1 - 50
1. T'A SIN
MIM, (T'.S.M.)
2. Hizi ni
Aya za Kitabu kinacho bainisha.
3.
Tunakusomea khabari za Musa na Firauni kwa Haki kwa ajili ya watu wanao amini.
4. Hakika
Firauni alitakabari katika nchi, na akawagawa wananchi makundi mbali mbali.
Akalidhoofisha taifa moja miongoni mwao, akiwachinja watoto wao wanaume na
akiwaacha watoto wao wanawake. Hakika yeye alikuwa katika mafisadi.
5. Na
tukataka kuwafadhili walio dhoofishwa katika nchi hiyo na kuwafanya wawe
waongozi na kuwafanya ni warithi.
6. Na
kuwapa nguvu katika nchi, na kutokana na wao kuwaonyesha kina Firauni na Hamana
na majeshi yao mambo yale waliyo kuwa wakiyaogopa.
7.
Tulimfunulia mama yake Musa kwa kumwambia: Mnyonyeshe. Na utakapo mkhofia basi mtie
mtoni, na usikhofu wala usihuzunike. Hakika Sisi tutamrudisha kwako na
tutamfanya miongoni mwa Mitume.
8. Basi wakamwokota watu wa Firauni, aje kuwa adui kwao na
huzuni. Hakika Firauni na Hamana na majeshi yao walikuwa wenye makosa.
9. Na mkewe Firauni alisema: Atakuwa kiburudisho cha macho
kwangu na kwako. Msimuuwe! Huenda akatufaa, au tumpange kuwa mwenetu. Wala wao
hawakutambua.
10. Na moyo wa mama yake Musa ukawa mtupu. Alikuwa karibu
kumdhihirisha, ingeli kuwa hatukumtia nguvu moyo wake ili awe miongoni mwa
Waumini.
11. Naye akamwambia dada yake Musa: Mfuatie. Basi naye
akawa anamuangalia kwa mbali bila ya wao kujua.
12. Na tukamjaalia awakatae wanyonyeshaji wote tangu
mwanzo, mpaka dada yake akasema: Je! Nikuonyesheni watu wa nyumba watakao mlea
kwa ajili yenu, nao pia watakuwa wema kwake?
13. Basi tukamrudisha kwa mama yake ili macho yake
yaburudike, wala asihuzunike. Na ajue ya kwamba ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya
kweli, lakini wengi wao hawajui.
14. Na Musa alipo fika utu-uzima baraabara, tulimpa akili
na ilimu. Na hivi ndivyo tunavyo walipa walio wema.
15. Na akaingia mjini wakati wa kughafilika wenyeji wake,
na akakuta humo watu wawili wanapigana - mmoja ni katika wenzake, na mwengine
katika maadui zake. Yule mwenzake alimtaka msaada kumpiga adui yake. Musa
akampiga ngumi, akamuuwa. Akasema: Hiki ni kitendo cha Shet'ani; hakika yeye ni
adui, mpotezaji dhaahiri.
16. Akasema: Mola wangu Mlezi! Hakika mimi nimejidhulumu
nafsi yangu; basi nisamehe. Akamsamehe; hakika Yeye ni Mwenye kusamehe Mwenye
kurehemu.
17. Akasema: Mola wangu Mlezi! Kwa ulivyo nineemesha, basi
mimi sitakuwa kabisa msaidizi wa wakosefu.
18. Akapambazukiwa mjini asubuhi naye ana khofu, akiangalia
huku na huku. Mara yule yule aliye mtaka msaada jana akawa anampigia kelele
amsaidie. Musa akamwambia: Hakika wewe ni mgomvi kweli kweli.
19. Basi alipo taka kumshika kwa nguvu yule aliye adui wao
wote wawili, akasema: Ewe Musa! Unataka kuniuwa kama ulivyo muuwa mtu jana?
Wewe hutaki ila kuwa jabari katika nchi, wala hutaki kuwa miongoni mwa wenye
maslaha..
20. Na akaja mtu kutoka mwisho wa mji akipiga mbio,
akasema: Ewe Musa! Wakubwa
wanashauriana kukuuwa. Basi toka! Hakika mimi ni katika wanao kupa nasaha.
21. Basi
akatoka, naye ana khofu, akiangalia huku na huku. Akasema: Mola wangu
Mlezi! Niokoe na watu madhaalimu.
22. Na alipo elekea upande wa Madyana alisema: Asaa Mola
wangu Mlezi akaniongoa njia iliyo sawa.
23. Na alipo yafikia maji ya Madyana alikuta umati wa watu
wananywesha (wanyama wao), na akakuta karibu yao wanawake wawili wanawazuia
wanyama wao. Akasema: Mna nini? Wakasema: Hatunyweshi sisi mpaka wamalize hao
wachunga. Na baba yetu ni mzee sana.
24. Basi Musa akawanyweshea; kisha akarudi kivulini, na
akasema: Mola wangu Mlezi! Hakika mimi ni mhitaji wa kheri utakayo niteremshia.
25. Basi mmoja katika wale wanawake wawili akamjia, naye
anaona haya. Akasema: Baba yangu anakwita akulipe ujira wa kutunyweshea. Basi
alipo mjia na akamsimulia visa vyake, alisema: Usiogope; umekwisha okoka kwenye
watu madhaalimu.
26. Akasema mmoja katika wale wanawake: Ewe baba yetu!
Muajiri huyu. Hakika mbora wa kumuajiri ni mwenye nguvu na muaminifu.
