91. SURAT ASH-SHAMS
(Imeteremka
Makka)
Mwenyezi Mungu Mtukufu
ameapa kuanzia Sura hii kwa vitu kadhaa wa kadhaa miongoni mwa viumbe vyake
vitukufu, vyenye kueleza utimilivu wa uweza wake Mwenyezi Mungu Mtukufu na
Upweke wake, juu ya kufuzu kwa mwenye kuisafisha nafsi yake kwa Imani na
ut'iifu, na kukhasiri kwa kupinga mwenye kuidhoofisha kwa ukafiri na maasi.
Kisha ikaingilia mfano wa Thamudi, kaumu ya Saleh, na yaliyo wafika hao, ili
apate kuzingatia kila mwenye inda mwenye kukadhibisha. Kwani hakika wao walipo
mkadhibisha Mtume wao, na wakamuuwa yule ngamia, Mwenyezi Mungu aliwaangamiza
wote, na Yeye hakhofu matokeo ya kuwaangamiza hao, na aliyo wateremshia, kwani
Yeye hasailiwi kwa anayo yatenda, na hakika amewateremshia wanayo stahiki.
KWA JINA LA MWENYEZI
MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
1. Naapa kwa jua na mwangaza wake!
2. Na kwa mwezi unapo lifuatia!
3. Na kwa mchana unapo lidhihirisha!
4. Na kwa usiku unapo lifunika!
5. Na kwa mbingu na kwa aliye ijenga!
6. Na kwa ardhi na kwa aliye itandaza!
7. Na kwa nafsi na kwa aliye itengeneza!
8. Kisha akaifahamisha uovu wake na wema wake,
9. Hakika amefanikiwa aliye itakasa,
10. Na hakika amekhasiri aliye iviza.
11. Kina Thamudi walikadhibisha kwa sababu ya upotofu wao,
12. Alipo simama mwovu wao mkubwa,
13. Hapo Mtume wa Mwenyezi Mungu alipo waambia: Huyu ni
ngamia wa Mwenyezi Mungu, mwacheni anywe maji fungu lake.
14. Lakini walimkadhibisha na wakamchinja ngamia, kwa hivyo
Mola wao Mlezi aliwaangamiza kwa sababu ya dhambi zao na akawafuta kabisa.
15. Wala
Yeye haogopi matokeo yake.
|