Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 38. SURAT S'AAD
    • 51 - 88
Previous - Next

Click here to show the links to concordance

51 - 88

51. Humo wataegemea matakia, wawe wanaagiza humo matunda mengi na vinywaji.

52. Na pamoja nao wake zao wenye kutuliza macho, hirimu zao.

53. Haya ndiyo mliyo ahidiwa kwa Siku ya Hisabu.

54. Hakika hii ndiyo riziki yetu isiyo malizika.

55. Ndio hivi! Na hakika wenye kuasi bila ya shaka watapata marudio maovu kabisa;

56. Nayo ni Jahannamu! Wataingia humo. Nacho hicho ni kitanda kiovu mno cha kulalia.

57. Ndio hivi! Basi na wayaonje maji ya moto na ya usaha!

58. Na adhabu nyenginezo za namna hii.

59. Hili ndilo kundi litakalo ingia pamoja nanyi. Hapana makaribisho mema kwao. Hakika hao wanaingia Motoni.

60. Waseme: Lakini nyinyi! Hamna mapokezi mazuri! Nyinyi ndio mlio tusabibisha haya, napo ni pahala paovu kabisa!

61. Waseme: Mola wetu Mlezi! Aliye tusabibisha haya mzidishie adhabu mara mbili Motoni.

62. Watasema: Tuna nini hata hatuwaoni wale watu ambao tukiwahisabu ndio katika waovu?

63. Tulikosea tulipo wafanyia maskhara, au macho yetu tu hayawaoni ?

64. Hakika hayo bila ya shaka ndiyo makhasimiano ya watu wa Motoni.

65. Sema: Hakika mimi ni mwonyaji tu; na hapana mungu ila Mwenyezi Mungu Mmoja, Mtenda nguvu,

66. Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na viliomo baina yake, Mwenye nguvu, Mwenye kusamehe.

67. Sema: Hii ni khabari kubwa kabisa.

68. Ambayo nyinyi mnaipuuza.

69. Sikuwa na ilimu ya mambo ya viumbe wakuu watukufu walipo kuwa wakishindana.

70. Haikufunuliwa kwangu isipo kuwa ya kwamba hakika mimi ni mwonyaji dhaahiri.

71. Mola wako Mlezi alipo waambia Malaika: Hakika Mimi nitaumba mtu kutokana na udongo.

72. Na nitakapo mkamilisha na kumpulizia roho inayo tokana nami, basi muangukieni kwa kumt'ii.

73. Basi Malaika wakat'ii wote pamoja.

74. Isipo kuwa Iblisi; alijivuna na akawa katika makafiri.

75. Mwenyezi Mungu akamwambia: Ewe Iblisi! Kipi kilicho kuzuia kumt'ii yule niliye muumba kwa mikono yangu? Je! Umejiona mkubwa, au umekuwa katika wakuu kweli?

76. Akasema: Mimi ni bora kuliko yeye. Umeniumba kwa moto, na yeye umemuumba kwa udongo.

77. Akasema: Basi toka humo, kwani hakika wewe umelaanika.

78. Na hakika laana yangu itakuwa juu yako mpaka Siku ya Malipo.

79. Akasema: Mola wangu Mlezi! Nipe muhula mpaka siku watayo fufuliwa viumbe.

80. Mwenyezi Mungu akasema: Basi umekwisha kuwa miongoni mwa walio pewa muhula,

81. Mpaka siku ya wakati maalumu.

82. Akasema (Iblisi): Naapa kwa utukufu wako, bila ya shaka nitawapoteza wote,

83. Isipo kuwa wale waja wako miongoni mwao walio khitariwa.

84. Akasema: Haki! Na haki ninaisema.

85. Bila ya shaka nitaijaza Jahannamu kwa wewe na kwa hao wote wenye kukufuata miongoni mwao.

86. Sema (Ewe Mtume) : Sikuombeni ujira juu ya haya, wala mimi si katika wadanganyifu.

87. Hayakuwa haya ila ni mawaidha kwa walimwengu wote.

88. Na bila ya shaka mtajua khabari zake baada ya muda.

 




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License