Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 4. SURAT AN-NISAAI
    • 151 - 176
Previous - Next

Click here to hide the links to concordance

151 - 176

151. Hao ndio makafiri kweli. Na tumewaandalia makafiri adhabu ya kudhalilisha.

152. Na walio muamini Mwenyezi Mungu na Mitume wake, wala wasimfarikishe yeyote kati yao, hao atawapa ujira wao. Na Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghfira, na Mwenye kurehemu.

153. Watu wa Kitabu wanakutaka uwateremshia kitabu kutoka mbinguni. Na kwa hakika walikwisha mtaka Musa makubwa kuliko hayo. Walisema: Tuonyeshe Mwenyezi Mungu wazi wazi. Wakapigwa na radi kwa hiyo dhulma yao. Kisha wakamchukua ndama kumuabudu, baada ya kwisha wajia hoja zilizo wazi. Nasi tukasamehe hayo, na tukampa Musa nguvu zilizo dhaahiri.

154. Na tukanyanyua mlima juu yao kwa kufanya agano nao. Na tukawaambia: Ingilieni mlangoni kwa unyenyekevu. Na tukawaambia: Msiivunje Siku ya Sabato (Jumaa mosi). Na tukachukua kwao ahadi iliyo madhubuti.

155. Basi kwa sababu ya kuvunja kwao ahadi zao, na kuzikataa kwao ishara za Mwenyezi Mungu, na kuwauwa kwao Manabii bila ya haki, na kusema kwao: Nyoyo zetu zimefumbwa; bali Mwenyezi Mungu amezipiga muhuri kwa kufuru zao, basi hawaamini ila kidogo tu -

156. Na pia kwa kufuru zao na kumsingizia kwao Maryamu uwongo mkubwa,

157. Na kwa kusema kwao: Sisi tumemuuwa Masihi Isa, mwana wa Maryamu, Mtume wa Mwenyezi Mungu - nao hawakumuuwa wala hawakumsalibu, bali walifananishiwa tu. Na hakika walio khitalifiana katika haya wamo katika shaka nayo. Wao hawana ujuzi nayo wowote, ila ni kufuata dhana tu. Wala hawakumuuwa kwa yakini.

158. Bali Mwenyezi Mungu alim- tukuza kwake, na hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

159. Na hawi katika Watu wa Kitabu ila hakika atamuamini yeye kabla ya kufa kwake. Naye Siku ya Kiyama atakuwa shahidi juu yao.

160. Basi kwa dhulma yao Mayahudi tuliwaharimishia vitu vizuri walivyo halalishiwa. Na kwa sababu ya kuwazuilia kwao watu wengi na Njia ya Mwenyezi Mungu,

161. Na kuchukua kwao riba, nao wamekatazwa, na kula kwao mali ya watu kwa dhulma. Basi tumewaandalia makafiri katika wao adhabu yenye uchungu.

162. Lakini walio bobea katika ilimu miongoni mwao, na Waumini, wanayaamini uliyo teremshiwa wewe, na yaliyo teremshwa kabla yako. Na wanao shika Sala, na wakatoa Zaka, na wanao muamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho - hao tutawapa malipo makubwa.

163. Hakika Sisi tumekuletea wahyi wewe kama tulivyo wapelekea wahyi Nuhu na Manabii walio kuwa baada yake. Na tulimpelekea wahyi Ibrahim na Ismail na Is-haka na Yaakub na wajukuu zake, na Isa na Ayub na Yunus na Harun na Suleiman, na Daud tukampa Zaburi.

164. Na Mitume tulio kwisha kukuhadithia kabla yake, na Mitume wengine hatukukuhadithia. Na Mwenyezi Mungu alinena na Musa kwa maneno.

165. Mitume hao ni wabashiri na waonyaji, ili watu wasiwe na hoja juu ya Mwenyezi Mungu baada ya kuletewa Mitume. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

166. Lakini Mwenyezi Mungu anayashuhudia aliyo kuteremshia wewe. Ameyateremsha kwa kujua kwake - na Malaika pia wanashuhudia. Na Mwenyezi Mungu anatosha kuwa shahidi.

167. Hakika walio kufuru na wakazuilia Njia ya Mwenyezi Mungu, wamekwisha potelea mbali.

168. Hakika wale walio kufuru na wakadhulumu hawi Mwenyezi Mungu kuwasamehe wala kuwaongoa njia.

169. Isipo kuwa njia ya Jahannamu. Humo watadumu milele. Na hayo kwa Mwenyezi Mungu ni mepesi.

170. Enyi Watu! Amekwisha kujieni Mtume huyu na haki itokayo kwa Mola wenu Mlezi. Basi aminini, ndiyo kheri yenu. Na mkikakanusha basi hakika viliomo mbinguni na duniani ni vya Mwenyezi Mungu tu. Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi Mwenye hikima.

171. Enyi Watu wa Kitabu! Msipite kiasi katika dini yenu, wala msimseme Mwenyezi Mungu ila kwa lilio kweli. Hakika Masihi Isa mwana wa Maryamu ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na neno lake tu alilo mpelekea Maryamu, na ni roho iliyo toka kwake. Basi Muaminini Mwenyezi Mungu na Mitume wake. Wala msiseme: Utatu. Komeni! Itakuwa kheri kwenu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mungu mmoja tu. Ametukuka Yeye na kuwa na mwana. Ni vyake Yeye vyote viliomo katika mbingu na katika ardhi. Na Mwenyezi Mungu ni Mtegemewa wa kutosha.

172. Masihi hataona uvunjifu kuwa mtumwa wa Mwenyezi Mungu, wala Malaika walio karibishwa. Na watakao ona uvunjifu utumwa wa Mwenyezi Mungu na kufanya kiburi, basi atawakusanya wote kwake.

173. Na ama walio amini na wakatenda mema atawalipa ujira wao sawa sawa, na atawazidishia kwa fadhila yake. Na ama wale walio ona uvunjifu na wakafanya kiburi, basi atawaadhibu adhabu iliyo chungu. Wala hawatopata mlinzi wala wa kuwanusuru asiye kuwa Mwenyezi Mungu.

174. Enyi watu! Umekufikieni ushahidi kutoka kwa Mola wenu Mlezi. Na tumekuteremshieni Nuru iliyo wazi.

175. Ama wale walio muamini Mwenyezi Mungu, na wakashikamana naye, basi atawatia katika rehema yake na fadhila, na atawaongoa kwenye Njia Iliyo Nyooka.

176. Wanakuomba uhukumu, sema: Mwenyezi Mungu anakupeni hukumu juu ya mkiwa. Ikiwa mtu amekufa, naye hana mtoto, lakini anaye ndugu wa kike, basi huyo atapata nusu alicho acha maiti. Na mwanamume atamrithi ndugu wa kike ikiwa hana mwana. Na ikiwa wao ni ndugu wa kike wawili, basi watapata thuluthi mbili za alicho acha maiti. Na wakiwa ndugu wanaume na wanawake, basi mwanamume atapata sehemu iliyo sawa na ya wanawake wawili. Mwenyezi Mungu anakubainishieni ili msipotee; na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu.

 




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License