101 - 120
101. Enyi mlio amini! Msiulize mambo ambayo mkidhihirishiwa
yatakuchukizeni. Na mkiyauliza inapo teremshwa Qur'ani mtabainishiwa. Mwenyezi Mungu amesamehe hayo. Na Mwenyezi
Mungu ni Mwenye maghfira Mpole.
102. Waliyauliza
hayo watu wa kabla yenu, kisha wakawa wenye kuyakataa.
103. Mwenyezi
Mungu hakujaalia uharamu wowote juu ya "Bahira" wala
"Saiba" wala "Wasila" wala "Hami". Lakini walio
kufuru humzulia uwongo Mwenyezi Mungu, na wengi wao hawatumii akili.
104. Na wanapo
ambiwa: Njooni kwenye yale aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu, na kwa Mtume,
husema: Yanatutosha tuliyo wakuta nayo baba zetu. Je, hata ikiwa baba zao
walikuwa hawajui kitu wala hawakuongoka?
105. Enyi mlio amini! Kilicho lazima juu yenu ni nafsi
zenu. Hawakudhuruni walio potoka ikiwa nyinyi mmeongoka. Ni kwa Mwenyezi Mungu
ndio marudio yenu nyote; basi atakwambieni yale mliyo kuwa mkiyatenda.
106. Enyi mlio amini! Yanapo mfikia mauti mmoja wenu na
akataka kutoa wasia, basi wawepo mashahidi wawili miongoni mwenu ambao ni
waadilifu. Na mnapo kuwa safarini, na msiba wa mauti ukakusibuni, basi
washuhudie wengineo wawili wasio kuwa katika nyinyi. Mtawazuia wawili hao baada
ya Sala na waape kwa Mwenyezi Mungu, mkitilia shaka, wakisema: Hatutopokea
thamani yoyote kwa haya hata kwa ajili ya jamaa; na wala hatutaficha ushahidi
wa Mwenyezi Mungu; hakika hapo tutakuwa miongoni mwa wenye dhambi.
107.Ikigundulikana kuwa wawili hao wamestahiki dhambi, basi
wawili wengineo kutokana na warithi wenye kudai haki washike makamo ya wa mwanzo.
Nao waape kwa Mwenyezi Mungu wakisema: Hakika ushahidi wetu ni wa haki zaidi
kuliko ushahidi wa wale. Na sisi hatujafanya dhambi; hakika hapo tutakuwa
miongoni mwa walio dhulumu.
108. Hivi inaelekea zaidi ya kwamba watatoa ushahidi ulio
sawa au wataogopa visije vikaletwa viapo vingine baada ya viapo vyao. Na mcheni
Mwenyezi Mungu na msikie. Na hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi wapotofu.
109. Ile siku ambayo Mwenyezi Mungu atapo wakusanya Mitume
awaambie: Mlijibiwa nini? Watasema: Hatuna ujuzi; hakika Wewe ndiye Mjuzi
Mkubwa wa yote yaliyo fichikana.
110. Na pale Mwenyezi Mungu atapo sema: Ewe Isa bin
Maryamu! Kumbuka neema yangu juu yako, na juu ya mama yako, nilipo kutia nguvu
kwa Roho Takatifu, ukazungumza na watu katika utoto na utuuzimani. Na nilivyo
kufunza kuandika na hikima na Taurati na Injili. Na ulipo tengeneza udongo sura
ya ndege, kwa idhini yangu, kisha ukapuliza ikawa ndege kwa idhini yangu; na
ulipo waponesha vipofu na wakoma kwa idhini yangu; na ulipo wafufua wafu kwa
idhini yangu; na nilipo kukinga na Wana wa Israili ulipo wajia na hoja zilizo
wazi, na wakasema walio kufuru miongoni mwao: Haya si lolote ila ni uchawi
mtupu!
111. Na nilipo wafunulia Wanafunzi kwamba waniamini Mimi na
Mtume wangu, wakasema: Tumeamini na shuhudia kuwa sisi ni Waislamu.
112. Wanafunzi walipo sema: Ewe Isa bin Maryamu! Je, Mola
wako Mlezi anaweza kututeremshia chakula kutoka mbinguni? Akasema: Mcheni
Mwenyezi Mungu ikiwa nyinyi ni Waumini.
113. Wakasema: Tunataka kukila chakula hicho, na nyoyo zetu
zitue, na tujue kwamba umetuambia kweli, na tuwe miongoni mwa wanao shuhudia.
114. Akasema Isa bin Maryamu: Ewe Mwenyezi Mungu, Mola
Mlezi wetu! Tuteremshia chakula kutoka mbinguni ili kiwe Sikukuu kwa ajili ya
wa mwanzo wetu na wa mwisho wetu, na kiwe ni Ishara itokayo kwako. Basi
turuzuku, kwani Wewe ndiye mbora wa wanao ruzuku.
115. Mwenyezi Mungu akasema: Hakika Mimi nitakuteremshieni
hicho. Lakini yeyote katika nyinyi atakaye kanya baadae, basi hakika Mimi
nitampa adhabu nisiyopata kumpa yeyote katika walimwengu.
116. Na pale Mwenyezi Mungu atakapo sema: Ewe Isa bin
Maryamu! Ati wewe uliwaambia watu: Nifanyeni mimi na mama yangu kuwa ni miungu
badala ya Mwenyezi Mungu? (Na Isa) atasema: Subhanaka, Wewe umetakasika!
Hainifalii mimi kusema ambayo si haki yangu. Ikiwa nilisema basi bila ya shaka
umekwisha yajua. Wewe unayajua yaliyo ndani ya nafsi yangu, lakini mimi siyajui
yaliyo katika nafsi yako. Hakika Wewe ndiye Mjuzi mkubwa wa yaliyo fichikana.
117. Sikuwaambia lolote ila uliyo niamrisha, nayo ni: Muabuduni
Mwenyezi Mungu, Mola wangu Mlezi na Mola wenu Mlezi. Na mimi nilikuwa shahidi
juu yao nilipo kuwa nao. Na ulipo nifisha ukawa Wewe ndiye Muangalizi juu yao.
Na Wewe ni shahidi juu ya kila kitu.
118. Ukiwaadhibu basi hao ni waja wako. Na ukiwasamehe basi
Wewe ndiye Mwenye nguvu na Mwenye hikima.
119. Mwenyezi Mungu atasema: Hii ndiyo Siku ambayo wasemao
kweli utawafaa ukweli wao. Wao watapata Bustani zipitazo mito kati yake. Humo
watadumu milele. Mwenyezi Mungu amewawia radhi, nao wawe radhi naye. Huku ndiko kufuzu kukubwa.
120. Mwenyezi
Mungu ndiye Mwenye ufalme wa mbingu na ardhi na vilivyomo. Naye ni Muweza wa
kila kitu.
|