Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 33. SURAT AL-AH'ZAB
Previous - Next

Click here to show the links to concordance

33. SURAT AL-AH'ZAB

(Imeteremka Madina)

Sura hii imeanza kwa kumtaka Mtume wa Mwenyezi Mungu s.a.w. amche Mwenyezi Mungu na amtegemee Yeye. Tena ikaingia kuzungumza juu ya mas-ala ya watoto wa kupanga, na ikakataa kuwa hao wana wanao walea kuwa ni watoto wao khasa. Na ikataja mapenzi na ut'iifu wa Mwenyezi Mungu alio wajibisha kwa ajili ya Mtume wake, na hishima na kuwatukuza Mamama wa Waumini, yaani wake za Mtume. Na Sura imeeleza ahadi aliyo ichukua Mwenyezi Mungu kwa Manabii kuwa wafikishe ujumbe; na ikafafanua khabari za Vita vya Ah'zab (Makundi) na khofu na misukosuko iliyo kuwako, na vipi mwishoe Waumini wakashinda na ahadi ya Mwenyezi Mungu ikatimia. Na Sura hii ikashughulikia kutaja adabu ambazo zinawapasa wake za Mtume kuzifuata, na wajilazimishe nafsi zao kuzishika. Tena ikaangukia kuzungumza juu ya watoto wa kupanga, na ikavunja ada ya siku za kijahiliya, za ujinga, ilipo kuwa kuharimisha mtu kuoana na mwana wa kupanga ambaye kwa hakika ni halali yake. Na Sura ikamsifu Mtume s.a.w. na ikamthibitishia aliyo kuwa anastahiki. Na ikausia kustareheshwa na kumwacha kwa wema mwanamke anaye pewa talaka kabla ya kuingia harusi. Na ikamkhusisha Mtume s.a.w. kuwa imemhalalishia mwanamke aliye jitolea kuolewa naye, na ikasema wazi kuwa si halali kwake kuzidisha kuowa wanawake wengine baada ya hao tisa alio kuwa nao. Kisha Sura tukufu ikabainisha yanayo wajibikia Waumini kuyafuata wanapo ingia nyumba za Nabii kwa ajili ya kula, na kuwa wakisha wende zao, na juu ya kuwauliza wake zake nyuma ya pazia. Na Sura ikawataka Mamama wa Waumini (wake za Mtume s.a.w.) wateremshe mitandio yao juu ya vifua vyao. Na Sura ikazungumza juu ya Saa na vitisho vya Kiyama, na ikatoa nasaha ya kumcha Mwenyezi Mungu, na kusema maneno yaliyo sawa, na ikakhitimishia kwa kutaja jukumu la Mwenyezi Mungu alilo libeba mwanaadamu, hali mbingu na ardhi na milima ilishindwa kulibeba.
Kutokana na hayo inaonekana kuwa makusudio muhimu kabisa ya Sura hii ni: Maneno juu ya watoto wa kupanga, na kuivunja ada iliyo kuwa imeenea wakati ule kuharimisha kuwaoa wana wa kupanga ambao ni halali kwao; na ihsani ya Mwenyezi Mungu kuwafanyia Waumini kwa ushindi kuwashinda washirikina kama alivyo waahidi; na kufafanua sharia aliyo wawekea Mwenyezi Mungu Waumini wanapo ingia nyumba za Nabii s.a.w. na kuwaharimishia kuwaoa wake zake baada yake, na kuzipanga adabu makhsusi zilizo wakhusu Mamama wa Waumini, yaani wake za Mtume s.a.w.

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License