Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Qu'rani

IntraText CT - Text

  • 43. SURAT AZZUKHRUF
    • 51 - 89
Previous - Next

Click here to show the links to concordance

51 - 89

51. Na Firauni alitangaza kwa watu wake, akisema: Enyi watu wangu! Kwani mimi sinao huu ufalme wa Misri, na hii mito inapita chini yangu? Je! Hamwoni?

52. Au mimi si bora kuliko huyu aliye mnyonge, wala hawezi kusema waziwazi?

53. Basi mbona hakuvikwa vikuku vya dhahabu, au hawakuja Malaika pamoja naye wakamwandama?

54. Basi aliwachezea watu wake, na wakamt'ii. Kwa hakika hao walikuwa watu wapotovu.

55. Walipo tukasirisha tuliwapatiliza tukawazamisha wote!

56. Kisha tukawafanya kuwa watangulizi na mfano kwa wa baadaye.

57. Na alipo pigiwa mfano Mwana wa Mariamu, watu wako waliupiga ukelele.

58. Wakasema: Miungu yetu kwani si bora kuliko huyu? Hawakukupigia mfano huo ila kwa ubishi tu. Bali hao ni watu wagomvi!

59. Hakuwa yeye (Isa) ila ni Mtumwa tuliye mneemesha na tukamfanya ni mfano kwa Wana wa Israili.

60. Na tungeli penda tungeli wafanyia miongoni mwenu Malaika katika ardhi wakifuatana.

61. Na kwa hakika yeye ni alama ya Saa ya Kiyama. Basi usiitilie shaka, na nifuateni. Hii ndiyo Njia Iliyo Nyooka.

62. Wala asikuzuilieni Shet'ani. Hakika yeye ni adui yenu wa dhaahiri.

63. Na alipo kuja Isa na dalili zilizo wazi, alisema: Nimekujieni na hikima, na ili nikuelezeni baadhi ya yale mliyo khitalifiana. Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na mnit'ii mimi.

64. Kwa hakika Mwenyezi Mungu ni Mola wangu Mlezi, na ni Mola wenu Mlezi. Basi Muabuduni Yeye tu. Hii ndiyo Njia Iliyo Nyooka.

65. Lakini makundi kwa makundi yao yalikhitalifiana wao kwa wao. Ole wao walio dhulumu kwa adhabu ya siku chungu.

66. Je! Nini wanangojea ila Saa iwajie kwa ghafla na wala wao hawatambui?

67. Siku hiyo marafiki watakuwa ni maadui, wao kwa wao, isipo kuwa wachamngu.

68. Enyi waja wangu! Hamtakuwa na khofu siku hiyo, wala hamtahuzunika.

69. Ambao waliziamini Ishara zangu na walikuwa Waislamu.

70. Ingieni Peponi, nyinyi na wake zenu; mtafurahishwa humo.

71. Watakuwa wanapitishiwa sahani za dhahabu na vikombe; na vitakuwamo ambavyo nafsi zinavipenda na macho yanavifurahia, na nyinyi mtakaa humo milele.

72. Na hiyo ni Pepo mliyo rithishwa kwa hayo mliyo kuwa mkiyafanya.

73. Mnayo humo matunda mengi mtakayo yala.

74. Kwa hakika wakosefu watakaa katika adhabu ya Jahannamu.

75. Hawatapumzishwa nayo na humo watakata tamaa.

76. Wala Sisi hatukuwadhulumu, bali wao ndio walio kuwa madhaalimu.

77. Nao watapiga kelele waseme: Ewe Malik! Na atufishe Mola wako Mlezi! Naye aseme: Hakika nyinyi mtakaa humo humo!

78. Kwa yakini tulikuleteeni Haki, lakini wengi katika nyinyi mlikuwa mnaichukia Haki.

79. Au waliweza kupitisha amri yao? Bali ni Sisi ndio tunao pitisha.

80. Au wanadhani kwamba hatusikii siri zao na minong'ono yao? Wapi! Na wajumbe wetu wapo karibu nao, wanayaandika.

81. Sema: Ingeli kuwa Rahmani ana mwana, basi mimi ningeli kuwa wa kwanza kumuabudu.

82. Ametakasika Mola Mlezi wa mbingu na ardhi, Mola Mlezi wa A'rshi, na hayo wanayo msifia.

83. Basi waache wapige porojo wakicheza mpaka wakutwe na hiyo siku yao waliyo ahidiwa.

84. Na Yeye ndiye Mungu mbinguni, na ndiye Mungu katika ardhi. Naye ndiye Mwenye hikima, Mwenye ujuzi.

85. Na ametukuka Mwenye ufalme wa mbingu na ardhi na viliomo ndani yake. Na uko kwake ujuzi wa Saa ya Kiyama, na kwake Yeye mtarudishwa.

86. Wala hao mnao waomba badala yake Yeye hawana uweza wa kumwombea mtu, isipo kuwa anaye shuhudia kwa haki, na wao wanajua.

87. Na ukiwauliza ni nani aliye waumba? Bila ya shaka watasema: Mwenyezi Mungu! Basi ni wapi wanako geuziwa?

88. Na usemi wake (Mtume) ni: Ewe Mola wangu Mlezi! Hakika hawa ni watu wasio amini.

89. Basi wasamehe, na uwambie maneno ya salama. Watakuja jua.

 




Previous - Next

Table of Contents | Words: Alphabetical - Frequency - Inverse - Length - Statistics | Help | IntraText Library

Best viewed with any browser at 800x600 or 768x1024 on Tablet PC
IntraText® (V89) - Some rights reserved by EuloTech SRL - 1996-2007. Content in this page is licensed under a Creative Commons License