Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 16. SUURAT AN NAH'L
    • 1 - 50
Previous - Next

Click here to show the links to concordance

1 - 50

1. Amri ya Mwenyezi Mungu itafika tu. Basi msiihimize. Ametakasika na Ametukuka na wanayo mshirikisha nayo.

2. Huwateremsha Malaika na Roho kwa amri yake juu ya amtakaye katika waja wake ili nyinyi muonye kwamba hapana mungu ila Mimi, basi nicheni Mimi.

3. Ameziumba mbingu na ardhi kwa Haki. Ametukuka na wanayo shirikisha.

4. Amemuumba mtu kwa tone la manii. Naye mara amekuwa mshindani dhaahiri.

5. Na nyama hoa amekuumbieni. Katika hao mna vifaa vya kutia joto, na manufaa mengineyo, na baadhi yao mnawala.

6. Na wanakupeni furaha pale mnapo warudisha jioni na mnapo wapeleka malishoni asubuhi.

7. Na hubeba mizigo yenu kupeleka kwenye miji msiyo weza kuifikia ila kwa mashaka ya nafsi. Hakika Mola wenu Mlezi ni Mpole na Mwenye kurehemu.

8. Na farasi, na nyumbu, na punda ili muwapande, na kuwa ni pambo. Na ataumba msivyo vijua.

9. Na ni juu ya Mwenyezi Mungu kuelekeza Njia. Na zipo njia za upotovu. Na angeli penda angeli kuongoeni nyote.

10. Yeye ndiye anaye kuteremshieni maji kutoka mbinguni. Katika hayo nyinyi mnapata ya kunywa, na miti ya kulishia.

11. Kwa hayo Yeye anaizalisha kwa ajili yenu mimea, na mizaituni, na mitende, na mizabibu, na kila namna ya matunda. Hakika katika haya zipo ishara kwa watu wanao fikiri.

12. Na amefanya ukutumikieni usiku na mchana, na jua na mwezi, na nyota zikutumikieni kwa amri yake. Hakika katika hayo zipo ishara kwa watu wenye akili.

13. Na hivi alivyo vieneza katika ardhi vya rangi mbali mbali. Hakika katika hayo ipo ishara kwa watu wanao waidhika.

14. Yeye ndiye aliye ifanya bahari ikutumikieni, ili kutokana na humo mpate kula nyama laini, na mtoe humo mapambo mnayo yavaa. Na unaona marikebu zikikata maji humo, ili mtafute fadhila yake, na mpate kushukuru.

15. Na kaweka katika ardhi milima ili ardhi isiyumbe yumbe nanyi. Na mito, na njia ili mpate kuongoka.

16. Na alama nyengine. Na kwa nyota wao wanajiongoza.

17. Ati anaye umba ni kama asiye umba? Basi hebu, hamkumbuki?

18. Na mkizihisabu neema za Mwenyezi Mungu, hamwezi kuzidhibiti. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye maghfira, Mwenye kurehemu.

19. Na Mwenyezi Mungu anayajua mnayo yaficha na mnayo yatangaza.

20. Na wale wanao waomba wasio kuwa Mwenyezi Mungu hawaumbi kitu, bali wao wameumbwa.

21. Ni wafu si wahai, na wala hawajui watafufuliwa lini.

22. Mungu wenu ni Mungu Mmoja. Lakini wasio iamini Akhera nyoyo zao zinakataa, nao wanajivuna.

23. Hapana shaka kuwa hakika Mwenyezi Mungu anayajua wanayo yaficha na wanayo yatangaza. Kwa hakika Yeye hawapendi wanao jivuna.

24. Na wanapo ambiwa: Kateremsha nini Mola wenu Mlezi? Husema: Hadithi za kubuni za watu wa kale!

25. Ili wabebe mizigo yao kwa ukamilifu Siku ya Kiyama, na sehemu ya mizigo ya wale wanao wapoteza bila ya kujua. Angalia, ni maovu mno hayo wanayo yabeba!

26. Walipanga vitimbi walio kuwa kabla yao, Mwenyezi Mungu akayasukua majengo yao kwenye misingi, dari zikawaporomokea juu yao, na adhabu ikawajia kutoka wasipo kujua.

27. Kisha Siku ya Kiyama atawahizi na atasema: Wako wapi hao washirika wangu ambao kwao mkiwakutisha (Manabii) mashaka? Watasema walio pewa ilimu: Hakika leo ndiyo hizaya na adhabu itawashukia makafiri,

28. Ambao Malaika waliwafisha nao wamejidhulumu nafsi zao! Basi watasalimu amri, waseme: Hatukuwa tukifanya uovu wowote. (Wataambiwa): Kwani! Hakika Mwenyezi Mungu anajua sana mliyo kuwa mkiyatenda.

