Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 36. SURAT YA-SIN
    • 51 - 83
Previous - Next

Click here to show the links to concordance

51 - 83

51. Na litapulizwa barugumu, mara watatoka makaburini wakikimbilia kwa Mola wao Mlezi.

52. Watasema: Ole wetu! Nani aliye tufufua kwenye malazi yetu? Haya ndiyo aliyo yaahidi Mwingi wa Rehema na wakasema kweli Mitume.

53. Haitakuwa ila ukelele mmoja tu, mara wote watahudhuruishwa mbele yetu.

54. Basi leo nafsi yoyote haitadhulumiwa kitu, wala hamtalipwa ila yale mliyo kuwa mkiyatenda.

55. Hakika watu wa Peponi leo wamo shughulini, wamefurahi.

56. Wao na wake zao wamo katika vivuli wameegemea juu ya viti vya fakhari.

57. Watapata humo kila namna ya matunda na watapata kila watakacho kitaka.

58. "Salama!" Hiyo ndiyo kauli itokayo kwa Mola Mlezi Mwenye kurehemu.

59. Na enyi wakosefu! Jitengeni leo!

60. Je! Sikuagana nanyi, enyi wanaadamu, kuwa msimuabudu Shet'ani? Hakika yeye ni adui dhaahiri kwenu.

61. Na ya kwamba mniabudu Mimi? Hii ndiyo Njia Iliyo Nyooka.

62. Na bila ya shaka yeye amekwisha lipoteza kundi kubwa miongoni mwenu. Je, hamkuwa mkifikiri?

63. Hii basi ndiyo Jahannamu mliyo kuwa mkiahidiwa.

64. Ingieni leo kwa vile mlivyo kuwa mkikufuru.

65. Leo tunaviziba vinywa vyao, na iseme nasi mikono yao, na itoe ushahidi miguu yao kwa waliyo kuwa wakiyachuma.

66. Na tungeli penda tungeli yafutilia mbali macho yao, wakawa wanaiwania njia. Lakini wange ionaje?

67. Na tungeli taka tunge wageuza sura hapo hapo walipo, basi wasinge weza kwenda wala kurudi.

68. Na tunaye mzeesha tunamrudisha nyuma katika umbo. Basi je! hawazingatii?

69. Wala hatukumfundisha (Muhammad) mashairi, wala hayatakikani kwake hayo. Haukuwa huu ila ni ukumbusho na Qur'ani inayo bainisha.

70. Ili imwonye aliye hai, na neno litimie juu ya makafiri.

71. Je! Hawaoni kwamba tumewaumbia kutokana na iliyo fanya mikono yetu wanyama wa mifugo, na wao wakawa wenye kuwamiliki.

72. Na Sisi tukawadhalilishia. Basi baadhi yao wako wanao wapanda, na baadhi yao wanawala.

73. Na wao wanapata kwao manufaa na vinywaji. Basi je, hawashukuru?

74. Na wameishika miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu ili ati wapate kusaidiwa!

75. Hawataweza kuwasaidia. Bali hao ndio watakuwa askari wao watakao hudhurishwa.

76. Basi maneno yao yasikuhuzunishe. Hakika Sisi tunayajua wanayo yaweka siri na wanayo yatangaza.

77. Kwani mwanaadamu haoni ya kwamba Sisi tumemuumba yeye kutokana na tone la manii? Kisha sasa yeye ndio amekuwa ndiye mgomvi wa dhaahiri!

78. Na akatupigia mfano, na akasahau kuumbwa kwake, akasema: Ni nani huyo atakaye ihuisha mifupa nayo imekwisha mung'unyika?

79. Sema: Ataihuisha huyo huyo aliye iumba hapo mara ya mwanzo. Na Yeye ni Mjuzi wa kila kuumba.

80. Aliye kujaalieni kupata moto kutokana na mti wa kijani nanyi mkawa kwa huo mnawasha.

81. Kwani aliye ziumba mbingu na ardhi hawezi kuwaumba mfano wao? Kwani! Naye ndiye Muumbaji Mkuu, Mjuzi.

82. Hakika amri yake anapo taka kitu ni kukiambia tu: Kuwa! Na kikawa.

83. Basi Ametakasika yule ambaye mkononi mwake umo Ufalme wa kila kitu; na kwake Yeye mtarejeshwa.

 




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License