51 - 100
51. Huwaoni wale walio pewa sehemu ya Kitabu? Wanaamini
masanamu na Shet'ani! Na wanawasema walio kufuru, kuwa hao wameongoka zaidi
katika njia kuliko Walio amini.
52. Hao ndio Mwenyezi Mungu amewalaani. Na ambaye Mwenyezi
Mungu amemlaani basi hutamwona kuwa na mwenye kumnusuru.
53. Au wanayo sehemu ya utawala? Basi hapo wasingewapa watu
hata tundu ya kokwa ya tende.
54. Au wanawahusudu watu kwa yale aliyo wapa Mwenyezi Mungu
kwa fadhila yake? Basi tuliwapa ukoo wa Ibrahim Kitabu na hikima na tukawapa
utawala mkubwa.
55. Basi wapo miongoni mwao waliyo yaamini, na wapo walio
yakataa. Na Jahannamu yatosha kuwa ni moto wa kuwateketeza.
56. Hakika wale walio zikataa Ishara zetu tutawaingiza
Motoni. Kila zitapo wiva ngozi zao tutawabadilishia ngozi nyengine ili waionje
hiyo adhabu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu na Mwenye hikima.
57. Na wale walio amini na wakatenda mema tutawaingiza
katika Pepo zipitazo mito kati yake kwa kudumu humo milele. Huko watakuwa na
wake walio takasika, na tutawaingiza katika vivuli vizuri kweli.
58. Hakika Mwenyezi Mungu anakuamrisheni mzirudishe amana
kwa wenyewe. Na mnapo hukumu baina ya watu mhukumu kwa uadilifu. Hakika haya
anayo kuwaidhini Mwenyezi Mungu ni mazuri sana. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye
Mwenye kusikia, Mwenye kuona.
59. Enyi mlio amini! Mt'iini Mwenyezi Mungu, na mt'iini
Mtume na wenye madaraka katika nyinyi. Na mkizozana katika jambo basi
lirudisheni kwa Mwenyezi Mungu na Mtume, ikiwa mnamuamini Mwenyezi Mungu na
Siku ya Mwisho. Hayo ndiyo bora zaidi na ndiyo yenye mwisho mwema.
60. Huwaoni wale wanao dai kwamba wameamini yale yaliyo
teremshwa kwako na yaliyo teremshwa kabla yako? Wanataka wakahukumiwe kwa njia
ya upotofu, na hali wameamrishwa wakatae hayo! Na Shet'ani anataka
kuwapotezelea mbali.
61. Na wanapo ambiwa: Njooni kwenye yale aliyo yateremsha
Mwenyezi Mungu, na njooni kwa Mtume; utawaona wanaafiki wanakukwepa kwa
upinzani.
62. Basi inakuwaje unapo wasibu msiba kwa sababu ya yale iliyo
tanguliza mikono yao? Hapo tena hukujia wakiapa kwa Mwenyezi Mungu wakisema:
Hatukutaka ila wema na mapatano.
63. Hao ndio wale ambao Mwenyezi Mungu anayajua yaliyomo
ndani ya nyoyo zao. Basi waachilie mbali, uwape mawaidha na uwaambie maneno ya
kuathiri na kuingia katika nafsi zao.
64. Na hatukumtuma Mtume yeyote ila at'iiwe kwa idhini ya
Mwenyezi Mungu. Na lau pale walipo jidhulumu nafsi zao wangeli kujia,
wakamwomba Mwenyezi Mungu msamaha, na Mtume akawaombea msamaha, hapana shaka
wangeli mkuta Mwenyezi Mungu ni Mwenye kupokea toba na Mwenye kurehemu.
65. La! Naapa kwa Mola wako Mlezi! Hawataamini mpaka
wakufanye wewe ndiye muamuzi katika yale wanayo khitalifiana, kisha wasione
uzito katika nyoyo zao juu ya hukumu utayo toa, na wanyenykee kabisa.
66. Na lau kuwa tumewaamrisha: Jiueni, au tokeni majumbani
kwenu, wasingeli fanya hayo ila wachache tu miongoni mwao. Na lau kama wangeli
fanya walio waidhiwa ingeli kuwa bora kwao na uthibitisho wa nguvu zaidi.
67. Na hapo tunge wapa malipo makubwa kutoka kwetu.
68. Na tungeli waongoa Njia iliyo nyooka.
69. Na wenye kumt'ii Mwenyezi Mungu na Mtume, hao wa pamoja
na wale alio waneemesha Mwenyezi Mungu miongoni mwa Manabii, na Masiddiqi, na
Mashahidi, na Watu wema. Na uzuri ulioje kuwa pamoja na watu hao!
70. Hiyo ni fadhila itokayo kwa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi
Mungu ni Mjuzi wa kutosha.
71. Enyi mlio amini! Chukueni hadhari yenu! Na mtoke kwa
vikosi au tokeni nyote pamoja!
