Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 9. SURATUT TAWBA
Previous - Next

Click here to show the links to concordance

9. SURATUT TAWBA

(Imeteremka Madina)

Suratut Tawba iliteremka Madina katika mwaka wa tisa wa Hijra, yaani miaka tisa baada ya Mtume s.a.w. kuhamia Madina. Akaichukua Sura hii Ali bin Abi Talib r.a. kuwapelekea Waislamu katika Hija na akawasomea. Na amir, yaani mwongozi, wa Hija hiyo alikuwa Abu Bakr Assidiq r.a. Na Aya zake ni 129. Imeanzia kwa kujitenga Mwenyezi Mungu Mtukufu na washirikina. Na kwa hivyo ikaitwa pia Sura ya Baraa-ah, yaani kujitenga, kutokuwa na dhima, kutokuwa na jukumu. Na baada ya hayo ikataja utakatifu wa miezi mitakatifu, na ahadi za washirikina, na ipasavyo kutimiza ahadi nao ikiwa wao hawajaivunja. Na mwenye kuvunja ahadi yapasa kupigana naye. Na baada ya hayo ikabainisha kuwa kiini cha kutaka kumkaribia Mwenyezi Mungu Mtukufu ni kumuamini Yeye. Na Imani haikamiliki ila akiwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake wanapendwa na Waumini kuliko kila kitu. Naye Subhanahu ametaja kuwa kujiona una nguvu ndio kunapelekea kuwa mbali ushindi, na akaashiria mfano wa vita vya Hunayni. Katika Sura hii wamepigiwa marfuku washirikina wasiingie katika Msikiti Mtakatifu wa Makka, kwa kuwa wao ni najisi!
Na katika Sura hii imetajwa kupasa kuwapiga vita Mayahudi na Wakristo mpaka watoe jizya, kodi ya kichwa, na imebainishwa idadi ya miezi mitakatifu. Na humu imebainishwa dharura ya kutoka kwenda vitani kila vikinadiwa bila ya kulegalega. Na humo imeashiriwa hukumu ya wanao bakia nyuma, na walemevu wasio weza kwenda kupigana, na imebainishwa hali ya wanaafiki ambao wanatafuta fitna kila wakati vinapo nadiwa vita. Na Mwenyezi Mungu akataja wanaafiki wanavyo watendea Waumini wakati wa salama na vita.
Katika Sura hii iko amri ya kukata iliyo tangazwa kuwatia adabu wanaafiki. Nayo ni kuwa Mtume s.a.w. asimsalie yeyote katika wanaafiki akifa. Naye Subhanahu ametaja udhuru unao mstahikia mtu kubaki nyuma asende vitani. Na pia Subhanahu ameeleza hali ya wale mabedui walio dhihirisha kuingia katika Uislamu, au wakafuata hukumu zake, baada ya kuwa Uislamu umepata nguvu. Na akaeleza kuwa hao mabedui wako kando kando ya Madina.
Na baada ya hayo ametaja hali za watu kwa mnasaba wa Imani. Na akataja khabari ya Msikiti wa Madhara walio ujenga wanaafiki ili upuuzwe Msikiti alio ujenga Mtume wa Mwenyezi Mungu s.a.w. Kisha Subhanahu akataja sifa za Waumini walio wakweli katika Imani yao, na toba ya wale walio mkhalifu Mtume wa Mwenyezi Mungu s.a.w., na Mwenyezi Mungu akakubali toba hiyo, kama alivyo taja Subhanahu wa Taa'la hali za watu katika kuzipokea Aya za Qur'ani zinapo teremka. Na Subhanahu wa Taala akakhitimisha Sura hii kwa kusema kuwa hakika Mwenyezi Mungu Mtukufu amemteua Muhammad kwa kumpa Utume, na kwamba yeye hawatakii shida hao alio tumwa kwao, na kwamba yeye ni mpole na mwenye huruma kwao, na kwamba ikiwa wakigeuka basi Mwenyezi Mungu anamtosheleza. (Angalia: Sura hii peke yake ndiyo haianzii kwa Bismillahi, Kwa Jina la Mwenyezi Mungu.)




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License