51 - 64
51. Haiwi kauli ya Waumini wanapo itwa kwa Mwenyezi Mungu
na Mtume wake ili ahukumu baina yao, ila ni kusema: Tumesikia, na tumet'ii! Na
hao ndio wenye kufanikiwa.
52. Na wenye kumt'ii Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na
wakamwogopa Mwenyezi Mungu na wakamcha, basi hao ndio wenye kufuzu.
53. Na wanaapa kwa Mwenyezi Mungu ukomo wa kiapo chao ya
kwamba ukiwaamrisha kwa yakini watatoka. Sema: Msiape! Ut'iifu unajuulikana.
Hakika Mwenyezi Mungu anazo khabari za mnayo yatenda.
54. Sema: Mt'iini Mwenyezi Mungu, na mt'iini Mtume. Na
mkigeuka, basi yaliyo juu yake ni aliyo bebeshwa, na yaliyo juu yenu ni mliyo
bebshwa nyinyi. Na mkimt'ii yeye mtaongoka. Na hapana juu ya Mtume ila
kufikisha Ujumbe wazi wazi.
55. Mwenyezi Mungu amewaahidi wale walio amini miongoni
mwenu na wakatenda mema, ya kwamba atawafanya makhalifa katika ardhi kama
alivyo wafanya makhalifa wa kabla yao, na kwa yakini atawasimamishia Dini yao
aliyo wapendelea, na atawabadilishia amani baada ya khofu yao. Wawe wananiabudu Mimi, wala
wasinishirikishe na chochote. Na watao kufuru baada ya hayo, basi hao ndio
wapotovu.
56. Na
shikeni Sala, na toeni Zaka, na mt'iini Mtume, ili mpate kurehemewa.
57. Msiwadhanie
walio kufuru kwamba watashinda katika nchi. Na makaazi yao ni Motoni, na hakika
ni maovu kweli marejeo yao.
58. Enyi mlio amini! Nawakutakeni idhini iliyo wamiliki
mikono yenu ya kulia na walio bado kubaalighi miongoni mwenu mara tatu - kabla
ya Sala ya alfajiri, na wakati mnapo vua nguo zenu adhuhuri, na baada ya Sala
ya isha. Hizi ni nyakati tatu za faragha kwenu. Si vibaya kwenu wala kwao baada
ya nyakati hizi, kuzungukiana nyinyi kwa nyinyi. Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu
anavyo kuelezeni Aya zake, na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi Mwenye hikima.
59. Na watoto wanapo fikilia umri wa kubaalighi basi
nawatake ruhusa, kama walivyo taka ruhusa wa kabla yao. Hivyo ndivyo anavyo
kubainishieni Mwenyezi Mungu Aya zake, na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi Mwenye
hikima.
60. Na wanawake wazee wasio taraji kuolewa, si vibaya kwao
kupunguza nguo zao, bila ya kujishaua kwa mapambo. Na wakijihishimu ni bora
kwao. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.
61. Si vibaya kwa kipofu, wala si vibaya kwa kiguru, wala
si vibaya kwa mgonjwa, wala kwenu nyinyi, mkila katika nyumba zenu, au nyumba
za baba zenu, au nyumba za mama zenu, au nyumba za kaka zenu, au nyumba za dada
zenu, au nyumba za ami zenu, au nyumba za shangazi zenu, au nyumba za wajomba
zenu, au nyumba za dada wa mama zenu, au za mlio washikia funguo zao, au rafiki
yenu. Si vibaya kwenu mkila pamoja au mbali mbali. Na mkiingia katika nyumba,
toleaneni salamu, kuwa ni maamkio yanayo toka kwa Mwenyezi Mungu, yenye baraka
na mema. Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu anavyo kubainishieni Aya zake mpate
kuelewa.
62. Hakika Waumini wa kweli ni walio muamini Mwenyezi Mungu
na Mtume wake; na wanapo kuwa pamoja naye kwa jambo la kuwakhusu wote
hawaondoki mpaka wamtake ruhusa. Kwa hakika wale wanao kuomba ruhusa, hao ndio
wanao muamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na wakikuomba ruhusa kwa baadhi ya
kazi zao, mruhusu umtakaye miongoni mwao, uwaombee msamaha kwa Mwenyezi Mungu.
Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemmu.
63. Msifanye wito wa Mtume baina yenu kama wito wa nyinyi
kwa nyinyi. Hakika Mwenyezi Mungu anawajua miongoni mwenu wanao ondoka kwa
uficho. Basi nawatahadhari wanao khalifu amri yake, usije ukawapata msiba au
ikawapata adhabu chungu.
64. Jueni kuwa hakika ni vya Mwenyezi Mungu vilivyomo
mbinguni na ardhini. Hakika Yeye anajua mlio nayo. Na siku mtapo rudishwa kwake
atawaeleza waliyo yafanya. Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu.
|