Chapter 12
1 Nitajivuna basi, ingawa haifai! Lakini sasa nitasema juu
ya maono na ufunuo alivyonijalia Bwana.
2 Namjua mtu mmoja Mkristo, ambaye miaka kumi na minne
iliyopita alinyakuliwa mpaka katika mbingu ya tatu. (Sijui kama alikuwa huko
kwa mwili au kwa roho; Mungu ajua.)
3 Narudia: najua kwamba mtu huyo alinyakuliwa mpaka peponi.
(Lakini sijui kama alikuwa huko kwa mwili au kwa roho; Mungu ajua.)
4 Huko akasikia mambo ya siri ambayo binadamu hastahili
kuyatamka.
5 Basi, nitajivunia juu ya mtu wa namna hiyo, na si juu
yangu mimi binafsi, isipokuwa tu juu ya udhaifu wangu.
6 Kama ningetaka kujivuna singekuwa mpumbavu hata kidogo,
maana ningekuwa nasema ukweli mtupu. Lakini sitajivuna; sipendi mtu anifikirie
zaidi ya vile anavyoona na kusikia kutoka kwangu.
7 Lakini, kusudi mambo haya makuu niliyofunuliwa
yasinifanye nilewe majivuno, nilipewa maumivu mwilini kama mwiba, mjumbe wa
Shetani mwenye kunipiga nisijivune kupita kiasi.
8 Nilimsihi Bwana mara tatu kuhusu jambo hili ili linitoke.
9 Lakini akaniambia: "Neema yangu inatosha kwa ajili
yako; maana uwezo wangu hukamilishwa zaidi katika udhaifu." Basi, ni radhi
kabisa kujivunia udhaifu wangu ili uwezo wake Kristo ukae juu yangu.
10 Kwa hiyo nakubali kwa radhi udhaifu, madharau, taabu,
udhalimu na mateso, kwa ajili ya Kristo; maana ninapokuwa dhaifu, ndipo
ninapokuwa na nguvu.
11 Nimekuwa kama mpumbavu, lakini, ninyi mmenilazimisha
kuwa hivyo. Ninyi ndio mngalipaswa kunisifu. Maana, ingawa mimi si kitu, kwa
vyovyote, mimi si mdogo zaidi kuliko hao "mitume wakuu."
12 Miujiza na maajabu yaonyeshayo wazi kwamba mimi ni mtume
yalifanyika miongoni mwenu kwa uvumilivu wote.
13 Je, mlipungukiwa nini zaidi kuliko makanisa mengine,
isipokuwa tu kwamba mimi kwa upande wangu sikuwasumbueni kupata msaada wenu?
Samahani kwa kuwakoseeni haki hiyo!
14 Sasa niko tayari kabisa kuja kwenu mara ya tatu, na
sitawasumbua. Maana ninachotafuta si mali zenu, bali ni ninyi wenyewe. Ni
kawaida ya wazazi kuwawekea watoto wao akiba, na si watoto kuwawekea wazazi
wao.
15 Mimi ni radhi kabisa kutumia nilicho nacho, na hata
kujitolea mimi mwenyewe kabisa, kwa faida ya roho zenu. Je, mtanipenda kidogo
ati kwa kuwa mimi nawapenda ninyi mno?
16 Basi, mtakubali kwamba sikuwa mzigo kwenu. Lakini labda
mtu mwingine atasema: "Kwa vile Paulo ni mwerevu, amewafanyieni
ulaghai."
17 Je, mimi niliwanyonyeni kwa njia ya mjumbe yeyote niliyemtuma
kwenu?
18 Mimi nilimwita Tito, nikamtuma kwenu na ndugu yetu
mwingine. Je, Tito aliwanyonyeni? Je, hamjui kwamba sisi tumekuwa tukiongozwa
na roho yuleyule, na mwenendo wetu ni mmoja?
19 Labda mnafikiri kwamba mpaka sasa tumekuwa tukijitetea
wenyewe mbele yenu! Lakini, tunasema mambo haya mbele ya Mungu, tukiwa
tumeungana na Kristo. Mambo hayo, yote, wapenzi wangu, ni kwa ajili ya
kuwajenga ninyi.
20 Naogopa, huenda nitakapokuja kwenu nitawakuta katika
hali nisiyopenda, nami itanilazimu kuwa katika hali msiyoipenda. Naogopa huenda
kukawa na ugomvi, wivu, uhasama, ubishi, masengenyano, kunong`ona, majivuno na
fujo kati yenu.
21 Naogopa huenda hapo nitakapokuja safari ijayo Mungu wangu
atanifanya niaibike mbele yenu, nami nitaomboleza kwa ajili ya wengi wa wale
waliotenda dhambi lakini hawakujutia huo uchafu, tamaa zao mbaya na uzinzi
waliokuwa wamefanya.
|