101 - 135
101.
Wadumu humo. Na ni mzigo muovu kwao kuubeba Siku ya Kiyama!
102. Siku
litakapo pulizwa barugumu, na tukawakusanya wakhalifu Siku hiyo, hali macho yao
ya kibuluu.
103.
Watanong'onezana wao kwa wao: Hamkukaa ila siku kumi tu.
104. Sisi
tunajua zaidi watakayo yasema, atakapo sema mbora wao katika mwendo: Nyinyi
hamkukaa ila siku moja tu.
105. Na wanakuuliza khabari za milima. Waambie: Mola wangu
Mlezi ataivuruga vuruga.
106. Na ataiacha tambarare, uwanda.
107. Hutaona humo mdidimio wala muinuko.
108. Siku hiyo watamfuata muitaji asiye na upotofu. Na
sauti zote zitamnyenyekea Arrahmani Mwingi wa Rahema. Basi husikii ila mchakato
na mnong'ono.
109. Siku hiyo uombezi haufai kitu, ila wa aliye mruhusu
Arrahmani Mwingi wa Rehema na akamridhia kusema.
110. Yeye anajua yaliyo mbele yao, na yaliyo nyuma yao.
Wala wao hawawezi kumjua Yeye vilivyo.
111. Na zitadhalilika nyuso mbele ya Aliye Hai Milele,
Mwangalizi Mkuu. Na atakuwa ameharibikiwa mwenye kubeba dhulma.
112. Na anaye tenda mema, naye ni Muumini, basi hatakhofu
kudhulumiwa wala kupunjwa.
113. Na namna hivi tumeiteremsha Qur'ani kwa Kiarabu, na
tumekariri humo maonyo ili wapate kuogopa na kujilinda na iwaletee makumbusho.
114. Ametukuka Mwenyezi Mungu, Mfalme wa Haki. Wala
usiifanyie haraka hii Qur'ani, kabla haujamalizika ufunuo wake. Na sema: Mola
wangu Mlezi! Nizidishie ilimu.
115. Na hapo zamani tuliagana na Adam, lakini alisahau,
wala hatukuona kwake azma kubwa.
116. Na tulipo waambia Malaika: Msujudieni Adam!
Wakasujudu, isipo kuwa Iblisi, alikataa.
117. Tukasema: Ewe Adam! Hakika huyu ni adui yako na wa
mkeo. Basi asikutoeni katika Bustani hii, mkaingia mashakani.
118. Hakika humo hutakuwa na njaa wala hutakuwa uchi.
119. Na hakika hutapata kiu humo wala hutapata joto.
120. Lakini Shet'ani alimtia wasiwasi, akamwambia: Ewe
Adam! Nikujuulishe mti wa kuishi milele na ufalme usio koma?
121. Basi wakaula wote wawili, na uchi wao ukawadhihirikia
na wakaanza kujibandika majani ya Bustani. Na Adam akamuasi Mola wake Mlezi, na
akapotea njia.
122. Kisha Mola wake Mlezi akamteuwa, naye akamkubalia toba
yake, naye akamwongoa.
123. Akasema: Ondokeni humu nyote, hali ya kuwa ni maadui
nyinyi kwa nyinyi. Na ukikufikieni uwongofu kutoka kwangu basi atakaye ufuata
uwongofu wangu, hatapotea wala hatataabika.
124. Na atakaye jiepusha na mawaidha yangu, basi kwa yakini
atapata maisha yenye dhiki, na Siku ya Kiyama tutamfufua hali ya kuwa kipofu.
125. Aseme: Ewe Mola wangu Mlezi! Mbona umenifufua kipofu,
nami nilikuwa nikiona?
126. (Mwenyezi Mungu) atasema: Ndivyo vivyo hivyo.
Zilikufikia ishara zetu, nawe ukazisahau; na kadhaalika leo unasahauliwa.
127. Na hivi ndivyo tutakavyo mlipa kila apitaye kiasi, na
asiye amini ishara za Mola wake Mlezi. Na hakika adhabu ya Akhera ni kali
zaidi, na inadumu zaidi.
128. Je! Haikuwabainikia tu; vizazi vingapi tuliviangamiza
kabla yao, nao wanatembea katika maskani zao? Hakika katika hayo zimo ishara
kwa wenye akili.
129. Na lau kuwa si neno lililo kwisha tangulia kutoka kwa
Mola wako Mlezi na muda ulio wekwa, bila ya shaka inge fika adhabu (hapa hapa).
130.
Yavumilie haya wayasemayo. Na umtakase Mola wako Mlezi kwa kumsifu kabla ya
kuchomoza jua, na kabla halijachwa, na nyakati za usiku pia umtakase, na ncha
za mchana ili upate ya kukuridhisha.
131. Wala
usivikodolee macho tulivyo wastareheshea baadhi ya watu miongoni mwao, kwa
ajili ya mapambo ya duniani, ili tuwajaribu. Na riziki ya Mola wako
Mlezi ni bora na inadumu zaidi.
132. Na waamrishe watu wako kusali, na uendelee mwenyewe
kwa hayo. Sisi hatukuombi wewe riziki, bali Sisi ndio tunakuruzuku. Na mwisho
mwema ni kwa mchamngu.
133. Na walisema: Kwa nini hakutuletea muujiza kutoka kwa
Mola wake Mlezi? Je! Haikuwafikilia dalili wazi ya yaliyomo katika Vitabu vya
kale?
134. Na lau kuwa tuliwaangamiza kwa adhabu kabla yake,
wangeli sema: Ewe Mola wetu Mlezi! Kwa nini usituletee Mtume tukazifuata ishara
zako kabla hatujadhilika na kuhizika.
135. Sema: Kila mmoja anangoja. Basi ngojeni! Hivi karibuni
mtajua nani mwenye njia sawa na nani aliye ongoka.
|