1 - 50
1. Alif Lam Raa. Hizi ni Aya za Kitabu kinacho bainisha.
2. Hakika Sisi tumeiteremsha Qur'ani kwa Kiarabu ili mpate
kuzingatia.
3. Sisi tunasimulia simulizi nzuri kwa kukufunulia Qur'ani
hii. Na ijapo kuwa kabla ya haya ulikuwa miongoni mwa wasio jua.
4. Yusuf alipo mwambia baba yake: Ewe babaangu! Hakika mimi
nimeota nyota kumi na moja, na jua, na mwezi. Nimeota zikinisujudia.
5. (Baba) akasema: Ewe mwanangu! Usiwasimulie nduguzo ndoto
yako, wasije wakakufanyia vitimbi. Hakika Shet'ani ni adui aliye dhaahiri kwa
mwanaadamu.
6. Na kadhaalika Mola wako Mlezi atakuteuwa na
atakufundisha tafsiri ya mambo. Na atatimiza neema zake juu yako na juu ya ukoo
wa Yaa'qub, kama alivyo watimizia hapo zamani baba zako Ibrahim na Is-haq.
Hakika Mola wako Mlezi ni Mjuzi Mwenye hikima.
7. Kwa yakini katika Yusuf na nduguze ziko ishara kwa wanao
uliza.
8. Pale walipo sema: Hakika Yusuf na nduguye wanapendwa
zaidi na baba yetu kuliko sisi, hali sisi ni kikundi chenye nguvu. Hakika baba
yetu yumo katika upotofu wa dhaahiri.
9. Muuweni Yusuf, au mtupeni nchi mbali ili uso wa baba
yenu ukuelekeeni nyinyi. Na baada ya haya mtakuwa watu wema.
10. Akasema msemaji kati yao: Msimuuwe Yusuf. Lakini
mtumbukizeni ndani ya kisima. Wasafiri watakuja mwokota; kama nyinyi mna sharti
ya kufanya jambo.
11.
Wakasema: Ewe baba yetu! Una nini hata hutuamini kwa Yusuf? Na hakika
sisi ni wenye kumtakia kheri!
12. Mpeleke kesho pamoja nasi, ale kwa furaha na acheze; na
bila ya shaka sisi tutamhifadhi.
13. Akasem: Kwa hakika inanihuzunisha kwamba nyinyi mwende
naye, na ninaogopa asije mbwa mwitu akamla nanyi mmeghafilika naye.
14. Wakasema: Ikiwa mbwa mwitu atamla na hali sisi ni kundi
lenye nguvu kabisa, basi bila ya shaka sisi tutakuwa khasarani.
15. Basi walipo mchukua na wakakubaliana wamtumbukize ndani
ya kisima, tulimfunulia Yusuf: Hapana shaka yoyote utakuja waambia kwa jambo
lao hili, na wala wao hawatambui.
16. Wakaja kwa baba yao usiku wakilia.
17.
Wakasema: Ewe baba yetu! Hakika tulikwenda kushindana na tukamwacha Yusuf penye
vitu vyetu. Basi mbwa mwitu akamla. Lakini wewe hutuamini ijapo kuwa tunasema
kweli.
18. Wakaja
na kanzu yake ina damu ya uwongo. Akasema: Bali nafsi zenu zimekushawishini
kutenda kitendo. Lakini subira ni njema; na Mwenyezi Mungu ndiye wa kuombwa
msaada kwa haya mnayo yaeleza.
19.
Ukafika msafara, wakamtuma mchota maji wao, naye akatumbukiza ndoo yake.
Alisema: Kheri Inshallah! Huyu hapa mvulana! Wakamficha ili kumfanya ni bidhaa.
Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa wanayo yatenda.
20. Na
wakamuuza kwa thamani duni, kwa akali ya pesa. Wala hawakuwa na haja naye.
21. Na yule
aliye mnunua huko Misri alimwambia mkewe: Mtengenezee makaazi ya hishima huyu;
huenda akatufaa au tukamfanya mwenetu. Na kama hivyo tulimweka Yusuf katika
nchi ili tumfundishe kufasiri mambo. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kushinda
katika jambo lake, lakini watu wengi hawajui.
22. Na alipo fikilia utu uzima tulimpa hukumu na ilimu. Na
kama hivi tunawalipa wanao tenda mema.
23. Na yule bibi wa nyumba aliyo kuwamo Yusuf alimtamani
kinyume cha nafsi yake, na akafunga milango. Akamwambia: Njoo! Yusuf akasema:
Audhubillahi! Najikinga na Mwenyezi Mungu. Huyu bwana wangu kaniweka maskani
nzuri, na hakika wenye kudhulumu hawatengenekewi.
24. Na hakika yule mwanamke alimtamani, na Yusuf angeli
mtamani lau kuwa hakuona ishara ya Mola wake Mlezi. Hayo hivyo ni kwa ajili
tumuepushe na uovu na uchafu. Hakika yeye alikuwa katika waja wetu walio
safishwa.
25. Na wote wawili wakakimbilia mlangoni, na mwanamke
akairarua kanzu yake Yusuf kwa nyuma. Na wakamkuta bwana wake mlangoni.
Mwanamke akasema: Hapana malipo ya mwenye kutaka kumfanyia maovu mkeo isipo
kuwa kufungwa au kupewa adhabu chungu.
26. Yusuf akasema: Yeye ndiye aliye nitaka bila ya mimi
kumtaka. Na shahidi aliye kuwa katika jamaa za mwanamke alisema: Ikiwa kanzu
yake imechanwa mbele basi mwanamke amesema kweli, naye Yusuf ni katika waongo.
27. Na ikiwa kanzu yake imechanwa nyuma, basi mwanamke
amesema uwongo, naye Yusuf ni katika wakweli.
