Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 7. SURAT AL- A'RAAF
    • 101 - 150
Previous - Next

Click here to hide the links to concordance

101 - 150

101. Miji hiyo, tunakusimulia baadhi ya khabari zake. Na hapana shaka Mitume wao waliwafikia kwa hoja zilizo waziwazi. Lakini hawakuwa wenye kuamini waliyo yakanusha zamani. Namna hivi Mwenyezi Mungu anazipiga muhuri nyoyo za makafiri.

102. Wala hatukuwaona wengi wao kuwa wanatimiza ahadi; bali kwa hakika tuliwakuta wengi wao ni wapotofu.

103. Kisha baada yao tukamtuma Musa na Ishara zetu kwa Firauni na waheshimiwa wake. Nao wakazikataa. Basi tazama ulikuwaje mwisho wa waharibifu.

104. Na Musa alisema: Ewe Firauni! Hakika mimi ni Mtume nitokaye kwa Mola Mlezi wa viumbe vyote.

105. Inafaa nisiseme juu ya Mwenyezi Mungu ila lilio la Haki. Nami hakika nimekujieni na dalili waziwazi kutokana na Mola Mlezi wenu. Basi waache Wana wa Israili wende nami.

106. Akasema Firauni: Ikiwa umekuja na Ishara, basi ilete ukiwa ni katika wasemao kweli.

107. Basi akaitupa fimbo yake, na mara ikawa nyoka dhaahiri.

108. Na akatoa mkono wake, mara ukawa mweupe kwa watazamao.

109. Wakasema waheshimiwa wa kaumu ya Firauni: Hakika huyo ni mchawi mjuzi.

110. Anataka kukutoeni katika nchi yenu. Basi mnatoa shauri gani?

111. Wakasema: Mwache kidogo yeye na nduguye, na watume mijini wakusanyao,

112. Wakuletee kila mchawi mjuzi.

113. Wakaja wachawi kwa Firauni, wakasema: Hakika tutapata ujira ikiwa tutashinda.

114. Akasema: Naam! Nanyi bila ya shaka mtakuwa katika wa karibu nami.

115. Wakasema: Ewe Musa! Je, utatupa wewe, au tutakuwa sisi tutao tupa?

116. Akasema: Tupeni! Basi walipo tupa waliyazuga macho ya watu na wakawatia khofu, na wakaleta uchawi mkubwa.

117. Nasi tukamfunulia Musa kumwambia: Tupa fimbo yako. Mara ikavimeza vyote vile walivyo vibuni.

118. Kweli ikathibiti na yakabat'ilika waliyo kuwa wakiyatenda.

119. Kwa hivyo walishindwa hapo, na wakageuka kuwa wadogo.

120. Na wachawi wakapoomoka wakisujudu.

121. Wakasema: Tumemuamini Mola Mlezi wa viumbe vyote,

122. Mola Mlezi wa Musa na Haarun.

123. Akasema Firauni: Mmemuamini kabla sijakupeni idhini? Hizi ni njama mlizo panga mjini mpate kuwatoa wenyewe. Lakini karibu mtajua!

124. Lazima nitaikata mikono yenu na miguu yenu mbali mbali. Kisha nitakutundikeni misalabani.

125. Wakasema: Sisi ni wenye kurejea kwa Mola wetu Mlezi.

126. Nawe hukuudhika nasi ila kwa kuwa tumeziamini Ishara za Mola Mlezi wetu zilipo tujia. Ewe Mola Mlezi wetu! Tumiminie uvumilivu na utufishe hali ni Waislamu.

127. Wakasema waheshimiwa wa kaumu ya Firauni: Unamuacha Musa na watu wake walete uharibifu katika nchi na wakuache wewe na miungu yako? Akasema: Tutawauwa wavulana wao, na tutawaacha hai wanawake wao. Na bila ya shaka sisi ni wenye nguvu juu yao.

128. Musa akawaambia watu wake: Ombeni msaada kwa Mwenyezi Mungu, na subirini. Hakika ardhi ni ya Mwenyezi Mungu. Naye humrithisha amtakaye katika waja wake. Na mwisho ni wa wachamngu.

129. Wakasema: Tumeudhiwa kabla hujatufikia, na baada ya wewe kutujia! Musa akasema: Huenda Mola wenu Mlezi akamhiliki adui wenu, na akakufanyeni nyinyi ndio wa kufuatia kushika nchi, ili atazame mtavyo kuja tenda nyinyi.

130. Na hakika tuliwaadhibu watu wa Firauni kwa miyaka (ya ukame) na kwa upungufu wa mazao, ili wapate kukumbuka.

131. Likiwafika jema wakisema: Haya ni haki yetu. Na likiwafika ovu husema: Musa na walio pamoja naye ni wakorofi. Hakika ukorofi wao huo unao wafikia unatoka kwa Mwenyezi Mungu. Lakini wengi wao hawajui.

132. Na wakisema: Hata ukituletea Ishara yoyote kutuzuga hatuto kuamini.

133. Basi tukawapelekea tufani, na nzige, na chawa, na vyura, na damu, kuwa ni Ishara mbali mbali. Nao wakapanda kiburi, na wakawa watu wakosefu.

