51 - 73
51. Unaweza kuakhirisha zamu kwa umtakaye katika wao, na
umsogeze umtakaye. Na kama ukimtaka yule uliye mtenga, basi si vibaya kwako.
Kufanya hivi kutapelekea yaburudike macho yao, wala wasihuzunike, na wawe radhi
juu ya kile unacho wapa wao wote. Na Mwenyezi Mungu anajua yaliyomo nyoyoni
mwenu, na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua, Mwenye hikima.
52. Baada ya hawa hawakuhalalikii wewe wanawake wengine,
wala kuwabadilisha kwa wake wengine ingawa uzuri wao ukikupendeza; isipo kuwa
yule uliye mmiliki kwa mkono wako wa kulia. Na Mwenyezi Mungu anachungua kila
kitu.
53. Enyi mlio amini! Msiingie nyumba za Nabii ila mpewe
ruhusa kwenda kula, sio kungojea kiwive. Lakini mtakapo itwa basi ingieni, na
mkisha kula tawanyikeni, wala msiweke mazungumzo. Hakika hayo yanamuudhi Nabii
naye anakustahini, lakini Mwenyezi Mungu hastahi kwa jambo la haki. Na mnapo
wauliza wakeze haja waulizeni nyuma ya mapazia. Hivyo ndio usafi zaidi kwa
nyoyo zenu na nyoyo zao. Wala haikufalieni kumuudhi Mtume wa Mwenyezi Mungu,
wala kuwaoa wake zake baada yake kabisa. Hakika jambo hilo ni kubwa mbele ya
Mwenyezi Mungu.
54. Mkidhihirisha chochote kile, au mkikificha, basi hakika
Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua kila kitu.
55. Hapana ubaya kwao (wake za Mtume) kuonana na baba zao,
wala watoto wao, wala ndugu zao, wala watoto wa ndugu zao wanaume, wala watoto
wa ndugu zao wanawake, wala wanawake wenzao, wala wale iliyo wamiliki mikono
yao ya kulia. Na enyi wanawake, mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni
Mwenye kushuhudia kila kitu.
56. Hakika Mwenyezi Mungu na Malaika wake wanamsalia Nabii.
Enyi mlio amini! Msalieni na mumsalimu kwa salamu.
57. Hakika wanao muudhi Mwenyezi Mungu na Mtume wake,
Mwenyezi Mungu amewalaani duniani na Akhera, na amewaandalia adhabu ya
kufedhehi.
58. Na wale wanao waudhi Waumini wanaume na wanawake pasina
wao kufanya kosa lolote, bila ya shaka wamebeba dhulma kubwa na dhambi zilio
dhaahiri.
59. Ewe
Nabii! Waambie wake zako, na binti zako, na wake za Waumini wajiteremshie nguo
zao. Hivyo ni karibu zaidi kuweza kutambulikana wasiudhiwe. Na Mwenyezi Mungu
ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.
60. Kama
wanaafiki na wale wenye maradhi nyoyoni mwao, na waenezao fitna katika Madina
hawatoacha, basi kwa yakini tutakusalitisha juu yao, kisha hawatakaa humo
karibu yako ila muda mchache tu.
61.
Wamelaanika! Popote watakapo onekana watakamatwa na watauliwa kabisa.
62. Hii ni
ada ya Mwenyezi Mungu iliyo kuwa kwa wale walio pita zamani. Wala hutapata
mabadiliko katika ada ya Mwenyezi Mungu.
63. Watu
wanakuuliza khabari ya Saa (ya Kiyama). Sema: Ujuzi wake uko kwa Mwenyezi
Mungu. Na nini kitakujuvya? Pengine hiyo Saa iko karibu.
64. Hakika
Mwenyezi Mungu amewalaani makafiri na amewaandalia Moto unao waka kwa nguvu.
65.
Watadumu humo milele. Hawampati mlinzi wala wa kuwanusuru.
66. Siku
ambayo nyuso zao zitapinduliwa pinduliwa katika Moto. Watasema: Laiti tungeli
mt'ii Mwenyezi Mungu, na tungeli mt'ii Mtume!
67. Na watasema: Mola wetu Mlezi! Hakika sisi tuliwat'ii
bwana zetu na wakubwa wetu; nao ndio walio tupoteza njia.
68. Mola wetu Mlezi! Wape wao adhabu mara mbili, na
uwalaani laana kubwa.
69. Enyi mlio amini! Msiwe kama wale walio mtaabisha Musa,
lakini Mwenyezi Mungu akamtakasa na waliyo yasema, naye alikuwa mwenye hishima
mbele ya Mwenyezi Mungu.
70. Enyi mlio amini! Mcheni Mwenyezi Mungu na semeni maneno
ya sawasawa.
71. Apate kukutengenezeeni vitendo vyenu na akusameheni
madhambi yenu. Na anaye mt'ii Mwenyezi Mungu na Mtume wake, bila ya shaka
amefanikiwa mafanikio makubwa.
72. Kwa hakika Sisi tulikadimisha amana kwa mbingu na ardhi
na milima; na vyote hivyo vikakataa kuichukua na vikaogopa. Lakini mwanaadamu
akaichukua. Hakika yeye amekuwa dhaalimu mjinga.
73. Kwa hivyo Mwenyezi Mungu anawaadhibu wanaafiki wanaume,
na wanaafiki wanawake, na washirikina wanaume, na washirikina wanawake; na
anawapokelea toba Waumini wanaume, na Waumini wanawake. Na Mwenyezi Mungu ni
Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.
|