28. Basi yule bwana alipoona kanzu yake imechanwa kwa
nyuma, alisema: Hakika haya ni katika vitimbi vyenu wanawake. Bila ya shaka
vitimbi vyenu ni vikuu.
29. Yusuf!
Wachilia mbali haya. Na wewe, mwanamke, omba msamaha kwa dhambi zako.
Kwa hakika wewe ni katika walio fanya makosa.
30. Na wanawake wa mjini wakawa wanasema: Mke wa Mheshimiwa
anamtamani mtumishi wake ! Hakika
amesalitika kwa mapenzi. Sisi hakika tunamwona yumo katika upotovu ulio
dhaahiri.
31. Alipo sikia
yule bibi masengenyo yao aliwaita, na akawawekea matakia ya kuegemea, na akampa
kila mmoja wao kisu. Akamwambia Yusuf: Tokeza mbele yao. Basi walipo mwona
waliona ni kitu kikubwa kabisa, na wakajikata mikono yao. Wakasema:
Hasha Lillahi! Huyu si mwanaadamu. Hakuwa huyu ila ni Malaika mtukufu.
32. Yule bibi aksema: Huyu basi ndiye huyo mliye nilaumia!
Na kweli mimi nilimtaka naye akakataa. Na akitofanya ninayo muamrisha basi
hapana shaka atafungwa gerezani, na atakuwa miongoni mwa walio chini kabisa.
33. Yusuf akasema: Ee Mola Mlezi wangu! Nastahabu kifungo
kuliko haya anayo niitia. Na usipo niondoshea vitimbi vya wanawake mimi
nitamili kwao, na nitakuwa katika wajinga.
34. Basi Mola wake Mlezi akamwitikia, na akamwondoshea
vitimbi vyao. Hakika Yeye ni Msikizi Mjuzi.
35. Basi ikawadhihirikia baada ya kuona Ishara kuwa
wamfunge kwa muda.
36. Wakaingia gerezani pamoja naye vijana wawili. Mmoja wao
akasema: Hakika mimi nimeota nakamua mvinyo. Na mwingine akasema: Mimi nimeota
nimebeba mikate juu ya kichwa changu, na ndege wanaila. Hebu tuambie tafsiri
yake, kwani sisi tunakuona wewe ni katika watu wema.
37. Akasema: Hakitakufikilieni chakula mtakacho pewa ila
nitakwambieni hakika yake kabla hakijakufikieni. Haya ni katika yale aliyo
nifundisha Mola wangu Mlezi. Hakika mimi nimeacha mila ya watu wasio muamini
Mwenyezi Mungu, na wakawa hawaiamini Akhera.
38. Na nimefuata mila ya baba zangu, Ibrahim, na Is-haq, na
Yaa'qub. Hatuna haki ya kumshirikisha Mwenyezi Mungu na chochote. Hiyo ni
katika fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yetu na juu ya watu; lakini watu wengi
hawashukuru.
39. Enyi wafungwa wenzangu wawili! Je, mabwana wengi wanao
farikiana wao kwa wao ni bora au Mwenyezi Mungu Mmoja Mwenye nguvu?
40. Hamuabudu badala yake ila majina tu mliyo yapanga
nyinyi na baba zenu. Mwenyezi Mungu hakuyateremshia hayo uthibitisho wowote. Hapana
hukumu ila ya Mwenyezi Mungu tu. Yeye ameamrisha msimuabudu yeyote isipo kuwa
Yeye tu. Hiyo ndiyo Dini Iliyo Nyooka. Lakini watu wengi hawajui.
41. Enyi wafungwa wenzangu wawili! Ama mmoja wenu
atamnywesha bwana wake mvinyo. Na ama mwengine atasulubiwa, na ndege watamla
kichwa chake. Imekwisha katwa hukumu ya hilo jambo mlilo kuwa mkiuliza.
42. Na akamwambia yule aliye jua kuwa atavuka katika wale
wawili: Nikumbuke kwa bwana wako. Lakini Shet'ani alimsahaulisha kumtaja kwa
bwana wake. Basi Yusuf akakaa gerezani miaka kadhaa.
43. Na siku moja mfalme alisema: Hakika mimi nimeota
ng'ombe saba wanene wanaliwa na ng'ombe saba walio konda. Na mashuke saba
mabichi na mengine makavu. Enyi waheshimiwa! Nambieni maana ya ndoto zangu,
ikiwa nyinyi mnaweza kuagua ndoto.
44. Wakasema: Hizi ni ndoto zilizo paraganyika, wala sisi
sio wenye kujua tafsiri ya ndoto hizi.
45. Hapo akasema yule aliye okoka katika wale wawili
akakumbuka baada ya muda: Mimi nitakwambieni tafsiri yake. Basi nitumeni.
46. Yusuf! Ewe mkweli! Tueleze nini maana ya ng'ombe saba
wanene kuliwa na ng'ombe saba walio konda. Na mashuke saba mabichi na mengine
makavu, ili nirejee kwa watu wapate kujua.
47. Akasema: Mtalima miaka saba kwa juhudi. Mtacho vuna
kiwacheni katika mashuke yake, isipo kuwa kidogo mtacho kula.
48. Kisha itakuja baadaye miaka saba ya shida itakayo kula
kile mlicho iwekea isipo kuwa kidogo mtacho kihifadhi.
49. Kisha baada ya haya utakuja mwaka ambao katika mwaka
huo watu watasaidiwa, na watakamua.
50. Na mfalme akasema: Mleteni kwangu! Basi mjumbe alipo
mjia Yusuf alisema: Rejea kwa bwana wako ukamuulize khabari ya wale wanawake
walio jikata mikono yao. Hakika Mola wangu Mlezi anazijua vyema hila zao.
|