Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 2. SURA AL- BAQARA
    • 1 - 50
Previous - Next

Click here to show the links to concordance

1 - 50

1. Alif Lam Mim.

2. Hiki ni Kitabu kisichokuwa na shaka ndani yake; ni uwongofu kwa wachamungu,

3. Ambao huyaamini ya ghaibu na hushika Sala, na hutoa katika tuliyo wapa.

4. Na ambao wanayaamini yaliyo teremshwa kwako, na yaliyo teremshwa kabla yako; na Akhera wana yakini nayo.

5. Hao wapo juu ya uwongofu utokao kwa Mola wao Mlezi, na hao ndio walio fanikiwa.

6. Hakika wale walio kufuru ni sawa kwao ukiwaonya au usiwaonye, hawaamini.

7. Mwenyezi Mungu amepiga muhuri juu ya nyoyo zao na juu ya masikio yao, na juu ya macho yao pana kifuniko. Basi watapata adhabu kubwa.

8. Na katika watu, wako wasemao: Tumemwamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho, wala wao si wenye kuamini.

9. Wanatafuta kumdanganya Mwenyezi Mungu na wale walio amini, lakini hawadanganyi ila nafsi zao; nao hawatambui.

10. Nyoyoni mwao mna maradhi, na Mwenyezi Mungu amewazidishia maradhi. Basi watakuwa na adhabu chungu kwa sababu ya kusema kwao uwongo.

11. Na wanapo ambiwa: Msifanye uharibifu ulimwenguni. Husema: Bali sisi ni watengenezaji.

12. Hakika wao ndio waharibifu, lakini hawatambui.

13. Na wanapo ambiwa: Aminini kama walivyo amini watu. Husema: Tuamini kama walivyo amini wapumbavu? Hakika wao ndio wapumbavu, lakini hawajui tu.

14. Na wanapo kutana na walio amini husema: Tumeamini. Na wanapo kuwa peke yao na mashet'ani wao husema: Hakika sisi tu pamoja nanyi. Hakika sisi tunawadhihaki tu.

15. Mwenyezi Mungu atawadhihaki wao na atawawacha katika upotofu wao wakitangatanga ovyo.

16. Hao ndio walio nunua upotofu kwa uwongofu; lakini biashara yao haikupata tija, wala hawakuwa wenye kuongoka.

17. Mfano wao ni kama mfano wa aliye koka moto, na ulipo tanda mwangaza wake kote kote Mwenyezi Mungu aliiondoa nuru yao na akawawacha katika giza, hawaoni.

18. Viziwi, mabubu, vipofu; kwa hivyo hawatarejea.

19. Au ni kama mvua kubwa itokayo mbinguni, ina giza na radi na umeme; wakawa wakitia vidole vyao masikioni mwao kwa ajili ya mingurumo, kwa kuogopa kufa. Na Mwenyezi Mungu amewazunguka makafiri.

20. Unakaribia umeme kunyakua macho yao. Kila ukiwatolea mwangaza huenda, na unapo wafanyia giza husimama. Na angelitaka Mwenyezi Mungu angeliondoa kusikia kwao na kuona kwao. Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu.

21. Enyi watu! Muabuduni Mola wenu Mlezi aliye kuumbeni nyinyi na wale wa kabla yenu, ili mpate kuokoka.

22. (Mwenyezi Mungu) ambaye amekufanyieni hii ardhi kuwa kama tandiko, na mbingu kama paa, na akateremsha maji kutoka mbinguni, na kwayo akatoa matunda yawe riziki zenu. Basi msimfanyizie Mwenyezi Mungu washirika, na hali nyinyi mnajua.

23. Na ikiwa mna shaka kwa hayo tuliyo mteremshia mja wetu basi leteni sura moja ya mfano wake, na muwaite mashahidi wenu badala ya Mwenyezi Mungu, ikiwa mnasema kweli.

24. Na mkitofanya - na wala hamtofanya kamwe - basi uogopeni moto ambao kuni zake ni watu na mawe walio andaliwa hao wanao kanusha.

25. Na wabashirie walio amini na wakatenda mema kwamba watapata mabustani yapitayo mito kati yake; kila watapo pewa matunda humo, watasema: Haya ndiyo kama tuliyo pewa mbele. Na wataletewa matunda yaliyo fanana; na humo watakuwa na wake walio takasika; na wao humo watadumu.

26. Hakika Mwenyezi Mungu haoni haya kutoa mfano hata wa mbu na ulio wa zaidi yake. Ama wale walio amini hujua ya kwamba hiyo ni haki iliyo toka kwa Mola wao Mlezi, lakini wale walio kufuru husema: Ni nini analo kusudia Mwenyezi Mungu kwa mfano huu? Kwa mfano huu huwapoteza wengi na huwaongoa wengi; lakini hawapotezi ila wale wapotovu,

27. Wanao vunja ahadi ya Mwenyezi Mungu baada ya kwisha ifunga, na wakayakata aliyo amrisha Mwenyezi Mungu kuungwa, na wakafanya uharibifu katika nchi; hao ndio wenye khasara.

