Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 23. SURATUL MUUMINUN
    • 51 - 100
Previous - Next

Click here to show the links to concordance

51 - 100

51. Enyi Mitume! Kuleni vyakula vizuri na tendeni mema. Hakika Mimi ni Mjuzi wa mnayo yatenda.

52. Na kwa yakini huu Umma wenu ni Umma mmoja, na Mimi ni Mola wenu Mlezi, basi nicheni Mimi.

53. Lakini walikatiana jambo lao mapande mbali mbali. Kila kundi likifurahia kwa waliyo nayo.

54. Basi waache katika ghafla yao kwa muda.

55. Je! Wanadhani ya kuwa kwa vile tunavyo wapa mali na watoto

56. Ndio tunawahimizia kheri? Lakini wenyewe hawatambui.

57. Kwa hakika hao ambao kwa kumwogopa Mola wao Mlezi wananyenyekea,

58. Na wale ambao Ishara za Mola wao Mlezi wanaziamini,

59. Na wale ambao Mola wao Mlezi hawamshirikishi,

60. Na wale ambao wanatoa walicho pewa, na hali nyoyo zao zinagopa kwa kuwa watarejea kwa Mola wao Mlezi,

61. Basi wote hao ndio wanao kimbilia katika mambo ya kheri, na ndio watakao tangulia kuyafikia.

62. Na hatuilazimishi nafsi ila kwa kadri ya uwezo wake. Na tunacho kitabu kisemacho kweli. Nao hawatadhulumiwa.

63. Lakini nyoyo zao zimeghafilika na hayo, na wanavyo vitendo vinginevyo wanavyo vifanya.

64. Hata tutakapo watia katika adhabu wale walio dekezwa kwa starehe kati yao, hapo ndipo watapo yayatika.

65. Msiyayatike leo! Hakika nyinyi hamtanusurika nasi.

66. Hakika zilikuwa Aya zangu mkisomewa, nanyi mkirudi nyuma juu ya visigino vyenu,

67. Na huku mkitakabari na usiku mkiizungumza (Qur'ani) kwa dharau.

68. Je, hawakuifikiri kauli, au yamewajia yasiyo wafikia baba zao wa zamani?

69. Au hawakumjua Mtume wao, ndio maana wanamkataa?

70. Au wanasema: Ana wazimu? Bali amewajia kwa Haki, na wengi wao wanaichukia Haki.

71. Na lau kuwa Haki ingeli fuata matamanio yao, basi zingeli haribika mbingu na ardhi na waliomo ndani. Bali tumewaletea ukumbusho wao, nao wanajitenga mbali na ukumbusho wao.

72. Au unawaomba ujira? Lakini ujira wa Mola wako Mlezi ni bora, na Yeye ndiye Mbora wa wanao ruzuku.

73. Na kwa yakini wewe unawaita kwenye Njia Iliyo Nyooka.

74. Na hakika wale wasio iamini Akhera wanajitenga na Njia hiyo.

75. Na lau tungeli warehemu na tukawaondolea shida waliyo nayo bila ya shaka wangeli endelea katika upotofu wao vile vile, wakitangatanga.

76. Na hakika tuliwatia adhabu kali; lakini hawakuelekea kwa Mola wao Mlezi wala hawakunyenyekea.

77. Mpaka tulipo wafungulia mlango wa adhabu kali, hapo ndipo wakawa wenye kukata tamaa.

78. Na Yeye ndiye aliye kuumbieni kusikia na kuona na nyoyo za kufahamu. Ni kuchache mno kushukuru kwenu.

79. Na Yeye ndiye aliye kuenezeni katika ardhi, na kwake Yeye mtakusanywa.

80. Na Yeye ndiye anaye huisha na kufisha, na yake Yeye mabadiliko ya usiku na mchana. Basi je! Hamfahamu?

81. Bali wanasema kama walivyo sema watu wa kwanza.

82. Walisema: Je! Tukisha kufa tukawa udongo na mifupa ndio tutafufuliwa?

83. Tuliahidiwa haya sisi na baba zetu zamani. Hayakuwa haya ila ni visa vya uwongo vya watu wa zamani.

84. Sema: Ni ya nani ardhi na viliomo ndani yake, kama nyinyi mnajua?

85. Watasema: Ni vya Mwenyezi Mungu! Sema: Basi, je, hamkumbuki?

86. Sema: Ni nani Mola Mlezi wa mbingu saba na Mola Mlezi wa A'rshi Kuu?

87. Watasema: Ni vya Mwenyezi Mungu. Sema: Basi je, hamwogopi?

88. Sema: Ni nani mkononi mwake umo Ufalme wa kila kitu, naye ndiye anaye linda, wala hakilindwi asicho taka, kama mnajua?

89. Watasema: (Ufalme huo) ni wa Mwenyezi Mungu. Sema: Basi vipi mnadanganyika?

90. Bali tumewaletea Haki, na kwa yakini hao ni waongo.

91. Mwenyezi Mungu hana mwana yeyote, wala hanaye mungu mwengine. Inge kuwa hivyo basi kila mungu angeli chukua alivyo umba, na baadhi yao wangeli washinda wengine. Mwenyezi Mungu ameepukana na sifa wanazo msifu.

92. Mjuzi wa siri na dhaahiri, na ametukuka juu ya hayo wanayo mshirikisha nayo.

93. Sema: Mola wangu Mlezi! Ukinionyesha adhabu waliyo ahidiwa,

94. Mola wangu Mlezi! Usinijaalie katika watu madhaalimu hao.

95. Na hakika Sisi ni waweza wa kukuonyeshsa tuliyo waahidi.

96. Kinga maovu kwa kutenda yaliyo mema zaidi. Sisi tunajua wayasemayo.

97. Na sema: Mola wangu Mlezi! Najikinga kwako na wasiwasi wa mashet'ani.

98. Na najikinga kwako, Mola wangu Mlezi, wasinikaribie.

99. Mpaka yanapo mfikia mmoja wao mauti, husema: Mola wangu Mlezi! Nirudishe.

100. Ili nitende mema sasa badala ya yale niliyo yaacha. Wapi! Hii ni kauli aisemayo yeye tu. Na nyuma yao kipo kizuizi mpaka siku watapo fufuliwa.




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License