51 - 100
51. Na tulipo muahidi Musa masiku arubaini, kisha mkachukua
ndama (mkamuabudu) baada yake, na mkawa wenye kudhulumu.
52. Kisha tukakusameheni baada ya hayo, ili mpate
kushukuru.
53. Na tulipo mpa Musa Kitabu na pambanuo ili mpate
kuongoka.
54. Na Musa alipo waambia watu wake: Enyi watu wangu!
Hakika nyinyi mmezidhulumu nafsi zenu kwa kuchukua kwenu ndama (kumuabudu).
Basi tubuni kwa Muumba wenu na ziueni nafsi zenu. Haya ni bora kwenu mbele ya
Muumba wenu. Naye akapokea toba yenu. Hakika Yeye ndiye apokeaye toba na Mwenye
kurehemu.
55. Na mlipo sema: Ewe Musa! Hatutakuamini mpaka tumwone
Mwenyezi Mungu waziwazi. Ikakunyakueni radi nanyi mnaangalia.
56. Kisha tukakufufueni baada ya kufa kwenu, ili mpate
kushukuru.
57. Na tukakutilieni kivuli kwa mawingu na
tukakuteremshieni Manna na Salwa; tukakwambieni: Kuleni vitu vizuri hivi
tulivyo kuruzukuni. Nao hawakutudhulumu Sisi lakini walikuwa wanajidhulumu
nafsi zao.
58. Na tulipo sema: Ingieni mji huu, na humo mle mpendapo
maridhawa, na ingieni katika mlango wake kwa unyenyekevu, na semeni: Tusamehe!
Tutakusameheni makosa yenu, na tutawazidishia wema wafanyao wema.
59.Lakini walio dhulumu waliibadili kauli isiyo kuwa waliyo
ambiwa. Kwa hivyo tukaiteremsha juu ya wale walio dhulumu adhabu kutoka mbinguni
kwa sababu ya walivyo kuwa wamepotoka.
60. Na Musa alipo omba maji kwa ajili ya watu wake,
tulimwambia: Lipige jiwe kwa fimbo yako. Mara zikatimbuka chemchem kumi na
mbili; kila kabila ikajua mahali pake pa kunywea. Tukawaambia: Kuleni na mnywe
riziki ya Mwenyezi Mungu, wala msiasi katika nchi mkafanya uharibifu.
61. Na mlipo sema: Ewe Musa! Hatuwezi kuvumilia chakula cha
namna moja tu, basi tuombee kwa Mola wako Mlezi atutolee vile vinavyo mea
katika ardhi, kama mboga zake, na matango yake, na thom zake, na adesi zake, na
vitunguu vyake. Akasema: Mnabadili kilicho duni kwa kilicho bora? Shukeni
mjini, huko mtapata mlivyo viomba. Na wakapigwa na unyonge,na umasikini, na
wakastahili ghadhabu ya Mwenyezi Mungu. Na haya ni kwa sababu walikuwa
wakiyakataa maneno ya Mwenyezi Mungu, na wakiwauwa Manabii pasipo haki. Hayo ni
kwa walivyo asi na wakapindukia mipaka.
62. Hakika Walio amini, na Mayahudi na Wakristo, na
Wasabai; yeyote atakaye muamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho na akatenda
mema basi watapata malipwa yao kwa Mola wao Mlezi, wala haitakuwa khofu juu
yao, wala hawatahuzunika.
63. Na tulipo chukua ahadi yenu, na tukaunyanyua mlima juu
yenu (tukakwambieni): Shikeni kwa nguvu haya tuliyo kupeni, na yakumbukeni
yaliyomo ndani yake ili mpate kujilinda.
64. Kisha mligeuka baada ya haya. Na lau kuwa si fadhila za
Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema zake, mngeli kuwa miongoni mwa wenye
kukhasirika.
65. Na hakika mlikwisha yajua ya wale miongoni mwenu walio
ivunja Sabato,(siku ya mapumziko, Jumaa Mosi) na tukawaambia: Kuweni manyani
wadhalilifu.
66. Kwa hivyo tukayafanya hayo kuwa onyo kwa wale walio
kuwa katika zama zao na walio kuja baada yao, na mawaidha kwa wachamngu.
67. Na Musa alipo waambia watu wake: Hakika Mwenyezi Mungu
anakuamrisheni mchinje ng'ombe. Wakasema: Je! Unatufanyia mzaha? Akasema:
Audhubil lahi! Najikinga kwa Mwenyezi Mungu nisiwe miongoni mwa wajinga.
