151 - 200
151.(Musa) akasema: Mola Mlezi wangu! Nisamehe mimi na
ndugu yangu, na ututie katika rehema yako. Nawe ni Mwenye kurehemu kushinda
wote wenye kurehemu.
152. Hakika wale walio muabudu ndama, itawapata ghadhabu ya
Mola wao Mlezi na madhila katika maisha ya dunia. Na hivi ndivyo tunavyo walipa
wazushi.
153. Na walio tenda maovu, kisha wakatubia baada yake na
wakaamini, hapana shaka kuwa Mola Mlezi wako baada ya hayo ni Mwenye kusamehe
Mwenye kurehemu.
154. Na Musa ilipo mtulia ghadhabu aliziokota zile mbao. Na
katika maandiko yake mna uwongofu na rehema kwa wanao mwogopa Mola wao Mlezi.
155. Na Musa akawateuwa watu sabiini katika kaumu yake kwa
miadi yetu. Na ulipo fika mtetemeko mkubwa alisema: Ewe Mola wangu Mlezi!
Ungeli taka ungeli wahiliki wao na mimi zamani! Unatuhiliki kwa waliyo yafanya
wajinga katika sisi? Haya si chochote ila ni mtihani wako, umpoteze umtakaye na
umhidi umtakaye. Wewe ndiye Rafiki Mlinzi wetu. Basi tughufirie na uturehemu.
Na Wewe ndiye mbora wa kughufiria.
156. Na utuandikie mema katika dunia hii na katika Akhera.
Sisi tumerejea kwako. (Mwenyezi Mungu) akasema: Adhabu yangu nitamsibu nayo
nimtakaye. Na rehema yangu imeenea kila kitu. Lakini nitawaandikia khasa wanao
mchamngu, na wanao toa Zaka, na wale ambao wanaziamini Ishara zetu,
157. Ambao kwamba wanamfuata huyo Mtume, Nabii, asiye soma
wala kuandika, wanaye mkuta kaandikwa kwao katika Taurati na Injili, anaye
waamrisha mema na anawakanya maovu, na anawahalalishia vizuri, na ana
waharimishia viovu, na anawaondolea mizigo yao na minyororo iliyo kuwa juu yao.
Basi wale walio muamini yeye, na wakamhishimu, na wakamsaidia, na wakaifuata
nuru iliyo teremshwa pamoja naye - hao ndio wenye kufanikiwa.
158. Sema: Enyi watu! Hakika mimi ni Mtume kwenu nyinyi
nyote, niliye tumwa na Mwenyezi Mungu Mwenye ufalme wa mbingu na ardhi. Hapana
mungu ila Yeye anaye huisha na anaye fisha. Basi muaminini Mwenyezi Mungu na
Mtume wake asiyejua kusoma na kuandika, ambaye anamuamini Mwenyezi Mungu na
maneno yake. Na mfuateni yeye ili mpate kuongoka.
159. Na katika kaumu ya Musa lipo kundi linao waongoa watu
kwa haki na kwa haki wanafanya uadilifu.
160. Na tuliwagawanya katika makabila kumi na mbili,
mataifa mbali mbali. Na tulimfunulia Musa walipo muomba maji watu wake
kumwambia: Lipige hilo jiwe kwa fimbo yako. Mara zikatibuka humo chemchem kumi
na mbili, na kila watu wakajua mahali pao pa kunywea. Na tukawafunika kivuli
kwa mawingu, na tukawateremshia Manna na Salwa. Tukawaambia: Kuleni vizuri hivi
tulivyo kuruzukuni. Wala hawakutu- dhulumu Sisi, bali wamejidhulumu wenyewe.
161. Na pale walipo ambiwa: Kaeni katika mji huu, na mle
humo mpendapo, na semeni: Tufutie dhambi zetu. Na ingieni katika mlango wake
kwa unyenyekevu, tupate kukusameheni makosa yenu. Walio wema tutawazidishia.
162. Lakini walio dhulumu miongoni mwao walibadilisha
kauli, sio ile waliyo ambiwa. Basi tukawapelekea adhabu kutoka mbinguni kwa
vile walivyo kuwa wakidhulumu.
