1 - 50
1.
Wanakuuliza juu ya Ngawira. Sema: Ngawira ni ya Mwenyezi Mungu na Mtume. Basi mcheni
Mwenyezi Mungu na suluhisheni mambo baina yenu, na mt'iini Mwenyezi Mungu na
Mtume wake ikiwa nyinyi ni Waumini.
2. Hakika
Waumini ni wale ambao anapo tajwa Mwenyezi Mungu nyoyo zao hujaa khofu, na
wanapo somewa Aya zake huwazidisha Imani, na wakamtegemea Mola wao Mlezi.
3. Hao
ambao wanashika Sala na wanatoa katika yale tunayo waruzuku.
4. Hao
kweli ndio Waumini. Wao wana vyeo, na maghfira, na riziki bora, kwa Mola wao
Mlezi.
5. Kama
Mola wako Mlezi alivyo kutoa nyumbani kwako kwa Haki, na hakika kundi moja la
Waumini linachukia.
6.
Wanajadiliana nawe kwa jambo la Haki baada ya kwisha bainika, kama kwamba
wanasukumwa kwenye mauti nao wanaona.
7. Na
Mwenyezi Mungu alipo kuahidini kuwa moja katika makundi mawili ni lenu. Nanyi
mkapenda lisilo na nguvu ndio liwe lenu; na Mwenyezi Mungu anapenda ahakikishe
Haki kwa maneno yake, na aikate mizizi ya makafiri.
8. Ili
ahakikishe Haki na auvunje upotovu na wangachukia wakosefu.
9. Mlipo
kuwa mkimuomba msaada Mola wenu Mlezi, naye akakujibuni kuwa: Kwa yakini Mimi
nitakusaidieni kwa Malaika elfu wanao fuatana mfululizo.
10. Na
Mwenyezi Mungu hakufanya haya ila kuwa ni bishara na ili nyoyo zenu zituwe. Na
haupatikani ushindi ila kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni
Mwenye nguvu, na Mwenye hikima.
11. Alipo
kufunikeni kwa usingizi uwe ni uaminisho kutoka kwake, na akakuteremshieni maji
kutoka mbinguni ili kukusafisheni kwayo na kukuondoleeni uchafu wa Shet'ani, na
kuzipa nguvu nyoyo zenu, na kuitia imara miguu yenu.
12. Mola
wako Mlezi alipo wafunulia Malaika: Hakika Mimi ni pamoja nanyi, basi watieni
nguvu walio amini. Nitatia woga katika nyoyo za walio kufuru. Basi wapigeni juu
ya shingo na wapigeni kwenye kila ncha za vidole.
13. Hayo
ni kwa sababu wamemuasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na mwenye kumuasi
Mwenyezi Mungu na Mtume wake basi Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.
14. Ndio hivyo! Basi ionjeni! Na bila ya shaka makafiri
wana adhabu ya Moto.
15. Enyi Mlio amini! Mkikutana na walio kufuru vitani
msiwageuzie mgongo.
16. Na atakaye wageuzia mgongo wake siku hiyo - isipo kuwa
kwa mbinu za vita au kuungana na kikosi - basi atakuwa amestahiki ghadhabu ya
Mwenyezi Mungu. Na pahala pake ni Jahannamu, na huo ni mwisho muovu.
17. Hamkuwauwa nyinyi lakini Mwenyezi Mungu ndiye aliye
wauwa. Na wewe hukutupa, walakini Mwenyezi Mungu ndiye aliye tupa, ili
awajaribu Waumini majaribio mema yatokayo kwake. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye
Msikizi na Mjuzi.
18. Ndio hivyo! Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye
kudhoofisha vitimbi vya makafiri.
19. Kama mnataka hukumu basi hukumu imekwisha kujieni. Na
mkiacha itakuwa ndio kheri kwenu. Na mkirejea Sisi pia tutarejea. Na jeshi lenu
halitakufaeni kitu, japo likiwa kubwa. Kwani hakika Mwenyezi yu pamoja na
Waumini.
20. Enyi mlio amini! Mt'iini Mwenyezi Mungu na Mtume wake,
wala msijiepushe naye, nanyi mnasikia.
21. Wala msiwe kama wale wanao sema: Tumesikia, na kumbe
hawasikii.
22. Hakika vinyama viovu mbele ya Mwenyezi Mungu ni vile
viziwi na bubu visio tumia akili zao.
23. Na Mwenyezi Mungu angeli jua wema wowote kwao ange
wasikilizisha, na lau ange wasikilizisha wangeli geuka wakapuuza.
24. Enyi mlio amini! Muitikieni Mwenyezi Mungu na Mtume
anapo kuitieni jambo la kukupeni uzima wa milele. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu
huingia kati ya mtu na moyo wake, na kwamba hakika kwake Yeye tu mtakusanywa.
25. Na jikingeni na Fitna ambayo haitowasibu walio dhulumu
peke yao kati yenu. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.
26. Na kumbukeni mlipo kuwa wachache, mkionekana wanyonge
katika nchi, mnaogopa watu wasikunyakueni, naye akakupeni pahala pazuri pa
kukaa, na akakutieni nguvu kwa nusura yake, na akakupeni riziki nzuri ili mpate
kushukuru.
27. Enyi mlio amini! Msimfanyie khiana Mwenyezi Mungu na
Mtume, wala msikhini amana zenu, nanyi mnajua.
28. Na jueni ya kwamba mali zenu na wana wenu ni Fitna
(mtihani), na kwamba kwa Mwenyezi Mungu upo ujira mkubwa.
29. Enyi mlio amini! Mkimcha Mwenyezi Mungu atakupeni
kipambanuo, na atakufutieni makosa, na atakusameheni, na Mwenyezi Mungu ni
Mwenye fadhila kubwa.