68. Wakasema: Tuombee kwa Mola wako Mlezi atupambanulie ni
ng'ombe gani? Akasema: Hakika Yeye anasema kwamba ng'ombe huyo si mpevu, wala
si kinda, bali ni wa katikati baina ya hao. Basi fanyeni mnavyo amrishwa.
69. Wakasema: Tuombee kwa Mola wako atupambanulie nini
rangi yake? Akasema: Yeye anasema, kuwa ng'ombe huyo ni wa manjano, na rangi
yake imekoza, huwapendeza wanao mtazama.
70. Wakasema: Tuombee kwa Mola wako Mlezi atupambanulie ni
yupi? Hakika tunaona ng'ombe wamefanana. Na kwa yakini, Inshaallah, Mwenyezi
Mungu akipenda, tutaongoka.
71. Akasema: Yeye anasema: Kuwa huyo ni ng'ombe asiye tiwa
kazini kulima ardhi wala kumwagia maji mimea, mzima, hana baka. Wakasema: Sasa
umeleta haki. Basi wakamchinja, na walikaribia kuwa wasifanye hayo.
72. Na mlipo muuwa mtu, kisha mkakhitalifiana kwayo, na
Mwenyezi Mungu ni mwenye kuyatoa hayo mliyo kuwa mkiyaficha.
73. Tukasema: Mpigeni kwa kipande chake (huyo ng'ombe).
Ndivyo hivi Mwenyezi Mungu huwahuisha wafu; na anakuonyesheni Ishara zake ili
mpate kufahamu.
74. Kisha nyoyo zenu zikawa ngumu baada ya hayo, hata
zikawa kama mawe au ngumu zaidi; kwani kuna mawe yanayo timbuka mito, na kuna
mengine yanayo pasuka yakatoka maji ndani yake, na kuna mengine huanguka kwa
sababu ya khofu ya Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu si mwenye kughafilika na
mnayo yafanya.
75. Mnatumai watakuaminini na hali baadhi yao walikuwa
wakisikia maneno ya Mwenyezi Mungu, kisha wakayabadili baada ya kuwa
wameyafahamu, na hali wanajua?
76. Na wanapo kutana na wale walio amini husema: Tumeamini.
Na wanapo kuwa peke yao, wao kwa wao, husema: Mnawaambia aliyo kufunulieni
Mwenyezi Mungu ili wapate kukuhojieni mbele ya Mola wenu Mlezi? Basi hamfahamu
nyinyi?
77. Hawajui ya kwamba Mwenyezi Mungu anayajua wanayo
yaficha na wanayo yatangaza?
78. Na wako miongoni mwao wasio jua kusoma; hawakijui
Kitabu isipo kuwa uwongo wanao utamani, nao hawana ila ni kudhania tu.
79. Basi ole wao wanao andika kitabu kwa mikono yao, kisha
wakasema: Hiki kimetoka kwa Mwenyezi Mungu, ili wachumie kwacho pato dogo. Basi
ole wao kwa yale iliyo andika mikono yao, na ole wao kwa yale wanayo yachuma.
80. Na walisema: Hautatugusa Moto ila kwa siku chache tu.
Sema: Mmechukua ahadi kwa Mwenyezi Mungu? Kweli Mwenyezi Mungu hatokwenda
kinyume na ahadi yake. Au mnamsingizia Mwenyezi Mungu mambo msiyo yajua?
81. Naam, anaye chuma ubaya - na makosa yake yakamzunguka -
hao ndio watu wa Motoni; humo watadumu.
82. Na wale walio amini na wakatenda mema, hao ndio watu wa
Peponi, humo watadumu.
83. Na tulipo funga agano na Wana wa Israili: Hamtamuabudu
yeyote ila Mwenyezi Mungu; na muwafanyie wema wazazi na jamaa na mayatima na
masikini, na semeni na watu kwa wema, na shikeni Sala, na toeni Zaka. Kisha
mkageuka isipo kuwa wachache tu katika nyinyi; na nyinyi mnapuuza.
84. Na tulipo chukua agano lenu kuwa hamtamwaga damu zenu,
wala hamtatoana majumbani mwenu; nanyi mkakubali nanyi mnashuhudia.
