7. SURAT AL- A'RAAF
(Imeteremka
Makka)
Sura
hii imeteremka Makka isipo kuwa Aya nane, nazo ni 163 mpaka 170. Na idadi za
Aya zake ni 206.
Mwanzo wa Sura hii ni kuendeleza yaliyo kuja mwisho wa Sura ya Al-Ana'm, na
baada ya hayo imeingia kueleza khulka ya kibinaadamu. Ikataja kisa cha Adam na
Hawa, na walivyo toka kwenye Bustani kwa kutiwa wasiwasi na Shet'ani, na
ikaeleza huo wasiwasi unaoendelea kwa watu katika mavazi na chakula. Kisha Aya
za Sura hii tukufu, kama sura nyengine za Qur'ani zikaingia kutupia jicho
kwenye mbingu na ardhi na viliomo ndani yao, na kuzingatia uumbaji wake wa
ajabu.
Kadhaalika Sura hii imeeleza hadithi za Manabii kama Nuhu na Hud na kaumu yake
kina A'ad. Kisha hadithi ya Saleh na kaumu yake, Thamud, walio sifika kwa nguvu
zao na wakapewa utajiri; na hadithi ya Lut' na kaumu yake, na ikataja maovu
waliyo kuwa wakiyafanya; na hadithi ya Shua'ib na watu wa Madyana. Na baada ya
hadithi hizo za kweli Sura imeeleza mafunzo na mazingatio yaliyomo. Naye
Subhanahu wa Ta'ala amefuatilizia hayo kwa kisa cha Musa na yaliyo tokea katika
mambo ya Firauni.
Na Sura ikakhitimishia kwa kumathilisha nini hali ya mwenye kupewa hidaya
khalafu akabanduka kwenye uwongofu akaingia kwenye upotovu kwa kumfwata
Shet'ani, na Sura pia ikamalizia kueleza Wito wa kuendea Haki alio kuja nao
Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.
KWA JINA LA MWENYEZI
MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
|