30. Na walipo kupangia mpango walio kufuru wakufunge, au
wakuuwe, au wakutoe. Wakapanga mipango yao, na Mwenyezi Mungu akapanga yake. Na
Mwenyezi Mungu ndiye mbora wa mipango.
31. Na wanapo somewa Aya zetu, wao husema: Tumesikia. Na
lau tungeli penda tunge sema kama haya. Haya si chochote ila hadithi za watu wa
kale tu.
32. Na walipo sema: Ee Mwenyezi Mungu! Ikiwa haya ni kweli
itokayo kwako basi tunyeshee mawe kutoka mbinguni, au tuletee adhabu yoyote
iliyo chungu.
33. Na Mwenyezi Mungu hakuwa wa kuwaadhibu nawe umo pamoja
nao, wala Mwenyezi Mungu si wa kuwaadhibu na hali ya kuwa wanaomba msamaha.
34. Lakini wana jambo gani hata Mwenyezi Mungu asiwaadhibu,
na hali ya kuwa wanawazuilia watu Msikiti Mtakatifu? Wala wao hawakuwa ndio
walinzi wake, bali walinzi wake hawakuwa ila wacha-Mngu tu. Lakini wengi katika
wao hawajui.
35. Na haikuwa ibada yao kwenye hiyo Nyumba (Al Kaaba) ila
ni kupiga miunzi na makofi. Basi onjeni adhabu kwa vile mlivyo kuwa mkikufuru.
36. Hakika wale walio kufuru hutoa mali yao ili kuzuilia
Njia ya Mwenyezi Mungu. Basi watayatoa, kisha yatakuwa juu yao majuto, na kisha
watashindwa. Na wale walio kufuru watakusanywa kwenye Jahannam.
37. Ili Mwenyezi Mungu apate kuwa pambanua walio waovu na
walio wema, na kuwaweka waovu juu ya waovu wengine, na kuwarundika wote pamoja,
na kuwatupa katika Jahannam. Hao ndio walio khasirika.
38. Waambie wale walio kufuru: Wakikoma watasamehewa yaliyo
kwisha pita. Na wakiyarudia basi imekwisha pita mifano ya wa zamani.
39. Na piganeni nao mpaka isiwepo fitna na mateso, na Dini
yote iwe kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Lakini wakiacha, basi hakika Mwenyezi
Mungu anayaona wanayo yatenda.
40. Na kama wakigeuka basi jueni kwamba Mwenyezi Mungu
ndiye Mola wenu, ni Mola Mwema na Msaidizi Mwema.
41. NA JUENI ya kwamba ngawira mnayo ipata, basi khums
(sehemu moja katika tano) ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na Mtume, na jamaa, na
mayatima, na masikini, na wasafiri, ikiwa nyinyi mmemuamini Mwenyezi Mungu na
tuliyo yateremsha kwa mja wetu siku ya kipambanuo, siku yalipo kutana majeshi
mawili. Na Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu.
42. Kumbukeni pale mlipo kuwa nyinyi kwenye ng'ambo ya
karibu ya bonde, na wao wakawa ng'ambo ya mbali, na msafara ulipo kuwa chini
yenu. Na ingeli kuwa mmeagana mngeli khitalifiana katika miadi. Lakini
(mkakutana) ili Mwenyezi Mungu atimize jambo lilio kuwa lazima litendeke, kwa
sababu aangamie wa kuangamia kwa dalili zilizo dhaahiri, na asalimike wa
kusalimika kwa dalili zilizo dhaahiri. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia
Mwenye kujua.
43. Kumbuka alipo kuonyesha usingizini mwako kwamba wao ni
wachache - na lau angeli kuonyesha kuwa ni wengi, mngeli ingiwa na woga, na
mngeli zozana katika jambo hilo. Lakini Mwenyezi Mungu kakuvueni. Hakika Yeye
ni Mwenye kuyajua yalio vifuani.
44. Na mlipo kutana akakuonyesheni machoni mwenu kuwa wao
ni wachache, na akakufanyeni nyinyi ni wachache machoni mwao, ili Mwenyezi
Mungu atimize jambo lilio kuwa liwe. Na mambo yote hurejezwa kwa Mwenyezi
Mungu.
45. Enyi mlio amini! Mkikutana na jeshi, basi kueni imara,
na mkumbukeni Mwenyezi Mungu sana ili mpate kufanikiwa.
46. Na mt'iini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wala msizozane
mkaingiwa woga, na zikapotea nguvu zenu. Na subirini. Hakika Mwenyezi Mungu yu
pamoja na wanao subiri.
47. Wala msiwe kama wale walio toka majumbani mwao kwa
fakhari na kujionyesha kwa watu, na wakawazuilia watu Njia ya Mwenyezi Mungu.
Na Mwenyezi Mungu ameyazunguka yote wanayo yafanya.
48. Na pale Shet'ani alipo wapambia vitendo vyao, na
akawaambia: Hapana watu wa kukushindeni hii leo, na hali mimi ni mlinzi wenu.
Yalipo onana majeshi mawili, akarudi nyuma, na akasema: Mimi si pamoja nanyi.
Mimi naona msiyo yaona. Mimi namwogopa Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu ni
mkali wa kuadhibu.
49. Na walipo sema wanaafiki, na wale wenye ugonjwa nyoyoni
mwao: Watu hawa dini yao imewadanganya. Na Mwenye kumtegemea Mwenyezi Mungu
basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu Ametukuka, na Mwenye hikima.
50. Na laiti ungeli ona Malaika wanapo wafisha wale walio
kufuru wakiwapiga nyuso zao na migongo yao, na kuwaambia: Ionjeni adhabu ya
Moto!
|