1 - 50
1. Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu aliye umba mbingu
na ardhi, na akafanya giza na mwangaza. Tena baada ya haya walio kufuru
wanawafanya wengine sawa na Mola wao Mlezi.
2. Yeye ndiye aliye kuumbeni kwa udongo, kisha
akakuhukumieni ajali, na muda maalumu uko kwake tu. Tena baada ya haya nyinyi
mnatia shaka.
3. Na Yeye ndiye Mwenyezi Mungu mbinguni na ardhini. Anajua
ya ndani yenu na ya nje yenu. Na anajua mnayo yachuma.
4. Na haiwafikii hata ishara moja katika ishara za Mola wao
Mlezi ila wao huwa wenye kuipa nyongo.
5. Wameikanusha Haki ilipo wajia. Basi zitawajia khabari za
yale waliyo kuwa wakiyakejeli.
6. Jee, hawaoni vizazi vingapi tulivyo viangamiza kabla
yao? Tuliwaweka katika nchi tusivyo kuwekeni nyinyi; tukawapelekea mvua nyingi
na tukaifanya mito inapita chini yao. Mwishoe tukawaangamiza kwa madhambi yao;
na tukaanzisha baada yao kizazi kingine.
7. Na lau tungeli kuteremshia kitabu cha karatasi,
wakakigusa kwa mikono yao, wangeli sema walio kufuru: Haya si chochote ila ni
uchawi dhaahiri.
8. Na wao husema: Mbona hakuteremshiwa Malaika? Na kama
tungeli teremsha Malaika, basi bila ya shaka ingesha hukumiwa amri, tena hapo
wasingeli pewa muhula.
9. Na kama tungeli mfanya Malaika bila ya shaka tungeli
mfanya kama binaadamu, na tungeli watilia matatizo yale wanayo yatatiza wao.
10. Na hakika Mitume walio kabla yako walifanyiwa kejeli,
lakini walio wafanyia kejeli wakaja kuzungukwa na yale yale waliyo kuwa wao
wanayafanyia kejeli.
11. Sema: Tembeeni ulimwenguni, kisha mtazame ulikuwaje
mwisho wa wanao kanusha.
12. Sema: Ni vya nani viliomo katika mbingu na katika ardhi?
Sema: Ni vya Mwenyezi Mungu. Yeye amejilazimisha nafsi yake kurehemu. Hakika
atakukusanyeni Siku ya Kiyama isiyo kuwa na shaka. Walio jikhasiri wenyewe hawaamini.
13. Na ni vyake vilio tulia usiku na mchana. Naye ndiye
Mwenye kusikia na Mwenye kujua.
14. Sema: Je, nimchukue rafiki mlinzi asiye kuwa Mwenyezi
Mungu, ambaye ndiye Muumba mbingu na ardhi, naye ndiye anaye lisha wala
halishwi? Sema: Mimi nimeamrishwa niwe wa kwanza wa wenye kusilimu. Na wala
kabisa usiwe miongoni wa washirikina.
15. Sema: Mimi naogopa adhabu ya Siku kubwa hiyo ikiwa
nitamuasi Mola wangu Mlezi.
16. Siku hiyo yule atakaye epushwa nayo adhabu hiyo atakuwa
Mwenyezi Mungu amemrehemu. Na huko ndiko kufuzu kulio wazi.
17. Na ikiwa Mwenyezi Mungu akikugusisha madhara, basi
hapana wa kukuondolea hayo ila Yeye. Na ikiwa akikugusisha kheri, basi Yeye
ndiye Mwenye uweza wa kila kitu.
18. Naye ndiye Mwenye nguvu juu ya waja wake, na ndiye
Mwenye hikima na Mwenye khabari zote.
19. Sema: Kitu gani ushahidi wake mkubwa kabisa? Sema:
Mwenyezi Mungu. Yeye ndiye shahidi baina yangu na nyinyi. Na nimefunuliwa
Qur'ani hii ili kwayo nikuonyeni nyinyi na kila inayo mfikia. Ati kweli nyinyi
mnashuhudia kuwa pamoja na Mwenyezi Mungu wapo miungu wengine? Sema: Mimi
sishuhudii hayo. Sema: Hakika Yeye ni Mungu mmoja tu, nami ni mbali na mnao
washirikisha.
20. Wale Tulio wapa Kitabu wanayajua haya kama wanavyo
wajua watoto wao. Wale walio zikhasiri nafsi zao hawaamini.
21. Na nani dhaalimu zaidi kuliko anaye mzulia uwongo
Mwenyezi Mungu, na akazikanusha Ishara zake? Hakika madhaalimu hawafanikiwi.
22. Siku tutapo wakusanya wote pamoja, kisha tuwaambie
walio shirikisha: Wako wapi washirikishwa wenu mlio kuwa mnadai?
23. Kisha hautakuwa udhuru wao ila ni kusema: Wallahi! Mola
wetu Mlezi! Hatukuwa washirikina.
24. Tazama jinsi wanavyo jisemea uwongo wenyewe. Na
yamewapotea waliyo kuwa wakiyazua.
25. Na wapo miongoni mwao wanao kusikiliza; na tumezitia
pazia nyoyo zao wasije kuyafahamu. Na upo uziwi masikioni mwao, na wakiona kila
Ishara hawaiamini. Hata wakikujia kwa kujadiliana nawe, wanasema walio kufuru:
Hizi si chochote ila hadithi za watu wa kale.
26. Nao huwazuia watu, na wao wenyewe wanajitenga nayo. Nao
hawaangamizi ila nafsi zao tu, wala wao hawatambui.