163. Na waulize khabari za mji ulio kuwa kando ya bahari,
wakiivunja Sabato (Jumaamosi ya mapumziko). Samaki walikuwa wakiwajia juu juu
siku ya mapumziko yao, na siku zisio kuwa za kupumzika hawakuwa wakiwajia. Kwa
namna hiyo tuliwajaribu kwa sababu walikuwa wakifanya upotovu.
164. Na kikundi kati yao walisema: Kwa nini mnawawaidhi
watu ambao tangu hapo Mwenyezi Mungu atawateketeza au atawaadhibu adhabu kali?
Wakasema: Ili uwe ni udhuru kwa Mola Mlezi wenu, na huenda nao wakamchamngu.
165. Basi walipo yasahau waliyo kumbushwa, tuliwaokoa walio
kuwa wakikataza maovu, na tukawatesa walio dhulumu kwa adhabu mbaya kwa vile
walivyo kuwa wakifanya upotovu.
166. Walipo jifakharisha katika waliyo kanywa tuliwaambia:
Kuweni manyani wa kudharauliwa.
167. Na pale alipo tangaza Mola wako Mlezi kwamba hapana
shaka atawaletea watu ambao watawaadhibu kwa adhabu mbaya mpaka Siku ya Kiyama.
Hakika Mola wako Mlezi ni Mwepesi wa kuadhibu, na bila ya shaka ni Mwenye
maghfira, na Mwenye kurehemu.
168. Na tuliwafarikisha katika ardhi makundi makundi. Wako
kati yao walio wema, na wengine kinyume cha hivyo. Na tukawajaribu kwa mema na
mabaya ili wapate kurejea.
169. Na wakafuatia baada yao kizazi kibaya walio rithi
Kitabu. Wakashika anasa za haya maisha duni, na wakasema: Tutasamehewa! Na
ikiwajia tena anasa kama hiyo wataishika pia. Je, hawakufanyiwa agano la Kitabu
kuwa wasiseme juu ya Mwenyezi Mungu ila Haki tu? Nao wamekwisha soma yaliomo
humo. Na nyumba ya Akhera ni bora kwa wanao jikinga na maasi. Basi je, hamtii akilini?
170. Na wale
wanao kishikilia Kitabu, na wakashika Sala - hakika Sisi hatupotezi ujira wa
watendao mema.
171. Na pale
tulipo unyanyua mlima juu yao ukawa kama kwamba ni kiwingu kilicho wafunika, na
wakadhani kuwa utawaangukia, (tukawaambia): Kamateni kwa nguvu tuliyo kupeni,
na yakumbukeni yaliyomo ndani yake ili mpate kumcha Mungu.
172. Na pale Mola
wako Mlezi alipo waleta katika wanaadamu kutoka migongoni mwao kizazi chao, na
akawashuhudisha juu ya nafsi zao, akawaambia: Je, Mimi si Mola Mlezi wenu?
Wakasema: Kwani! Tumeshuhudia. Msije mkasema Siku ya Kiyama sisi tulikuwa
tumeghafilika na hayo.
173. Au mkasema:
Hakika baba zetu ndio walio shirikisha kabla yetu, na sisi ni dhuriya zao tu baada
yao. Basi utatuangamiza kwa sababu ya waliyo yafanya wapotovu?
174. Ndio kama
hivyo tunavyo zipambanua Ishara, kwa kutaraji kuwa watarejea.
175. Na wasomee
khabari za yule ambaye tulimpa Ishara zetu, naye akajivua nazo. Na
Shet'ani akamuandama, akawa miongoni walio potea.
176. Na tungelitaka tungeli mtukuza kwa hizo Ishara, lakini
yeye aliushikilia ulimwengu na akafuata pumbao lake. Basi mfano wake ni mfano
wa mbwa. Ukimhujumu hupumua na kutoa ulimi na ukimwacha pia hupumua na kutoa
ulimi. Huo ni mfano wa kaumu wanao zikanusha Ishara zetu. Basi simulia hadithi,
huenda wakatafakari.
177. Huu ni mfano muovu kabisa wa watu wanao kanusha Ishara
zetu na wakajidhulumu nafsi zao.
178. Yule ambaye Mwenyezi Mungu amemhidi basi huyo
amehidika; na alio waacha kupotea basi hao ndio walio khasirika.
179. Na tumeiumbia Jahannamu majini wengi na watu. Wana
nyoyo, lakini hawafahamu kwazo. Na wana macho, lakini hawaoni kwayo. Na wana
masikio, lakini hawasikii kwayo. Hao ni kama nyama howa, bali wao ni wapotofu
zaidi. Hao ndio walio ghafilika.