27. Akasema: Mimi nataka kukuoza mmojawapo katika binti
zangu hawa wawili kwa kunitumikia miaka minane. Ukitimiza kumi, khiari yako;
lakini mimi sitaki kukutaabisha. Inshallah utanikuta miongoni mwa watu wema.
28. Musa akasema: Hayo yamekwisha kuwa baina yangu na wewe.
Muda mmojapo nikiumaliza sitiwi ubayani. Na Mwenyezi Mungu ni Mlinzi juu ya haya
tunayo yasema.
29. Basi alipo timiza muda wake na akasafiri na ahali zake,
aliona moto upande wa Mlima T'uri. Akawaambia ahali zake: Ngojeni! Mimi nimeona
moto, labda nitakuleteeni kutoka huko khabari au kijinga cha moto ili mpate
kuota moto.
30. Basi alipo ufikia aliitwa kutoka ng'ambo ya bonde la
kuliani katika eneo lilio barikiwa kutoka kwenye mti: Ewe Musa! Hakika Mimi ni
Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote.
31. Na tupa chini fimbo yako. Basi alipo iona ikitikisika
kama nyoka, akarudi nyuma wala hakutazama. (Akaambiwa): Ewe Musa! Njoo mbele wala usiogope. Hakika wewe ni miongoni mwa walio
salimika.
32. Ingiza mkono wako kwenye mfuko wako, utatoka mweupe
pasipo na ubaya. Na jiambatishe mkono wako ukihisi khofu. Basi hizi ni dalili
mbili zitokazo kwa Mola wako Mlezi kumpelekea Firauni na wakuu wa umma wake.
Hakika hao walikuwa watu mafaasiki.
33. Akasema: Mola wangu Mlezi! Hakika mimi nilimuuwa mtu
katika wao, kwa hivyo naogopa wataniuwa.
34. Na ndugu yangu Harun ni fasihi zaidi ulimi wake kuliko
mimi. Basi mtume ende nami kunisaidia, ili anisadikishe. Hakika mimi nina khofu
watanikadhibisha.
35. (Mwenyezi Mungu) akasema: Tutautia nguvu mkono wako kwa
nduguyo, na tutakupeni madaraka, hata wasikufikilieni. Kwa sababu ya Ishara
zetu nyinyi na watakao kufuateni mtashinda.
36. Basi alipo wafikia Musa na Ishara zetu, walisema: Haya
si chochote ila ni uchawi ulio zuliwa. Na hatukuyasikia haya kwa baba zetu wa
zamani.
37. Na Musa akasema: Mola wangu Mlezi ni Mwenye kujua
kabisa nani anaye kuja na uwongofu unao toka kwake, na nani atakaye kuwa na
mwisho mwema wa makaazi. Hakika wenye kudhulumu hawatafanikiwa.
38. Na Firauni akasema: Enyi waheshimiwa! Sijui kama mnaye
mungu asiye kuwa mimi. Ewe Haman! Niwashie moto unichomee udongo, unijengee
mnara nipate kumchungulia mungu wa Musa. Na hakika mimi namwona yeye ni katika
waongo.
39. Na alipanda kiburi yeye na majeshi yake katika nchi
bila ya haki, na wakadhania kuwa hawatarudishwa kwetu.
40. Basi tukamshika yeye na majeshi yake, na tukawatupa
baharini. Basi hebu angalia ulikuwaje mwisho wa wenye kudhulumu?
41. Na tuliwafanya ni waongozi waitao kwenye Moto. Na Siku
ya Kiyama hawatanusuriwa.
42. Na tukawafuatishia laana katika dunia hii, na Siku ya
Kiyama watakuwa miongoni mwa wanao chusha.
43. Na hakika bila ya shaka tulimpa Musa Kitabu baada ya
kwisha ziangamiza kaumu za mwanzo, ili kiwafumbue macho watu, na kiwe uwongofu,
na rehema, ili wapate kukumbuka.
44. Wala wewe hukuwa upande wa magharibi tulipo mpa Musa
amri, wala hukuwa katika walio hudhuria.
45. Lakini Sisi tuliziumba kaumu, na ukawa mrefu umri juu
yao. Wala hukuwa mkaazi na watu wa Madyana ukiwasomea Aya zetu. Lakini ni Sisi
tulio kuwa tukiwatuma Mitume.
46. Wala hukuwa kando ya mlima tulipo nadi. Lakini ni rehema
itokayo kwa Mola wako Mlezi ili uwaonye watu wasio pata kufikiwa na mwonyaji
kabla yako, huenda wakakumbuka.
47. Na usije kuwasibu msiba kwa iliyo yatanguliza mikono
yao, wakasema: Ewe Mola wetu Mlezi! Mbona hukututumia Mtume nasi, tukafuata
Ishara zako, na tukawa miongoni mwa Waumini?
48. Ilipo wajia Haki kutoka kwetu walisema: Mbona hakupewa
kama aliyo pewa Musa? Je! Kwani wao hawakuyakataa aliyo pewa Musa zamani?
Walisema: Ni wachawi wawili wanasaidiana. Na wakasema: Hakika sisi tunawakataa
wote.
49. Sema: Basi leteni Kitabu kinacho toka kwa Mwenyezi
Mungu chenye kuongoka zaidi kuliko hivi viwili tukifuate, kama nyinyi mnasema
kweli.
50. Na ikiwa hawakuitikii, basi jua kuwa wanafuata pumbao
lao tu. Na nani aliye potea zaidi kumshinda anaye fuata pumbao lake bila ya
uwongofu utokao kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi watu wenye
kudhulumu.
|