151 - 165
151. Sema: Njooni nikusomeeni aliyo kuharimishieni Mola
wenu Mlezi. Nayo ni kuwa, msimshirikishe Yeye na chochote. Na wazazi wenu wafanyieni
wema. Wala msiwauwe watoto wenu kwa sababu ya umasikini. Sisi tunakuruzukuni
nyinyi na wao. Wala msikaribie mambo machafu, yanayo onekana, na yanayo
fichikana. Wala msiuwe nafsi ambayo Mwenyezi Mungu ameharimisha kuiuwa, ila
ikiwa kwa haki. Hayo amekuusieni ili myatie akilini.
152. Wala msiyakaribie mali ya yatima ila kwa njia ya wema
kabisa, mpaka afikilie utu-uzima. Na timizeni vipimo na mizani kwa uadilifu.
Sisi hatumkalifishi mtu ila kwa kadiri ya uwezo wake. Na msemapo semeni kwa
uadilifu ingawa ni jamaa. Na ahadi ya Mwenyezi Mungu itekelezeni. Hayo
amekuusieni ili mpate kukumbuka.
153. Na kwa hakika hii ndiyo Njia yangu Iliyo Nyooka. Basi
ifuateni, wala msifuate njia nyingine, zikakutengeni na Njia yake. Haya
amekuusieni ili mpate kuchamngu.
154. Tena tulimpa Musa Kitabu kwa kumtimizia (neema) aliye
fanya wema, na kuwa ni maelezo ya kila kitu, na uwongofu na rehema, ili wapate
kuamini mkutano wao na Mola wao Mlezi.
155. Na hichi ni Kitabu tulicho kiteremsha, kilicho
barikiwa. Basi kifuateni, na mchenimngu, ili mrehemewe.
156. Msije mkasema: Hakika mataifa mawili kabla yetu
yameteremshiwa Kitabu; na sisi tulikuwa hatuna khabari ya waliyo kuwa
wakiyasoma.
157. Au mkasema: Lau kuwa tumeteremshiwa sisi Kitabu
tungeli kuwa waongofu zaidi kuliko wao. Basi imekufikieni bayana kutoka kwa
Mola wenu Mlezi, na uwongofu, na rehema. Basi nani aliye dhaalimu mkubwa zaidi
kuliko yule anaye kanusha Ishara za Mwenyezi Mungu, na akajitenga nazo?
Tutawalipa wanao jitenga na Ishara zetu adhabu kali kabisa kwa sababu ya
kujitenga kwao.
158. Wanangoja jengine ila wawafikie Malaika, au awafikie
Mola wako Mlezi, au zifike baadhi ya Ishara za Mola wako Mlezi? Siku zitakapo
fika baadhi ya Ishara za Mola wako Mlezi, kuamini hapo hakutomfaa mtu kitu,
ikiwa hakuwa ameamini kabla yake, au amefanya kheri katika Imani yake. Sema:
Ngojeni, nasi pia tunangoja.
159. Hakika walio igawa Dini yao na wakawa makundi makundi,
huna ukhusiano nao wowote. Bila ya shaka shauri yao iko kwa Mwenyezi Mungu;
kisha atawaambia yale waliyo kuwa wakiyatenda.
160. Afanyae wema atalipwa mfano wake mara kumi. na afanyae
ubaya hatalipwa ila sawa nao tu. Na wao hawatadhulumiwa.
161. Sema: Kwa hakika mimi Mola wangu Mlezi ameniongoa
kwenye Njia Iliyo Nyooka, Dini iliyo sawa kabisa, ambayo ndiyo mila ya Ibrahim
aliye kuwa mwongofu, wala hakuwa miongoni mwa washirikina.
162. Sema: Hakika Sala yangu, na ibada zangu, na uhai
wangu, na kufa kwangu, ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe
vyote.
163. Hana
mshirika wake. Na hayo ndiyo niliyo amrishwa, na mimi ni wa kwanza wa Waislamu.
164. Sema:
Je nitafute Mola Mlezi asiye kuwa Mwenyezi Mungu, na hali Yeye ndiye Mola Mlezi
wa kila kitu? Na kila nafsi haichumii ila nafsi yake. Na habebi mwenye kubeba
mzigo wa mwenziwe. Kisha marejeo yenu ni kwa Mola wenu Mlezi, naye atakuambieni
mliyo kuwa mkikhitalifiana.
165. Naye
ndiye aliye kufanyeni makhalifa wa duniani, na amewanyanyua baadhi yenu juu ya
wengine daraja kubwa kubwa, ili akujaribuni kwa hayo aliyo kupeni. Hakika Mola
Mlezi wako ni Mwepesi wa kuadhibu, na hakika Yeye ni Mwenye kusamehe, Mwenye
kurehemu.
|