180. Na Mwenyezi Mungu ana majina mazuri kabisa, basi muombeni
kwa hayo. Na waacheni wale wanao haribu utakatifu wa majina yake. Hao watakuja
lipwa waliyo kuwa wakiyatenda.
181. Na katika tulio waumba wako watu wanao ongoza kwa
Haki, na kwayo wanafanya uadilifu.
182. Na wale walio kadhibisha Ishara zetu, tutawapururia
pole pole kwa namna ambayo wenyewe hawaijui.
183. Nami nitawapa muda. Hakika mpango wangu ni madhubuti.
184. Je, hawafikiri?
Huyu mwenzao hana wazimu. Hakuwa yeye ila ni mwonyaji aliye dhaahiri.
185. Je,
hawatazami ufalme wa mbingu na ardhi, na vitu alivyo viumba Mwenyezi Mungu, na
pengine ajali yao imekwisha karibia? Basi maneno gani baada ya haya
watayaamini?
186. Aliye mwacha Mwenyezi Mungu kupotea hana wa kumwongoa.
Atawaacha hao wakitangatanga katika upotofu wao.
187. Wanakuuliza hiyo Saa (ya mwisho) itakuwa lini? Sema:
Kuijua kwake kuko kwa Mola Mlezi wangu. Haidhihirishi hiyo kwa wakati wake ila
Yeye. Ni nzito katika mbingu na ardhi. Haikujiini ila kwa ghafla tu.
Wanakuuliza kama kwamba wewe una pupa ya kuijua. Sema: Ujuzi wake uko kwa
Mwenyezi Mungu. Lakini aghlabu ya watu hawajui.
188. Sema: Siimilikii nafsi yangu manufaa wala madhara, ila
apendavyo Mwenyezi Mungu. Na lau kuwa ninayajua ya ghaibu ninge jizidishia mema
mengi, wala ovu lisinge nigusa. Mimi si chochote ila ni mwonyaji na mbashiri
kwa watu wanao amini.
189. Yeye ndiye aliye kuumbeni katika nafsi moja; na katika
hiyo hiyo akamfanya mwenzi wake, ili akae naye kwa utulivu. Na anapo muingilia
hubeba mzigo mwepesi, akitembea nao. Anapo kuwa mja mzito, wote wawili humwomba
Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wao: Kama ukitupa mwana mwema tutakuwa katika wanao
shukuru.
190. Basi anapo wapa mwana mwema, wanamfanyia washirikina
Mwenyezi Mungu katika kile kile alicho wapa. Mwenyezi Mungu ametukuka na huko
kushirikisha kwao.
191. Ati wanawafanya viumbe kuwa ni washirika wa Mwenyezi
Mungu, nao hawaumbi, bali wao ndio wanaumbwa?
192. Wala hawana uwezo wa kuwanusuru wala wenyewe
hawajinusuru.
193. Na mkiwaita kwenye uwongofu, hawakufuateni. Ni mamoja
kwenu ikiwa mtawaita au mkinyamaza.
194. Hakika hao mnao waomba asiye kuwa Mwenyezi Mungu ni
waja mfano wenu nyinyi. Hebu waombeni, nao wakuitikieni, kama mnasema kweli.
195. Je,
wao wanayo miguu ya kwendea? Au wanayo mikono ya kutetea? Au wanayo macho ya kuonea? Au wanayo masikio
ya kusikizia? Sema: Iiteni hio miungu yenu ya ushirikina. Kisha nifanyieni mimi
vitimbi, wala msinipe muhula.
196. Hakika
Mlinzi wangu ni Mwenyezi Mungu aliye teremsha Kitabu. Naye ndiye awalindae
walio wema.
197. Na hao mnao
waomba asiye kuwa Mwenyezi hawawezi kukunusuruni, wala hawajinusuru wenyewe.
198. Na mkiwaita
kwenye uwongofu hawasikii. Na unawaona wanakutazama, nao hawaoni.
199. Shikamana
na kusamehe, na amrisha mema, na jitenge na majaahili.
200. Na
uchochezi wa Shet'ani ukikuchochea basi omba ulinzi wa Mwenyezi Mungu. Hakika
Yeye ni Msikizi, Mjuzi.
|