Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 26. SURAT ASH-SHUA'RAA
    • 51 - 100
Previous - Next

Click here to show the links to concordance

51 - 100

51. Hakika sisi tunatumai Mola wetu Mlezi atatusamehe makosa yetu, kwa kuwa ndio wa kwanza wa kuamini.

52. Na tulimuamrisha Musa kwa wahyi: Nenda na waja wangu wakati wa usiku. Kwa hakika mtafuatwa.

53. Basi Firauni akawatuma mijini wapiga mbiu za mgambo.

54. (Wakieneza): Hakika hawa ni kikundi kidogo.

55. Nao wanatuudhi.

56. Na sisi ni wengi, wenye kuchukua hadhari.

57. Basi tukawatoa katika mabustani na chemchem,

58. Na makhazina, na vyeo vya hishima,

59. Kadhaalika; na tukawarithisha hayo Wana wa Israili.

60. Basi wakawafuata lilipo chomoza jua.

61. Na yalipo onana majeshi mawili haya, watu wa Musa wakasema: Hakika sisi bila ya shaka tumepatikana!

62. (Musa) akasema: Hasha! Hakika yu pamoja nami Mola wangu Mlezi. Yeye ataniongoa!

63. Tulimletea wahyi Musa tukamwambia: Piga bahari kwa fimbo yako. Basi ikatengana, na kila sehemu ikawa kama mlima mkubwa.

64. Na tukawajongeza hapo wale wengine.

65. Tukawaokoa Musa na walio kuwa pamoja naye wote.

66. Kisha tukawazamisha hao wengine.

67. Hakika bila ya shaka katika hayo ipo Ishara; lakini wengi wao si katika wenye kuamini.

68. Na kwa hakika Mola wako Mlezi ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.

69. Na wasomee khabari za Ibrahim.

70. Alipo mwambia baba yake na kaumu yake: Mnaabudu nini?

71. Wakasema: Tunaabudu masanamu, daima tunayanyenyekea.

72. Akasema: Je! Yanakusikieni mnapo yaita?

73. Au yanakufaeni, au yanakudhuruni?

74. Wakasema: Bali tumewakuta baba zetu wakifanya hivyo hivyo.

75. Je! Mmewaona hawa mnao waabudu-

76. Nyinyi na baba zenu wa zamani?

77. Kwani hakika hao ni adui zangu, isipo kuwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

78. Ambaye ndiye aliye niumba, na Yeye ndiye ananiongoa,

79. Na ambaye ndiye ananilisha na kuninywesha.

80. Na ninapo ugua ni Yeye ndiye anaye niponesha.

81. Na ambaye atanifisha, na kisha atanihuisha.

82. Na ambaye ndiye ninaye mtumai kunisamehe makosa yangu Siku ya Malipo.

83, Mola wangu Mlezi! Nitunukie hukumu na uniunganishe na watendao mema.

84. Na unijaalie nitajwe kwa wema na watu watakao kuja baadaye.

85. Na unijaalie katika warithi wa Bustani za neema.

86. Na umsamehe baba yangu, kwani hakika alikuwa miongoni mwa wapotovu.

87. Wala usinihizi Siku watapo fufuliwa.

88. Siku ambayo kwamba mali hayato faa kitu wala wana.

89. Isipo kuwa mwenye kumjia Mwenyezi Mungu na moyo safi.

90. Na Pepo itasogezwa kwa wachamngu.

91. Na Jahannamu itadhihirishwa kwa wapotovu.

92. Na wataambiwa: Wako wapi mlio kuwa mkiwaabudu

93. Badala ya Mwenyezi Mungu? Je! Wanakusaidieni, au wanajisaidia wenyewe?

94. Basi watavurumizwa humo wao na hao wakosefu,

95. Na majeshi ya Ibilisi yote.

96. Watasema, na hali ya kuwa wanazozana humo:

97. Wallahi! Kwa yakini tulikuwa katika upotovu ulio dhaahiri,

98. Tulipo kufanyeni ni sawa na Mola Mlezi wa walimwengu wote.

99. Na hawakutupoteza ila wale wakosefu.

100. Basi hatuna waombezi.




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License