5. SURAT AL MAIDA
(Imeteremka Madina)
Hii Sura ya Madina. Idadi za Aya zake ni 120. Na hii ni katika Sura
zilizo shuka karibu na mwisho. Humu umebainishwa waajibu wa kutimiza maagano,
sawa yakiwa baina ya mja na Mola wake Mlezi, au baina ya watu wenyewe kwa
wenyewe. Na Sura hii imebainisha baadhi ya vyakula vilivyo harimishwa, kama
ilivyo bainisha vilivyo halali, na kuhalalisha kuwaoa wanawake wa Ahlil Kitabi,
Wakristo na Mayahudi. Zimetajwa pia humu nguzo za udhu na kutayamamu.
Kadhaalika imeelezwa kutakikana kufanya uadilifu na adui. Na Sura hii
imeashiria neema za Mwenyezi Mungu juu ya Waislamu, na waajibu wao kukihifadhi
Kitabu chao, na ikaelezea kuwa Mayahudi wameyatengua maneno kutokana na pahala
pake, na Wakristo wakayasahau baadhi ya mambo waliyo kumbushwa, na kwamba wao
wamekufuru kwa kusema kwao kuwa Masihi ni mwana wa Mungu. Kadhaalika Sura hii
inawakanusha Mayahudi na Wakristo kwa yale madai yao kwamba ati wao ni wana wa
Mungu na vipenzi vyake. Kisha tena Sura hii imekusanya baadhi ya khabari za
Mayahudi, kama ilivyo kusanya kisa cha wana wawili wa Adam. Kisa hichi
kinathibitisha kuwa uvamizi na kudhulumiana ni katika tabia za kibinaadamu.
Tena kuwajibika kumtoza kisasi mwenye kudhulumu ni njia ya kuidhibiti tabia hii
mbovu isivuke mpaka! Na Sura Al Maidah imeeleza adhabu ya kumtia adabu mwenye
kufanya fiski na wizi. Tena baadae ikarejea kubainisha vipi Mayahudi walivyo
pindua hukumu za sharia zilizo kuwamo katika Taurati, na ikabainisha kwamba
katika Taurati na Injili ulikuwapo ukweli na haki kabla ya kuchezewa na
kugeuzwa geuzwa. Na ikahakikishwa kuwa ni waajibu kuhukumu kwa mujibu alivyo
teremsha Mwenyezi Mungu. Sura imeashiria juu ya uadui wa Mayahudi na Wakristo
kwa Waumini, na waajibu wa kutowanyenyekea, na kutowaridhia kwa wanayo tenda,
na kuwa ni dharura kuwapinga. Na Sura imethibitisha kuwa Wakristo wamekufuru
kwa kusema kwao Mwenyezi Mungu ni mmoja wa Watatu! Tena Qur'an katika Sura hii
imewasifu baadhi ya Wakristo ambao wameikubali haki na wakaiamini, na
ikamkataza Muumini kujiharimishia mwenyewe vitu vizuri, na ikabainisha nini
kafara ya kuvunja kiapo. Sura hii kadhaalika imeharimisha ulevi kabisa, na
imebainisha ibada za Hija na cheo cha Alkaaba na miezi mitakatifu, na ikaeleza
upotovu wa baadhi ya mambo waliyo jiharimishia Waarabu wenyewe kwa wenyewe bila
ya hoja wala dalili yoyote, kama ilivyo bainisha wasia wakati wa safari.
Mwishoe Sura hii imekhitimisha kwa kutaja miujiza iliyo tokea kwa Nabii Isa
a.s. Na juu ya hiyo miujiza Banu Israili walimkanya. Pia Sura imetaja kuwa
Nabii Isa a.s. hana dhambi ya walio potoka wakamuabudu, na imeeleza Ufalme wa
Mwenyezi Mungu Subhanahu juu ya mbingu na ardhi, na ukamilifu wa uwezo wake.
KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU,
MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU.
|