72. Na yupo kati yenu anaye bakia nyuma; na ukikusibuni
msiba husema: Mwenyezi Mungu kanifanyia kheri sikuwa nao.
73. Na ikikufikieni fadhila kutoka kwa Mwenyezi Mungu
husema - kama kwamba hapakuwa mapenzi baina yenu naye: Laiti ningeli kuwa
pamoja nao nikafanikiwa mafanikio makubwa.
74. Basi nawapigane katika Njia ya Mwenyezi Mungu wale
ambao wanao uza uhai wa dunia kwa Akhera. Na anaye pigana katika Njia ya
Mwenyezi Mungu kisha akauliwa au akashinda basi tutakuja mpa ujira mkubwa.
75. Na mna nini msipigane katika Njia ya Mwenyezi Mungu na
ya wale wanao onewa, wanaume na wanawake na watoto, ambao husema: Mola Mlezi
wetu! Tutoe katika mji huu ambao watu wake ni madhaalimu, na tujaalie tuwe na
mlinzi anaye toka kwako, na tujaalie tuwe na wa kutunusuru anaye toka kwako.
76. Walio amini wanapigana katika Njia ya Mwenyezi Mungu,
na walio kufuru wanapiana katika njia ya upotofu. Basi piganeni na marafiki wa
Shet'ani. Hakika hila za Shet'ani ni dhaifu.
77. Je, huwaoni wale walio ambiwa: Izuieni mikono yenu, na
mshike Sala na mtoe Zaka. Na walipo amrishwa kupigana, mara kundi moja kati yao
liliwaogopa watu kama kumwogopa Mwenyezi Mungu, au kwa khofu kubwa zaidi. Na
wakasema: Mola Mlezi wetu! Kwa nini umetuamrisha kupigana? Laiti unge
tuakhirishia kiasi ya muda kidogo hivi! Sema: Starehe ya dunia ni ndogo, na
Akhera ni bora zaidi kwa mwenye kuchamngu. Wala hamtadhulumiwa hata uzi wa
kokwa ya tende.
78. Popote mlipo mauti yatakufikieni, na hata mkiwa katika
ngome zilizo na nguvu. Na likiwafikilia jema wanasema: Hili limetoka kwa Mwenyezi
Mungu. Na likiwafikilia ovu wanasema: Hili limetoka kwako wewe. Sema: Yote
yanatokana na Mwenyezi Mungu. Basi wana nini watu hawa hata hawakaribii
kufahamu maneno?
79. Jema lilio kufikia limetokana na Mwenyezi Mungu. Na ovu
lilio kusibu linatokana na nafsi yako. Nasi tumekutuma kwa watu uwe ni Mtume.
Na Mwenyezi Mungu ni shahidi wa kutosha.
80. Mwenye kumt'ii Mtume basi ndio amemt'ii Mwenyezi Mungu.
Na anaye kengeuka, basi Sisi hatukukutuma wewe uwe ni mlinzi wao.
81. Na wanasema: Tunat'ii. Lakini wanapo toka kwako kundi
moja miongoni mwao hupanga njama usiku kinyume na unayo yasema. Na Mwenyezi
Mungu anayaandika yote hayo wanayo yapangia njama za usiku. Basi waachilie
mbali, na umtegemee Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu ni Mtegemewa wa kutosha.
82. Hebu hawaizingatii hii Qur'ani? Na lau kuwa imetoka kwa
asiye kuwa Mwenyezi Mungu bila ya shaka wangeli kuta ndani yake khitilafu
nyingi.
83. Na linapo wafikia jambo lolote lilio khusu amani au la
kitisho wao hulitangaza. Na lau kuwa wangeli lipeleka kwa Mtume na kwa wenye
mamlaka kati yao, wale wanao chunguza wangeli lijua. Na lau kuwa si fadhila ya
Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake mngeli mfuata Shet'ani ila wachache wenu
tu.
84. Basi pigana katika Njia ya Mwenyezi Mungu. Hukalifishwi
ila nafsi yako tu. Na wahimize Waumini. Huenda Mwenyezi Mungu akayazuia
mashambulio ya walio kufuru. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mkali zaidi wa kushambulia
na Mkali zaidi wa kuadhibu.
85. Mwenye kusaidia msaada mwema ana fungu lake katika
hayo, na mwenye kusaidia msaada mwovu naye ana sehemu yake katika hayo. Na
hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye uweza na ujuzi juu ya kila kitu.
86. Na mnapo amkiwa kwa maamkio yoyote, basi nanyi itikieni
kwa yaliyo bora kuliko hayo, au rejesheni hayo hayo. Hakika Mwenyezi Mungu ni
Mwenye kuhisabu kila kitu.
87.
Mwenyezi Mungu, hapana mungu isipo kuwa Yeye. Kwa yakini atakukusanyeni Siku ya
Kiyama. Halina shaka hilo. Na ni nani msema kweli kuliko Mwenyezi Mungu?
88.
