39. SURAT AZZUMAR
(Imeteremka
Makka)
Sura hii ni ya Makka,
yasemekana, isipo kuwa Aya 52, 53 na 54. Na Aya zake ni 75. Imefunguliwa Sura hii kwa kuisifu Qur'ani, kisha kwa
kuwataka watu wamsafie ibada Mwenyezi Mungu peke yake, na inawarudi wale wanao
sema kwamba Mwenyezi ana mwana. Kisha Aya zikaeleza uwezo wa Mwenyezi Mungu
Mtukufu katika kuumba mbingu na ardhi, na kumuumba mtu; na kwamba watu
wakimkanya Yeye basi Yeye si mwenye kuwahitajia wao, na kwamba wakimshukuru,
Yeye huwa radhi nao, na wala hawaridhii wakimkanusha. Na kadhaalika Sura hii
imeeleza khulka ya binaadamu katika hali mbili, yaani anapo patwa na shida
humwomba Mola wake na akarejea kwake, na akimneemesha mara husahau yale aliyo
kuwa akiyaomba kabla yake.
Kisha Sura ikaunganisha makhusiano baina ya anaye tahadhari na Akhera na
akataraji rehema ya Mola wake Mlezi, na wale wanao muasi; na malipo aliyo
waandalia hawa na wale kwa Siku ya Kiyama. Kisha inawakumbusha neema za
Mwenyezi Mungu kwa kuwateremshia maji, na kwamba Yeye huihuisha ardhi baada ya
kufa kwake, na huotesha mimea ambayo inapitia viwango mbali mbali. Na katika
hayo yapo makumbusho kwa wenye akili.
Kisha Sura inarejea kusimulia khabari ya Qur'ani na athari zake kwa wanao
mwogopa Mola wao Mlezi. Na kwamba Mwenyezi Mungu kawapigia mifano ndani yake
ili wazingatie, hiyo ni Qur'ani isio na pogo ili wamchemungu. Kisha Sura
ikalinganisha baina ya mja mshirikina na mja mwenye kumtakasisha Mwenyezi Mungu
kwa ibada, na kuwa hakika hawa wawili hawawi sawa. Na kuwa hakika mauti ndio
mwisho wa wote, na baadae mbele ya Mola wao Mlezi ndio watazozana.
Kisha Sura ikabainisha mwisho wa mwenye kumzulia uwongo Mwenyezi Mungu na
akaikadhibisha kweli, na mwisho wa wasemao kauli ya kweli, wenye kusadiki
waliyo teremshiwa. Na hakika hao washirikina ukiwauliza: Nani aliye umba mbingu
na ardhi? Hapana shaka watasema: Mwenyezi Mungu. Lakini nao juu ya hayo
wanawaabudu wasio walinda na madhara pindi Mwenyezi Mungu akitaka kuwadhuru,
wala hawaizuii rehema ya Mwenyezi Mungu pindi akiwatakia rehema. Tena Sura hii
inathibitisha kwamba Kitabu hichi kimeteremshwa kwa haki. Basi mwenye kuongoka
ni kwa maslaha ya nafsi yake, na mwenye kupotea dhambi zake ni juu ya nafsi
yake. Na hakika Mtume s.a.w. si mwakilishi juu yao.
Kisha Sura inarejea kuwakumbusha kufa na kufufuliwa, na kwamba wale miungu ya
kishirikina (ya kipagani) walio wafuata badala ya Mwenyezi Mungu hawawafai
kitu, hata kuwaombea. Kwani hakika uombezi wote uko kwa Mwenyezi Mungu.
Na yalipo kithiri maneno juu ya adhabu chungu walio andaliwa waasi na
waharibifu - na labda haya ndiyo yaliyo zipelekea nyoyo zao kukata tamaa na
rehema ya Mwenyezi Mungu - amewafungulia mlango wa kutumai rehema yake kwa
kusema: "Sema: Enyi waja wangu walio jidhulumu nafsi zao! Msikate tamaa na
rehema ya Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu husamehe dhambi zote. Hakika
Yeye ni Msamehevu Mwenye kurehemu." Na akawataka warejee kwake kabla
haijawajia adhabu kwa ghafla na wao hawatambui: "Na Siku ya Kiyama
utawaona wale walio msingizia uwongo Mwenyezi Mungu nyuso zao zimesawijika. Je!
Si katika Jahannamu makaazi ya wale wanao takabari?" Na wenye kuchamngu
halitawagusa ovu, na wala hawatahuzunika. Na Sura ikakhitimisha kwa kusimulia
khabari za Siku ya Mwisho, tangu mwanzo wake litapo pulizwa barugumu wakapigwa bumbuazi
walioko mbinguni na kwenye ardhi isipo kuwa wale ambao Mwenyezi Mungu
amewatakia. Mpaka pale kila mwenye haki akaitwaa haki yake. Tena wakasukumwa
watu wa Motoni wende Motoni, na watu wa Peponi wakapelekwa huko. Nao hao
waseme: Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu aliye timiza ahadi yake, na
akawahukumia wote kwa haki, na ikasemwa: Alhamdulilahi Rabbi'la'alamiin. Sifa
njema zote ni za Mola Mlezi wa viumbe vyote.
KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
|