Chapter 20
1 Siku moja, Yesu alipokuwa akiwafundisha watu Hekaluni na
kuwahubiria juu ya Habari Njema, makuhani wakuu na walimu wa Sheria pamoja na
wazee walifika,
2 wakasema, "Tuambie! Unafanya mambo haya kwa mamlaka
gani?"
3 Yesu akawaambia, "Na mimi nitawaulizeni swali:
4 mamlaka ya Yohane ya kubatiza yalitoka kwa Mungu au kwa
watu?"
5 Lakini wao wakajadiliana hivi: "Tukisema yalitoka
mbinguni, yeye atatuuliza: `Mbona hamkumsadiki?`
6 Na tukisema yalitoka kwa binadamu, watu wote hapa
watatupiga mawe, maana wote wanaamini kwamba Yohane alikuwa nabii."
7 Basi, wakamwambia, "Hatujui mamlaka hayo yalitoka
wapi."
8 Yesu akawaambia, "Hata mimi sitawaambia ninafanya
mambo haya kwa mamlaka gani."
9 Yesu akaendelea kuwaambia watu mfano huu: "Mtu mmoja
alilima shamba la mizabibu, akalikodisha kwa wakulima; kisha akasafiri hadi
nchi ya mbali, akakaa huko kwa muda mrefu.
10 Wakati wa mavuno, mtu huyo alimtuma mtumishi wake kwa
wale wakulima, akachukue sehemu ya matunda ya shamba la mizabibu. Lakini wale
wakulima wakampiga mtumishi huyo wakamrudisha mikono mitupu.
11 Yule bwana akamtuma tena mtumishi mwingine; lakini wao
wakampiga huyo vilevile na kumtendea vibaya, wakamrudisha mikono mitupu.
12 Akamtuma tena wa tatu; huyu naye, baada ya kumwumiza,
wakamfukuza.
13 Yule mwenye shamba akafikiri: `Nitafanya nini? Nitamtuma
mwanangu mpenzi; labda watamjali yeye.`
14 Wale wakulima walipomwona tu, wakasemezana: `Huyu ndiye
mrithi. Basi, tumwue ili urithi wake uwe wetu.`
15 Basi, wakamtoa nje ya lile shamba la mizabibu,
wakamwua." Yesu akauliza, "Yule mwenye shamba atawafanya nini hao
wakulima?
16 Atakuja kuwaangamiza wakulima hao, na atawapa wakulima
wengine hilo shamba la mizabibu." Watu waliposikia maneno hayo, walisema:
"Hasha! Yasitukie hata kidogo!"
17 Lakini Yesu akawatazama, akawaambia, "Maandiko haya
Matakatifu yana maana gani basi? `Jiwe walilokataa waashi, sasa limekuwa jiwe
kuu la msingi!`
18 Mtu yeyote akianguka juu ya jiwe hilo, atavunjika
vipandevipande; na likimwangukia mtu yeyote, litamsaga kabisa."
19 Walimu wa Sheria na makuhani wakuu walifahamu kwamba
mfano huo ulikuwa unawahusu, na hivyo walitaka kumkamata palepale, ila tu
waliogopa watu.
20 Basi, wakawa wanatafuta wakati wa kufaa. Wakawahonga
watu fulani wajisingizie kuwa wema, wakawatuma wamnase Yesu kwa maswali, na
hivyo waweze kumtia nguvuni na kumpeleka kwa wakuu wa serikali.
21 Hao wapelelezi wakamwambia, "Mwalimu, tunajua
kwamba unasema na kufundisha mambo ya kweli; tunajua kwamba wewe huna ubaguzi;
wewe wafundisha ukweli juu ya njia ya Mungu.
22 Basi, twambie kama ni halali, au la, kulipa kodi kwa
Kaisari!"
23 Yesu alitambua mtego wao, akawaambia,
24 "Nionyesheni sarafu. Je, sura na chapa ni vya nani?"
25 Nao
wakamjibu, "Ni vya Kaisari." Yesu akawaambia, "Basi, mpeni
Kaisari vilivyo vyake Kaisari, na Mungu vilivyo vyake Mungu."
26 Hawakufaulu
kumnasa kwa neno lolote pale mbele ya watu na hivyo wakakaa kimya
wakilistaajabia jibu lake.
27 Kisha
Masadukayo, ambao husema kwamba wafu hawafufuki, wakamjia Yesu, wakasema:
28
"Mwalimu, Mose alituandikia kwamba kama ndugu ya mtu fulani akifa na
kumwacha mjane wake bila watoto, ni lazima ndugu yake amchukue huyo mama mjane,
amzalie watoto ndugu yake marehemu.
29 Sasa, wakati
mmoja kulikuwa na ndugu saba. Yule wa kwanza alioa na baadaye akafa bila kuacha
mtoto.
30 Yule ndugu wa
pili akamwoa yule mjane, naye pia, akafa;
31 na ndugu wa
tatu vilevile. Mambo yakawa yaleyale kwa wote saba - wote walikufa bila kuacha
watoto.
32 Mwishowe
akafa pia yule mwanamke.
33 Je, siku wafu
watakapofufuliwa, mwanamke huyo atakuwa mke wa nani? Alikuwa ameolewa na wote
saba."
34 Yesu
akawaambia, "Watu wa nyakati hizi huoa na kuolewa;
35 lakini wale
ambao Mungu atawawezesha kushiriki ule wakati wa ufufuo, hawataoa wala kuolewa.
36 Ama hakika,
hawawezi kufa tena, kwa sababu watakuwa kama malaika, na ni watoto wa Mungu kwa
vile wamefufuliwa katika wafu.
37 Lakini,
kwamba kuna kufufuka kutoka wafu, hata Mose alithibitisha jambo hilo katika
Maandiko Matakatifu. Katika sehemu ya Maandiko Matakatifu juu ya kile kichaka
kilichokuwa kinawaka moto, anamtaja Bwana kama Mungu wa Abrahamu, Isaka na
Yakobo.
38 Basi, yeye si
Mungu wa wafu, bali ni Mungu wa wale walio hai; maana wale aliowaita kwake,
wanaishi naye."
39 Baadhi ya
wale walimu wa Sheria wakasema, "Mwalimu, umejibu vema kabisa."
40 Walisema
hivyo kwa sababu hawakuthubutu kumwuliza tena maswali mengine.
41 Yesu akawauliza,
"Yasemekanaje kwamba Kristo ni mwana wa Daudi?
42 Maana Daudi
mwenyewe anasema katika Zaburi: `Bwana alimwambia Bwana wangu: Keti upande
wangu wa kulia
43 mpaka
niwafanye adui zako kama kiti cha kuwekea miguu yako.`
44 Ikiwa Daudi
anamwita yeye, `Bwana,` basi atakuwaje mwanawe?"
45 Yesu
aliwaambia wanafunzi wake mbele ya watu wote,
46
"Jihadharini na walimu wa Sheria ambao hupenda kupitapita wamevalia kanzu.
Hupenda kusalimiwa na watu kwa heshima masokoni, huketi mahali pa heshima
katika masunagogi na kuchukua nafasi za heshima katika karamu.
47 Huwadhulumu
wajane huku wakisingizia kuwa wema kwa kusali sala ndefu. Hao watapata hukumu
kali zaidi!"
|