Mmekuwaje kuwa makundi mawili kwa khabari ya wanaafiki, na hali Mwenyezi Mungu
amewageuza kwa sababu ya yale waliyo yachuma? Je! Mnataka kumwona mwongofu
ambaye Mwenyezi Mungu amemhukumu kuwa kapotea? Na aliye mhukumu Mwenyezi Mungu
kuwa amekwisha potea wewe hutampatia njia.
89.
Wanapenda lau kuwa nanyi mnge kufuru kama walivyo kufuru wao, ili muwe sawa
sawa. Basi msiwafanye marafiki miongoni mwao mpaka wahame kwa ajili ya Dini ya
Mwenyezi Mungu. Na wakikengeuka basi wakamateni na wauweni popote mnapo wapata.
Wala msimfanye rafiki katika wao wala msaidizi.
90.
Isipokuwa wale walio fungamana na watu ambao mna ahadi baina yenu na wao, au
wanakujieni na vifua vyao vina dhiki kupigana nanyi, au kupigana na watu wao.
Na lau angeli penda Mwenyezi Mungu angeli wasaliti juu yenu wakapigana nanyi.
Basi wakijitenga nanyi, wasipigane nanyi, na wakakuleteeni amani, basi Mwenyezi
Mungu hakukupeni njia kupigana nao.
91.
Mtawakuta wengine wanataka wapate salama kwenu na salama kwa watu wao. Kila
wakirudishwa kwenye fitna hudidimizwa humo. Ikiwa hawajitengi nanyi, na wakakuleteeni
salama, na wakazuia mikono yao, basi wakamateni na wauweni popote mnapo wakuta.
Na juu ya hao ndio tumekupeni hoja zilizo wazi.
92. Na
haiwi Muumini kumuuwa Muumini ila kwa kukosea. Na mwenye kumuuwa Muumini kwa
kukosea basi amkomboe mtumwa aliye Muumini, na atoe diya kuwapa jamaa za maiti,
isipo kuwa waache wenyewe kuwa ni sadaka. Na akiwa ni jamaa wa maadui zenu,
hali yeye ni Muumini, basi ni kumkomboa mtumwa aliye Muumini. Na akiwa ni
miongoni wa watu ambao pana ahadi baina yenu na wao basi wapewe diya watu wake
na akombolewe mtumwa Muumini. Na asiye pata, basi afunge miezi miwili
mfululizo, kuwa ni toba kwa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi na
Mwenye hikima.
93. Na
mwenye kumuuwa Muumini kwa kukusudia, basi malipo yake ni Jahannamu humo
atadumu, na Mwenyezi Mungu amemkasirikia, na amemlaani, na amemuandalia adhabu
kubwa.
94. Enyi mlio amini! Mnapo safiri katika Njia ya Mwenyezi
Mungu basi hakikisheni, wala msimwambie anaye kutoleeni salamu: Wewe si Muumini;
kwa kutaka manufaa ya maisha ya dunia hii, hali ya kuwa kwa Mwenyezi Mungu zipo
ghanima nyingi. Hivyo ndivyo mlivyo kuwa nyinyi zamani, na Mwenyezi Mungu
akakuneemesheni. Basi chunguzeni sawa sawa. Hakika Mwenyezi Mungu anazo khabari
za mnayo yatenda.
95. Hawawi sawa Waumini wanao kaa tu wala hawanadharura, na
wale wanao pigana katika Njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali yao na nafsi zao.
Mwenyezi Mungu amewatukuza cheo wale wanao pigana kwa mali yao na nafsi zao
kuliko wale wanao kaa tu. Ingawa Mwenyezi Mungu amewaahidi wote mashukio mema,
lakini Mwenyezi Mungu amewafadhili wanao pigana kwa ujira mkubwa kuliko wanao
kaa tu.
96. Ni vyeo hivyo vinavyo toka kwake, na maghfira na
rehema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghfira na Mwenye kurehemu.
97. Hakika Malaika watawaambia wale ambao wamewafisha nao
wamejidhulumu nafsi zao: Mlikuwa vipi? Watasema: Tulikuwa tunaonewa.
Watawaambia: Kwani ardhi ya Mwenyezi Mungu haikuwa na wasaa wa kuhamia humo?
Basi hao makaazi yao ni Jahannamu, nayo ni marejeo mabaya kabisa.
98. Isipo kuwa wale walio kuwa wanyonge miongoni mwa
wanaume na wanawake na watoto wasio na uweza wa hila ya kuongoza njia ya
kuhama.
99. Basi hao huenda Mwenyezi Mungu akawasamehe. Na Mwenyezi
Mungu ni Mwingi wa kusamehe, Mwingi wa maghfira.
100. Na mwenye kuhama katika Njia ya Mwenyezi Mungu atapata
pengi duniani pa kukimbilia, na atapata wasaa. Na anaye toka nyumbani kwake
kuhama kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake, kisha yakamfika mauti njiani
basi umethibiti ujira wake kwa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye
maghfira na Mwenye kurehemu.
|