Chapter 7
1 Yahusu
sasa mambo yale mliyoandika: naam, ni vizuri kama mtu haoi;
2 lakini
kwa sababu ya hatari ya uzinzi, basi, kila mwanamume na awe na mke wake
mwenyewe, na kila mwanamke awe na mume wake mwenyewe.
3 Mume
atimize wajibu alio nao kwa mkewe, naye mke atimize wajibu alio nao kwa mumewe.
4 Mke hana
mamlaka juu ya mwili wake, bali mumewe anayo; hali kadhalika naye mume, hana
mamlaka juu ya mwili wake, bali mkewe anayo.
5
Msinyimane haki zenu, isipokuwa kama mnaafikiana kufanya hivyo kwa kitambo tu,
ili mpate nafasi nzuri ya kusali. Kisha rudianeni tena mara, ili Shetani asije
akawajaribu kwa sababu ya udhaifu wenu.
6 Ninayowaambieni sasa ni mawaidha, si amri.
7 Ningependa watu wote wawe kama mimi nilivyo; lakini kila mmoja
anacho kipaji chake kutoka kwa Mungu; mmoja kipaji hiki na mwingine kile.
8 Basi, wale ambao hawajaoana na wale walio wajane
nawaambia kwamba ni vema kuendelea kuwa kama mimi nilivyo.
9 Hata hivyo, kama mtu hawezi kujizuia basi, na aoe; maana
ni afadhali zaidi kuoa kuliko kuwaka tamaa.
10 Kwa wale waliooa ninayo amri, tena si yangu, ila ni ya
Bwana: mke asiachane na mumewe;
11 lakini kama akiachana naye, basi abaki bila kuolewa; ama
la, apatanishwe na mume wake. Mume naye asimpe talaka mkewe.
12 Kwa wale wengine, (mimi binafsi, si Bwana) nasema hivi:
Ikiwa mwanamume Mkristo anaye mke asiyeamini, na huyo mwanamke akakubali
kuendelea kuishi naye, asimpe talaka.
13 Na, kama mwanamke Mkristo anaye mume asiyeamini, na huyo
mwanamume akakubali kuendelea kuishi naye, basi, asimpe talaka mumewe.
14 Kwa maana huyo mume asiyeamini hupokelewa kwa Mungu kwa
kuungana na mkewe; na huyo mke asiyeamini hupokelewa kwa Mungu kwa kuungana na
mumewe. Vinginevyo watoto wao wangekuwa si wa Mungu; kumbe sasa ni watoto wake
Mungu.
15 Hata hivyo, ikiwa yule asiyeamini anataka kumwacha
mwenzake aliye Mkristo, basi, na amwache tu. Hapo huyo Mkristo, mume au mke,
atakuwa huru. Maana Mungu amewaiteni ninyi muishi kwa amani.
16 Wewe mama Mkristo, unawezaje kuwa na hakika kwamba
hutaweza kumwokoa mume wako? Au wewe mume Mkristo, unawezaje kuwa na hakika
kwamba hutaweza kumwokoa mkeo?
17 Kwa vyovyote kila mmoja na aishi kufuatana na vipaji
alivyogawiwa na Bwana, na kama alivyoitwa na Mungu. Hili ndilo agizo langu kwa
makanisa yote.
18 Kama mtu aliitwa akiwa ametahiriwa, basi asijisingizie
kwamba hakutahiriwa; na kama alipoitwa hakuwa ametahiriwa, basi na asitahiriwe.
19 Maana kutahiriwa au kutotahiriwa si kitu; kilicho muhimu
ni kuzishika amri za Mungu.
20 Basi, kila mmoja na abaki kama alivyokuwa wakati
alipoitwa.
21 Je, wewe ulikuwa mtumwa wakati ulipoitwa? Sawa, usijali;
lakini ukipata fursa ya kuwa huru, itumie.
22 Maana yeye aliyeitwa na Bwana akiwa mtumwa huyo huwa mtu
huru wa Bwana. Hali kadhalika naye aliyeitwa akiwa mtu huru, huwa mtumwa wa
Kristo.
23 Nyote mmenunuliwa kwa bei; kwa hiyo msiwe tena watumwa
wa watu.
24 Ndugu zangu, kila mmoja wenu basi, na abaki na Mungu
kama alivyokuwa wakati alipoitwa.
25 Sasa, kuhusu mabikira na waseja, sina amri kutoka kwa
Bwana; lakini natoa maoni yangu mimi ambaye kwa huruma yake Bwana nastahili
kuaminiwa.
26 Basi, kutokana na shida iliyopo sasa nadhani ingefaa mtu
abaki kama alivyo.
27 Je, umeoa?
Basi, usitake kuachana na mkeo. Wewe hukuoa? Basi, usitake kuoa.
28 Lakini ikiwa
utaoa hutakuwa umetenda dhambi; na msichana akiolewa hatakuwa ametenda dhambi.
Hao watakaooana watapatwa na matatizo ya dunia hii, lakini mimi ningependa hayo
yasiwapate ninyi.
29 Ndugu, nataka
kusema hivi: muda uliobaki ni mfupi. Na tangu sasa wale waliooa na waishi kama vile hawakuoa;
30 wenye
kulia wawe kama hawalii, na wenye kufurahi wawe kama hawafurahi; wanaonunua
wawe kama hawana kitu;
31 nao
wenye shughuli na dunia hii wawe kama vile hawana shughuli sana nayo. Maana
ulimwengu huu, kama tuujuavyo, unapita.
32
Ningependa ninyi msiwe na wasiwasi. Mtu asiye na mke hujishughulisha na kazi ya
Bwana jinsi atakavyompendeza Bwana.
33 Mtu
aliyeoa hujishughulisha na mambo ya dunia jinsi atakavyompendeza mkewe,
34 naye
amegawanyika. Mwanamke asiyeolewa au bikira hujishughulisha na mambo ya Bwana
apate kujitolea mwili na roho kwa Bwana. Lakini mwanamke aliyeolewa
hujishughulisha na mambo ya dunia hii jinsi atakavyompendeza mumewe.
35
Nawaambieni haya kwa faida yenu, na si kwa kuwawekeeni kizuio. Nataka tu muwe
na mpango unaofaa, mpate kumtumikia Bwana kwa moyo na nia moja.
36 Kama
mtu anaona kwamba hamtendei vyema mchumba wake asipomwoa, na kama tamaa zake
zinamshinda, na afanye atakavyo; waoane tu; hatakuwa ametenda dhambi.
37 Lakini kama
huyo mwanamume akiamua kwa hiari moyoni mwake kutooa na kama anaweza kuzitawala
tamaa zake na kuamua namna ya kufanya, basi, anafanya vizuri zaidi asipomwoa
huyo mwenzake bikira.
38 Kwa
maneno mengine: yule anayeamua kumwoa huyo mchumba wake anafanya vema; naye
anayeamua kutomwoa anafanya vema zaidi.
39
Mwanamke huwa amefungwa na mumewe kwa muda wote mumewe aishipo. Lakini mumewe
akifa, mama huyo yuko huru, na akipenda anaweza kuolewa na mtu yeyote, mradi tu
iwe Kikristo.
40 Lakini,
nionavyo mimi, atakuwa na heri zaidi kama akibaki hivyo alivyo. Hayo ni maoni
yangu, na nafikiri mimi pia ninaye Roho wa Mungu.
|