27. Na unge ona watakapo simamishwa kwenye Moto, wakawa
wanasema: Laiti tungeli rudishwa, wala hatutakanusha tena Ishara za Mola wetu
Mlezi, na tutakuwa miongoni wa Waumini.
28. Bali yamewadhihirikia waliyo kuwa wakiyaficha zamani.
Na kama wangeli rudishwa bila ya shaka wange yarejea yale yale waliyo katazwa.
Na hakika hao ni waongo.
29. Na walisema: Hakuna mengine ila maisha yetu haya ya
duniani, wala sisi hatutafufuliwa.
30. Na lau ungeli ona watavyo simamishwa mbele ya Mola wao
Mlezi, akawaambia: Je, si kweli haya? Na wao watasema: Kwani? Tunaapa kwa Mola
Mlezi wetu ni kweli. Yeye atasema: Basi onjeni adhabu kwa sababu ya vile mlivyo
kuwa mnakataa.
31. Hakika wamekhasirika walio kanusha kukutana na Mwenyezi
Mungu, mpaka ilipo wajia Saa kwa ghafla, wakasema: Ole wetu kwa tuliyo yapuuza!
Nao watabeba mizigo yao juu ya migongo yao. Ni maovu hayo wanayo yabeba.
32. Na maisha ya dunia si chochte ila ni mchezo na pumbao
tu. Na hakika nyumba ya Akhera ni bora zaidi kwa wanao mcha Mungu. Basi, je, hamtii akilini?
33. Tunajua ya
kwamba yanakuhuzunisha wanayo yasema. Basi hakika wao hawakukanushi wewe,
lakini hao madhaalimu wanazikataa Ishara za Mwenyezi Mungu.
34. Na hakika
walikanushwa Mitume wa kabla yako. Nao wakavumilia kule kukanushwa, na
kuudhiwa, mpaka ilipo wafikia nusura yetu. Na hapana wa kubadilisha maneno ya
Mwenyezi Mungu. Na bila ya shaka zimekujia baadhi ya khabari za Mitume hao.
35. Na ikiwa ni
makubwa kwako huku kukataa kwao, basi kama unaweza kutafuta njia ya chini kwa
chini ya ardhi, au ngazi kwendea mbinguni ili uwaletee Ishara -- Na lau kuwa
Mwenyezi Mungu angependa angeli wakusanya kwenye uwongofu. Basi usiwe
miongoni mwa wasio jua.
36. Hakika wanao kubali ni wale wanao sikia. Na ama wafu
Mwenyezi Mungu atawafufua, na kisha kwake Yeye ndio watarejeshwa.
37. Na wamesema: Kwa nini hakuteremshiwa muujiza kutoka kwa
Mola wake Mlezi? Sema: Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kuteremsha muujiza. Lakini wengi wao hawajui.
38. Na
hapana mnyama katika ardhi, wala ndege anaye ruka kwa mbawa zake mbili, ila ni
umma kama nyinyi. Hatukupuuza Kitabuni kitu chochote. Kisha kwa Mola wao Mlezi
watakusanywa.
39. Na
walio kanusha Ishara zetu ni viziwi na mabubu waliomo gizani. Mwenyezi Mungu humwachia
kupotea amtakaye, na humweka katika Njia iliyo nyooka amtakaye.
40. Sema:
Mwaonaje ikikujieni adhabu ya Mwenyezi Mungu, au ikakufikieni hiyo Saa - mtamwomba
asiye kuwa Mwenyezi Mungu, ikiwa nyinyi ni wakweli?
41. Bali
Yeye ndiye mtakaye mwomba, naye atakuondoleeni mnacho mwombea akipenda. Na
mtasahau hao mnao wafanya washirika wake.
42. Na kwa
yakini tulipeleka Mitume kwa kaumu zilizo kuwa kabla yako, kisha tukazitia
katika dhiki na mashaka ili zipate kunyenyekea.
43. Kwa
nini wasinyenyekee ilipo wafika adhabu yetu? Lakini nyoyo zao zilikuwa ngumu,
na Shet'ani akawapambia waliyo kuwa wakiyafanya.
44. Basi
walipo sahau walio kumbushwa tuliwafungulia milango ya kila kitu. Mpaka walipo
furahia yale waliyo pewa tuliwashika kwa ghafla, na mara wakawa wenye kukata
tamaa.
45.
Ikakatwa mizizi ya watu walio dhulumu - na wa kuhimidiwa ni Mwenyezi Mungu,
Mola Mlezi wa viumbe vyote.
46. Sema:
Mwaonaje Mwenyezi Mungu akanyakua kusikia kwenu, na kuona kwenu, na akaziziba
nyoyo zenu, ni mungu gani asiye kuwa Mwenyezi Mungu ataye kuleteeni hayo tena?
Angalia vipi tunavyo zieleza Ishara, kisha wao wanapuuza.
47. Sema:
Mwaonaje, ikikufikieni adhabu ya Mwenyezi Mungu kwa ghafla, au kwa dhaahiri,
jee wataangamizwa isipo kuwa walio dhulumu?
48. Na
hatuwatumi Mitume ila huwa ni wabashiri na waonyaji. Na wenye kuamini na
wakatenda mema haitakuwa khofu juu yao, wala hawatahuzunika.
49. Na
walio kanusha Ishara zetu itawagusa adhabu kwa walivyo kuwa wakipotoka.
50. Sema:
Mimi sikwambiini kuwa ninazo khazina za Mwenyezi Mungu. Wala sijui mambo
yaliyo fichikana. Wala sikwambiini kuwa mimi ni Malaika. Mimi sifuati ila
yanayo funuliwa kwangu. Sema: Je, wanakuwa sawa, kipofu na mwenye kuona. Basi
hamfikiri?
|