28. Vipi mnamkanusha Mwenyezi Mungu na hali mlikuwa wafu akakufufueni! Kisha atakufisheni, tena atakufufueni, kisha kwake mtarejeshwa?.

29. Yeye ndiye aliye kuumbieni vyote vilivyomo katika ardhi. Tena akazielekea mbingu, na akazifanya mbingu saba. Naye ndiye Mjuzi wa kila kitu.

30. Na pale Mola wako Mlezi alipo waambia Malaika: Mimi nitamweka katika ardhi Khalifa (mfwatizi), wakasema: Utaweka humo atakaye fanya uharibifu humo na kumwaga damu, hali sisi tunakutakasa kwa sifa zako na tunakutaja kwa utakatifu wako? Akasema: Hakika Mimi nayajua msiyo yajua.

31. Na akamfundisha Adam majina ya vitu vyote, kisha akaviweka mbele ya Malaika, na akasema: Niambieni majina ya hivi ikiwa mnasema kweli.

32. Wakasema: Subhanaka, Wewe umetakasika! Hatuna ujuzi isipokuwa kwa uliyo tufunza Wewe. Hakika Wewe ndiye Mjuzi Mwenye hikima.

33. Akasema: Ewe Adam! Waambie majina yake. Basi alipo waambia majina yake alisema: Sikukwambieni kwamba Mimi ninajua siri za mbinguni na za duniani, na ninayajua mnayo yadhihirisha na mliyo kuwa mnayaficha?

34. Na tulipo waambia Malaika: Msujudieni Adam, wakamsujudia wote isipo kuwa Iblis, alikataa na akajivuna na akawa katika makafiri.

35. Na tulisema: Ewe Adam! Kaa wewe na mkeo katika Bustani, na kuleni humo maridhawa popote mpendapo, lakini msiukaribie mti huu tu; mkawa katika wale walio dhulumu.

36. Lakini Shet'ani aliwatelezesha hao wawili na akawatoa katika waliyo kuwamo, na tukasema: Shukeni, nanyi ni maadui nyinyi kwa nyinyi. Katika ardhi yatakuwa makaazi yenu na starehe kwa muda.

37. Kisha Adam akapokea maneno kwa Mola wake Mlezi, na Mola wake Mlezi alimkubalia toba yake; hakika Yeye ndiye Mwingi wa kukubali toba na Mwenye kurehemu.

38. Tukasema: Shukeni nyote; na kama ukikufikieni uwongofu utokao kwangu, basi watakao fuata uwongofu wangu huo haitakuwa khofu juu yao wala hawatahuzunika.

39. Na wenye kukufuru na kuzikanusha ishara zetu, hao ndio watakao kuwa watu wa Motoni, humo watadumu.

40. Enyi Wana wa Israili! Kumbukeni neema yangu niliyo kuneemesheni, na timizeni ahadi yangu, na Mimi nitatimiza ahadi yenu, na niogopeni Mimi tu.

41. Na aminini niliyo yateremsha ambayo yanasadikisha mliyo nayo, wala msiwe wa kwanza kuyakataa. Wala msiuze Ishara zangu kwa thamani ndogo. Na niogopeni Mimi tu.

42. Wala msichanganye kweli na uwongo na mkaificha kweli nanyi mnajua.

43. Na shikeni Sala, na toeni Zaka, na inameni pamoja na wanao inama.

44. Je! Mnawaamrisha watu mema na mnajisahau nafsi zenu, na hali nyinyi mnasoma Kitabu? Basi je, hamzingatii?

45. Na tafuteni msaada kwa kusubiri na kwa kusali; na kwa hakika jambo hilo ni gumu isipokuwa kwa wanyenyekevu,

46. Ambao wana yakini kuwa hakika watakutana na Mola wao Mlezi na ya kuwa hakika watarejea kwake.

47. Enyi Wana wa Israili! Kumbukeni zile neema zangu nilizo kuneemesheni, na nikakuteuweni kuliko wote wengineo.

48. Na iogopeni Siku ambayo mtu hatomfaa mtu kwa lolote, wala hayatakubaliwa kwake maombezi, wala hakitapokewa kikomboleo kwake; wala hawatanusuriwa.

49. Na vile tulipo kuokoeni kwa watu wa Firauni walio kupeni adhabu mbaya, wakiwachinja wana wenu wa kiume na wakawawacha hai wanawake; na katika hayo ulikuwa ni mtihani mkubwa ulio toka kwa Mola wenu Mlezi.

50. Na tulipo ipasua bahari kwa ajili yenu na tukakuokoeni, tukawazamisha watu wa Firauni, na huku mnatazama.




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License