa Mwenyezi Mungu. Hakika mimi
nakukhofieni isikupateni adhabu ya siku iliyo kuu.
22. Wakasema: Je! Umetujia ili ututenge mbali na miungu
yetu? Basi tuletee hayo unayo tuahidi ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.
23. Akasema: Hakika ujuzi uko kwa Mwenyezi Mungu. Mimi
nakufikishieni niliyo tumwa. Lakini nakuoneni kuwa nyinyi mnafanya ujinga.
24. Basi walipo liona wingu likielekea kwenye mabonde yao,
walisema: Wingu hili la kutunyeshea mvua! Kumbe sivyo, haya ni hayo mliyo
yahimiza, upepo ambao ndani yake imo adhabu chungu!
25. Unaangamiza kila kitu kwa amri ya Mola wake Mlezi.
Wakawa hawaonekani ila nyumba zao tu. Hivyo ndivyo tuwalipavyo wakosefu!
26. Na bila ya shaka tuliwaweka vizuri sio kama tulivyo
kuwekeni nyinyi; na tuliwapa masikio, na macho, na nyoyo. Na hayakuwafaa kitu
masikio yao, wala macho yao, wala nyoyo zao kwa lolote. Kwani hao walikuwa
wakizikataa Ishara za Mwenyezi Mungu, na yale waliyo kuwa wakiyafanyia maskhara
ndiyo yakawazunguka.
27. Na hakika tuliiangamiza miji ilio jirani zenu, na
tulizitumia Ishara ili wapate kurejea.
28. Basi mbona wale walio washika badala ya Mwenyezi Mungu,
kuwa ati hao ndio wawakurubishe, hawakuwanusuru? Bali waliwapotea! Na huo ndio
uwongo walio kuwa wakiuzua.
29. Na wakati tulipo waleta kundi la majini kuja kwako
kusikiliza Qur'ani. Basi walipo ihudhuria walisema: Sikilizeni! Na ilipo kwisha
somwa, walirudi kwa kaumu yao kwenda kuwaonya.
30. Wakasema: Enyi kaumu yetu! Sisi tumesikia Kitabu
kilicho teremshwa baada ya Musa, kinacho sadikisha yaliyo kuwa kabla yake, na
kinacho ongoza kwenye Haki na kwenye Njia Iliyo Nyooka.
31. Enyi kaumu yetu! Muitikieni Mwenye kuitia kwa Mwenyezi
Mungu, na muaminini, Mwenyezi Mungu atakusameheni, na atakukingeni na adhabu
chungu.
32. Na wasio mwitikia Mwitaji wa Mwenyezi Mungu basi hao
hawatashinda katika ardhi, wala hawatakuwa na walinzi mbele yake. Hao wamo
katika upotovu ulio dhaahiri.
33. Je! Hawaoni ya kwamba Mwenyezi Mungu, aliye ziumba
mbingu na ardhi, na hakuchoka kwa kuziumba, kuwa ni Muweza wa kuwafufua wafu?
Kwani? Hakika Yeye ni Muweza wa kila kitu.
34. Na siku watakapo letwa makafiri Motoni wakaambiwa: Je!
Haya si kweli? Watasema: Kwani? Tunaapa kwa Mola wetu Mlezi, ni kweli! Atasema:
Basi onjeni adhabu kwa sababu ya kule kukataa kwenu.
35. Basi subiri, kama walivyo subiri Mitume wenye stahmala
kubwa, wala usiwafanyie haraka. Siku watakayo yaona waliyo ahidiwa itakuwa kama
kwamba hawakukaa ulimwenguni ila saa moja ya mchana. Huu ndio ufikisho! Kwani
huangamizwa wengine isipo kuwa walio waovu tu?
|