85. Kisha nyinyi kwa nyinyi mnauwana, na mnawatoa baadhi
yenu majumbani kwao, mkisaidiana kwa dhambi na uadui. Na wakikujieni mateka
mnawakomboa, na hali kuwatoa mmekatazwa. Je! Mnaamini baadhi ya Kitabu na
mnakataa baadhi yake? Basi hana malipo mwenye kutenda hayo miongoni mwenu ila
hizaya katika maisha ya duniani, na Siku ya Kiyama watapelekwa kwenye adhabu
kali kabisa. Na Mwenyezi Mungu si mwenye kughafilika na yale mnayo yatenda.
86. Hao ndio walio nunua uhai wa dunia kwa (uhai wa)
Akhera; kwa hivyo hawatapunguziwa adhabu wala hawatanusuriwa.
87. Na hakika tulimpa Musa Kitabu na tukafuatisha baada
yake Mitume wengine. Na tukampa Isa, mwana wa Mariamu, hoja zilizo waziwazi, na
tukamtia nguvu kwa Roho Takatifu. Basi kila walipo kufikieni Mitume kwa yale
ambayo hayapendwi na nafsi zenu, mlijivuna; wengine mkawakanusha, na wengine
mkawauwa.
88. Na walisema: Nyoyo zetu zimefunikwa. Bali Mwenyezi
Mungu amewalaani kwa kufuru zao: kwa hivyo ni kidogo tu wanayo yaamini.
89. Na kilipo wajia Kitabu kitokacho kwa Mwenyezi Mungu
kinacho thibitisha waliyo nayo - na wao walikuwa wakitafutia ushindi kuwashinda
makafiri - yalipo wajia yale waliyo kuwa wakiyajua waliyakanusha. Basi laana ya
Mwenyezi Mungu juu ya wakanushao!
90. Kiovu kweli walicho jiuzia nafsi zao, nacho ni kule
kukataa kwao aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu, kwa ajili ya kuona maya kwa kuwa
Mwenyezi Mungu humteremshia fadhila yake amtakaye miongoni mwa waja wake. Basi
wamejiletea wenyewe ghadhabu juu ya ghadhabu. Na makafiri watapata mateso ya
kudhalilisha.
91. Na wanapo ambiwa: Yaaminini aliyo yateremsha Mwenyezi
Mungu. Wao husema: Tunaamini tuliyo teremshiwa sisi. Na huyakataa yasiyo kuwa
hayo. Na hali ya kuwa hii ndiyo Haki inayo thibitisha yale waliyo nayo wao.
Sema: Mbona mliwauwa Manabii wa Mwenyezi Mungu hapo zamani ikiwa kweli mlikuwa
Waumini?
92. Na alikufikieni Musa na hoja zilizo waziwazi, kisha
mkamchukua ndama (kumuabudu) baada yake, na mkawa wenye kudhulumu.
93. Na tulipo chukua ahadi yenu na tukauinua mlima juu yenu
(tukakwambieni): Kamateni kwa nguvu haya tuliyo kupeni na sikieni. Wakasema:
Tumesikia na tumekataa! Na wakanyweshwa nyoyoni mwao (imani ya) ndama kwa
kufuru yao. Sema: Ni uovu mno iliyo kuamrisheni imani yenu ikiwa ni wenye
kuamini.
94. Sema: Ikiwa nyumba ya Akhera iliyoko kwa Mwenyezi Mungu
ni yenu tu bila ya watu wengine, basi tamanini mauti kama nyinyi mnasema kweli.
95. Wala hawatayatamani kamwe kwa sababu ya yale yaliyo
tangulizwa na mikono yao; na Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwajua vyema wanao
dhulumu.
96. Na hakika utawaona ni wenye kuwashinda watu wote kwa
pupa ya kuishi, na kuliko washirikina. Kila mmoja wao anatamani lau angeli pewa
umri wa miaka elfu. Wala hayo ya kuzidishiwa umri hayamuondoshei adhabu; na
Mwenyezi Mungu anayaona wanayo yatenda.
97. Sema: Aliye kuwa ni adui wa Jibril, basi huyo ndiye
aliye iteremsha Qur'ani moyoni mwako kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, inayo
thibitisha yaliyo kuwa kabla yake, na ni uwongofu na bishara njema kwa Waumini.
98. Aliye kuwa adui wa Mwenyezi Mungu na Malaika wake na
Mitume wake na Jibril na Mikail, basi hakika Mwenyezi Mungu ni adui wa
makafiri.
99. Hakika tumekuteremshia Ishara zilizo wazi na hapana
wanao zikataa ila wapotovu.
100. Je! Ati ndio kila wanapo funga ahadi huwapo kikundi
miongoni mwao kikaivunja? Bali wengi wao hawaamini.
|