29. Basi ingieni milango ya Jahannamu, humo mdumu. Ni maovu mno makaazi ya wafanyao kiburi!

30. Na wataambiwa walio mcha Mungu: Mola wenu Mlezi kateremsha nini? Watasema: Kheri. Walio fanya wema katika dunia hii watapata wema. Na nyumba ya Akhera ni bora zaidi, na njema mno nyumba ya wachamngu.

31. Bustani za milele wataziingia; iwe inapita kati yake mito. Humo watapata watakacho. Hivi ndivyo Mwenyezi Mungu awalipavyo wenye kumcha.

32. Wale ambao Malaika huwafisha katika hali njema, wanawaambia: Amani iwe juu yenu! Ingieni Peponi kwa sababu ya yale mliyo kuwa mkiyatenda.

33. Wanangojea jengine hawa ila Malaika wawafikie, au iwafikie amri ya Mola wako Mlezi? Kama hivyo walitenda walio kuwa kabla yao. Na Mwenyezi Mungu hakuwadhulumu, lakini walijidhulumu wenyewe.

34. Basi ukawafikia uovu wa waliyo yatenda, na waliyo kuwa wakiyakejeli yakawazunguka.

35. Na washirikina wanasema: Mwenyezi Mungu angeli taka tusingeli abudu chochote badala yake, sisi wala baba zetu, wala tusingeli harimisha chochote bila ya Yeye. Kama hivyo walifanya walio kuwa kabla yao. Basi lipo lolote juu ya Mitume isipo kuwa kubalighisha kwa uwazi?

36. Na kwa hakika kwa kila umma tuliutumia Mtume kwamba: Muabuduni Mwenyezi Mungu, na muepukeni Shetani. Basi kati yao wapo alio waongoa Mwenyezi Mungu. Na kati yao wapo ambao ulio wathibitikia upotovu. Basi tembeeni katika ardhi, muangalie ulikuwaje mwisho wa wanao kanusha.

37. Hata ukiwa na pupa ya kutaka kuwaongoa, lakini Mwenyezi Mungu hamwongoi yule anaye shikilia kupotea. Wala hawatapata wa kuwanusuru.

38. Na wanaapa kwa Mwenyezi Mungu ukomo wa viapo vyao kwamba Mwenyezi Mungu hatomfufua aliye kufa. Kwani! Ni ahadi iliyo juu yake kikweli; lakini watu wengi hawajui.

39. Ili kuwabainishia yale waliyo khitalifiana, na ili wajue walio kufuru kwamba wao walikuwa ni waongo.

40. Kauli yetu kwa kitu tunacho kitaka kiwe, ni kukiambia: Kuwa! Basi kinakuwa.

41. Na wale walio hama kwa ajili ya Mwenyezi Mungu baada ya kudhulumiwa, bila ya shaka tutawaweka duniani kwa wema; na ujira wa Akhera ni mkubwa zaidi; laiti kuwa wanajua!

42. Wale wanao subiri na wakamtegemea Mola wao Mlezi.

43. Nasi hatukuwatuma kabla yako ila watu wanaume tulio wapa Wahyi (Ufunuo). Basi waulizeni wenye ukumbusho kama nyinyi hamjui

44. Kwa Ishara wazi na Vitabu. Nasi tumekuteremshia wewe Ukumbusho ili uwabainishie watu yaliyo teremshwa kwao, wapate kufikiri.

45. Je! Wameaminisha wanao fanya vitimbi vya uovu kwamba Mwenyezi Mungu hatawadidimiza katika ardhi, na haitawafika adhabu kutoka wasipo pajua?

46. Au hatawashika katika nyendo zao, na wala hawataponyoka?

47. Au hatawashika kwa kitisho na kuwapunguza kidogo kidogo? Hakika Mola wenu Mlezi ni Mwenye huruma, Mwenye kurehemu.

48. Je! Hawavioni vitu alivyo viumba Mwenyezi Mungu - vivuli vyao vinaelekea kushotoni na kuliani, kumsujudia Mwenyezi Mungu na vikinyenyekea?

49. Na vyote viliomo katika mbingu na katika ardhi, tangu wanyama mpaka Malaika, vinamsujuidia Mwenyezi Mungu, na wala havitakabari.

50. Vinamkhofu Mola wao Mlezi aliye juu yao, na vinafanya vinavyo amrishwa.




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License