134. Na ilipo waangukia adhabu wakasema: Ewe Musa! Tuombee kwa Mola wako Mlezi kwa aliyo kuahidi. Ukituondolea adhabu hii hapana shaka tutakuamini, na tutawaachilia Wana wa Israili wende nawe.

135. Lakini tukiwaondolea adhabu mpaka muda fulani wao waufikie, mara wakivunja ahadi yao.

136. Basi tuliwapatiliza, tuka- wazamisha baharini kwa sababu walizikanusha Ishara zetu, na wakaghafilika nazo.

137. Na tukawarithisha watu walio kuwa wanadharauliwa mashariki na magharibi ya ardhi tuliyo ibariki. Na likatimia neno jema la Mola Mlezi wako juu ya Wana wa Israili, kwa vile walivyo subiri. Na tukayaangamiza aliyo kuwa akiyafanya Firauni na kaumu yake, na waliyo kuwa wakiyajenga.

138. Na tukawavusha bahari Wana wa Israili, wakafika kwa watu wanao abudu masanamu yao. Wakasema: Ewe Musa! Hebu tufanyie na sisi miungu kama hawa walivyo kuwa na miungu. Musa akasema: Hakika nyinyi ni watu msio jua kitu.

139. Hakika haya waliyo nayo watu hawa yatakuja angamia, na hayo waliyo kuwa wakiyafanya yamepotea bure.

140. Akasema: Je, nikutafutieni mungu asiye kuwa Mwenyezi Mungu, na Yeye ndiye aliye kufadhilisheni juu ya viumbe vyote?

141. Na pale tulipo kuokoeni kwa watu wa Firauni walio kupeni adhabu za mwisho wa uovu. Wakiwauwa wavulana wenu, na wakawaacha hai wanawake wenu. Na katika hayo yalikuwa majaribio makubwa kutokana na Mola wenu Mlezi.

142. Tulimuahidi Musa masiku thalathini na tukayatimiza kwa kumi; ikatimia miadi ya Mola wake Mlezi masiku arubaini. Na Musa akamwambia nduguye Haarun: Shika mahala pangu kwa watu wangu na utengeneze wala usifuate njia ya waharibifu.

143. Na alipo kuja Musa kwenye miadi yetu, na Mola wake Mlezi akamsemeza, alisema: Mola wangu Mlezi! Nionyeshe nikutazame. Mwenyezi Mungu akasema: Hutoniona. Lakini utazame huo mlima. Ukibaki pahala pake basi utaniona. Basi alipo jionyesha Mola Mlezi wake kwa mlima, aliufanya uvurugike, na Musa akaanguka chini amezimia. Alipo zindukana alisema: Subhanaka, Umetakasika! Natubu kwako, na mimi ni wa kwanza wa Waumini.

144. (Mwenyezi Mungu) akasema: Ewe Musa! Mimi nimekuteuwa wende kwa watu na Ujumbe wangu na maneno yangu. Basi chukua niliyo kupa na uwe katika wanao shukuru.

145. Na tukamuandikia katika mbao kila kitu, mawaidha na maelezo ya mambo yote. (Tukamwambia): Basi yashike kwa nguvu na uwaamrishe watu wako wayashike kwa ubora wake. Nami nitakuonyesheni makaazi ya wapotofu.

146. Nitawatenga na Ishara zangu wale wanao fanya kiburi katika nchi bila ya haki. Na wao wakiona kila Ishara hawaiamini. Wakiiona njia ya uwongofu hawaishiki kuwa ndiyo njia; lakini wakiiona njia ya upotofu wanaishika kuwa ndiyo njia. Hayo ni kwa sababu wamezikanusha Ishara zetu, na wameghafilika nazo.

147. Na walio zikanusha Ishara zetu na mkutano wa Akhera a'mali zao zimeharibika. Kwani watalipwa ila kwa yale waliyo kuwa wakiyatenda?

148. Na baada yake walimfanya ndama kutokana na mapambo yao (kumuabudu), kiwiliwili tu kilicho kuwa na sauti. Hivyo, hawakuona kuwa hawasemezi wala hawaongoi njia? Wakamuabudu, na wakawa wenye kudhulumu.

149. Na walipo juta na wakaona ya kwamba wamekwisha potea, walisema: Ikiwa Mola wetu Mlezi hakuturehemu na akatusamehe, bila ya shaka tutakuwa miongoni mwa walio khasiri.

150. Na alipo rudi Musa kwa watu wake, naye amekasirika na kuhuzunika, alisema: Ni maovu yalioje mlio nifanyia nyuma yangu! Je, mmeitangulia amri ya Mola wenu Mlezi? Na akaziweka chini zile mbao, na akamkamata kichwa ndugu yake akimvutia kwake. (Haarun) akasema: Ewe mwana wa mama yangu! Hakika hawa watu wamenidharau, na wakakaribia kuniuwa. Basi usiwafurahishe maadui juu yangu, wala usinifanye pamoja na watu madhaalimu.




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License